Mkutano Mkuu
Je, Mwokozi Amefanya Nini kwa ajili Yetu Sisi?
Mkutano mkuu wa Aprili 2021


Je, Mwokozi Amefanya Nini kwa ajili Yetu Sisi?

Yeye Kristo amefanya kila kitu ambacho ni muhimu kwa ajili ya safari yetu hapa duniani kuelekea kudura iliyoelezwa katika mpango wa Baba yetu wa Mbinguni.

Katika jioni ya Jumamosi moja ya mkutano wa kigingi miaka mingi iliyopita, nilikutana na mwanamke mmoja aliyesema marafiki zake wamemwomba arudi kanisani baada ya miaka mingi ya kutokuhudhuria kikamilifu, lakini yeye hakuweza kufikiria sababu yoyote ya kwa nini anafaa kurudi. Ili kumtia moyo, nilimwambia, “Unapofikiria mambo yote ambayo Mwokozi ameyafanya kwa ajili yako, unakuwa na sababu nyingi za kukufanya urudi kumwabudu na kumtumikia.” Nilistaajabu alipojibu, “Yeye amefanya nini kwa ajili yangu mimi?”

Picha
Ujio wa Pili

Je, Yesu Kristo amefanya nini kwa ajili ya kila mmoja wetu? Yeye amefanya kila kitu ambacho ni muhimu kwa ajili ya safari yetu hapa duniani kuelekea kudura iliyoelezwa katika mpango wa Baba yetu wa Mbinguni. Nitaongelea sehemu muhimu kuu nne za mpango huo. Katika kila moja ya hizi Mwanaye wa Pekee, Yesu Kristo, ndiye mtu kitovu. Chenye kutia hamasa kati ya yote haya ni “upendo wa Mungu, ambao unaenea wenyewe kila mahali katika mioyo ya watoto wa watu; kwa sababu hii, ni wakupendeza zaidi ya vitu vyote” (1 Nefi 11:22).

I.

Kabla tu ya Jumapili ya Pasaka, ni wakati muafaka kuongelea kwanza juu ya Ufufuko wa Yesu Kristo. Ufufuko kutoka kwa wafu ni hakikisho binafsi la nguzo ya imani yetu. Linaongeza maana kwenye mafundisho yetu, hamasisho kwenye tabia zetu, matumaini kwa siku zetu za baadae.

Kwa sababu tunaamini katika maelezo ya Biblia na Kitabu cha Mormoni juu ya Ufufuko halisi wa Yesu Kristo, tunakubali mafundisho mengi ya kimaandiko kwamba ufufuko wa aina hiyo hiyo utakuja kwa wote wenye mwili ambao wamewahi kuishi juu ya dunia hii.1 Kama Yesu alivyofundisha, “Kwa sababu Mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai” (Yohana 14:19). Na Mitume Wake walifundisha kwamba “wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu” na “mwili huu wa kufa utakapovaa kutokufa” (1 Wakorintho 15:52, 54).

Picha
Ufufuko

Lakini Ufufuko unatupatia sisi zaidi ya uhakikisho huu wa kutokufa. Unabadilisha namna tunavyoyatazama maisha katika mwili wenye kufa.

Ufufuko unatupa mtazamo na nguvu ya kuvumilia changamoto za kidunia zinazomkabili kila mmoja wetu na wale tunaowapenda. Unatupatia namna mpya ya kuyatazama mapungufu ya kimwili, kiakili, au kihisia tuyapatayo wakati wa kuzaliwa au tuyapatayo katika maisha yetu ya duniani. Unatupa nguvu ya kuvumilia huzuni, kushindwa, na kukatishwa tamaa. Kwa sababu kila mmoja wetu anao uhakikisho wa uhakika wa ufufuko, tunajua kwamba kasoro hizi za kidunia na upinzani ni vya muda tu.

Ufufuko pia unatupatia sisi kichocheo chenye nguvu cha kushika amri za Mungu wakati wa maisha yetu ya hapa duniani. Tunapoamka kutoka kwa wafu na kusonga kwenye Hukumu yetu ya Mwisho, tunataka tuwe wenye kustahili baraka zilizo bora zaidi zilizoahidiwa kwa viumbe vitakavyofufuka.2

Picha
Tunaweza kuishi kama familia milele.

Kwa kuongezea, ile ahadi kwamba Ufufuko unaweza kujumuisha fursa ya kuwa pamoja na wanafamilia—mume, mke, watoto, wazazi, na ukoo—ni himizo lenye nguvu la kutimiza majukumu yetu ya kifamilia hapa duniani. Pia inatusaidia sisi kuishi pamoja katika upendo kwenye maisha haya na inatufariji katika kifo cha wapendwa wetu. Tunajua kwamba kutengana kwetu hapa duniani ni kwa muda tu, na tunatarajia kuungana tena na kuendeleza uhusiano wetu siku za baadae. Ufufuko unatupatia matumaini na nguvu ya kuwa wavumilivu wakati tukingojea. Pia unatuandaa sisi kwa ujasiri na heshima ya kukabiliana na mauti yetu sisi wenyewe—hata kwa kifo cha kabla ya wakati wake.

Mambo haya yote juu ya Ufufuko ni sehemu ya jibu la kwanza la swali “Yesu Kristo amefanya nini kwa ajili yangu mimi?”

II.

Kwa wengi wetu, fursa ya kusamehewa dhambi zetu ndio maana muhimu ya Upatanisho wa Yesu Kristo. Katika kuabudu, kwa unyenyekevu tunaimba:

Damu yake ya thamani yeye aliimwaga kwa hiari;

Uhai Wake aliutoa kwa hiari,

Dhabihu ya asiye na dhambi kwa ajili ya wenye hatia,

Aokoe ulimwengu.3

Mwokozi na Mkombozi wetu aliteseka mateso tusiyoweza kuelewa ili awe dhabihu kwa dhambi za wenye mwili wote ambao wangetubu. Dhabihu hii ya kulipia dhambi ilitoa kudura njema, mwanakondoo safi asiye na doa, kwa ajili ya uovu, dhambi za ulimwengu mzima. Ilifungua mlango kwa ajili ya kila mmoja wetu sisi kuoshwa dhambi zetu binafsi ili tuweze kukubaliwa tena kuingia katika uwepo wa Mungu, Baba wetu wa Milele. Mlango huu ulio wazi unapatikana kwa watoto wote wa Mungu. Katika kuabudu, tunaimba:

Nashangaa kwamba angeweza kushuka kutoka kwenye kiti cha uungu

Kuokoa nafsi asi sana na yenye kiburi kama yangu,

Kwamba atoe upendo wake mkuu kwa mtu kama mimi.4

Matokeo mazuri kabisa na yasioeleweka ya Upatanisho wa Yesu Kristo yanategemea upendo wa Mungu kwa kila mmoja wetu. Huthibitisha tamko Lake kwamba “thamani ya nafsi”—ya kila mmtu—“ni kubwa mbele za Mungu” (Mafundisho na Maagano 18:10). Katika Biblia, Yesu Kristo alielezea hili katika maneno ya upendo wa Baba yetu wa Mbinguni: “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele” (Yohana 3:16). Katika ufunuo wa siku hizi Mkombozi wetu Yesu Kristo alitamka kwamba Yeye “aliupenda ulimwengu hata akautoa uhai wake mwenyewe, kwamba wale wote watakaoamini waweze kuwa watoto wa Mungu” (Mafundisho na Maagano 34:3).

Je! inashangaza, hata kwamba Kitabu cha Mormoni: Ushuhuda Mwingine wa Yesu Kristo huhitimisha kwa mafundisho kwamba ili tuweze “kukamilishwa” na “kutakaswa katika Kristo” sisi lazima “tumpende Mungu kwa moyo, akili, na nguvu [zetu] zote”? (Moroni 10:32–33). Mpango Wake unaohamasishwa kwa upendo ni lazima upokelewe kwa upendo.

III.

Je, ni kitu gani kingine Mwokozi wetu Yesu Kristo amefanya kwa ajili yetu sisi? Kupitia mafundisho ya mitume Wake na kupitia huduma Yake binafsi, Yesu alitufundisha mpango wa wokovu. Mpango huu unajumuisha Uumbaji, kusudi la maisha, umuhimu wa upinzani, na zawadi ya haki ya kujiamulia. Yeye pia alitufundisha amri na maagano ambayo ni lazima tutii na ibada ambazo lazima tuzipitie ili ziturudishe kwa wazazi wetu wa mbinguni.

Picha
Mahubiri ya Mlimani

Katika Biblia, tunasoma mafundisho Yake: “Mimi ni nuru ya ulimwengu: yule ambaye ananifuata mimi hatatembea gizani, bali atapata nuru ya uzima” (Yohana 8:12). Na katika ufunuo wa leo tunasoma, “Tazama, Mimi ni Yesu Kristo, … nuru ambayo haiwezi kufichika gizani” (Mafundisho na Maagano 14:9). Kama tunafuata mafundisho Yake, Yeye anaiangaza njia yetu katika maisha haya na kuhakikisha hatima yetu katika ulimwengu ujao.

Kwa sababu anatupenda sisi, Anatupatia changamoto ya kufokasi Kwake Yeye na siyo juu ya mambo ya ulimwengu huu wenye kufa. Katika mahubiri Yake makuu juu ya mkate wa uzima, Yesu alifundisha kwamba hatupaswi kuwa miongoni mwa wale ambao huvutiwa sana na mambo ya ulimwengu—mambo ambayo husaidia maisha ya duniani lakini hayatoi lishe kuelekea uzima wa milele.5 Kama vile Yesu alivyotualika sisi tena na tena na tena, “Unifuate.”6

IV.

Kwa kumalizia, Kitabu cha Mormoni kinatufundisha kwamba kama sehemu ya Upatanisho Wake, Yesu Kristo “aliteseka maumivu na masumbuko na majaribu ya kila aina; na hii kwamba neno litimizwe ambalo linasema atabeba maumivu na magonjwa ya watu wake” (Alma 7:11).

Kwa nini Yeye apitie hizi changamoto za maisha ya duniani za “kila aina”? Alma alielezea kwamba “Na atajichukulia unyonge wao, ili moyo wake ujae rehema, kulingana na mwili, ili ajue kulingana na mwili, jinsi ya kuwasaidia watu wake kulingana na unyonge wao” (Alma 7:12).

Picha
Kristo katika Gethsemane

Mwokozi wetu anahisi na anajua majaribu yetu, masumbuko yetu, shida zetu, na kuteseka kwetu, kwani Yeye kwa hiari aliyapitia yote kama sehemu muhimu ya Upatanisho Wake. Maandiko mengine yanathibitisha hili. Agano Jipya linatangaza, “na kwa kuwa mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wao wanaojaribiwa” (Waebrania 2:18). Isaya anafundisha, “Usiogope; kwa maana mimi ni pamoja nawe: … nitakutia nguvu; naam, nitakusaidia” (Isaya 41:10). Wale wote wanaoteseka kwa aina yoyote ya udhaifu wanapaswa kukumbuka kwamba Mwokozi wetu pia alipitia aina hiyo ya maumivu na kwamba kupitia Upatanisho Wake anampatia kila mmoja wetu nguvu ya kuvumilia.

Nabii Joseph Smith alifupisha yote haya katika Makala ya tatu ya Imani yetu: “Tunaamini kwamba kwa njia ya Upatanisho wa Kristo, wanadamu wote wanaweza kuokolewa, kwa kutii sheria na ibada za Injili” (Makala ya Imani 1:3).

“Yesu Kristo amefanya nini kwa ajili yangu mimi?” dada yule aliuliza. Chini ya mpango wa Baba yetu wa Mbinguni, “Yeye aliumba mbingu na dunia” (Mafundisho na Maagano 14:9) ili kila mmoja wetu aweze kupitia maisha ya duniani yaliyo muhimu katika kutafuta hatima yetu ya kiungu. Kama sehemu ya mpango wa Baba, ufufuko wa Yesu Kristo ulishinda mauti ili kumthibitishia kila mmoja wetu kutokufa. Dhabihu ya Yesu Kristo ya kulipia dhambi inampatia kila mmoja wetu fursa ya kutubu dhambi zetu na kurudi nyumbani kwetu mbinguni tukiwa wasafi. Amri Zake na maagano hutuonyesha njia, na ukuhani wake hutupa mamlaka ya kufanya ibada ambazo ni muhimu ili kufika kwenye hatima yetu. Na mwokozi wetu kwa hiari alipitia maumivu na udhaifu wote wa mwili wenye kufa ili ajue jinsi ya kutuimarisha katika mateso yetu.

Picha
Yesu Kristo

Yesu Kristo alifanya haya yote kwa sababu Yeye anawapenda watoto wote wa Mungu. Upendo ndio kichocheo cha haya yote, na ilikuwa hivyo kutoka mwanzo kabisa. Mungu ametuambia katika ufunuo wa sasa kwamba “alimuumba mtu … mwanaume na mwanamke kwa mfano wake … na akawapa wao amri kwamba wanapaswa kumpenda na kumtumikia yeye” (Mafundisho na Maagano 20:18–19).

Ninashuhudia juu ya haya yote na kuomba kwamba sote tutakumbuka kile ambacho Mwokozi wetu amekifanya kwa kila mmoja wetu na kwamba sisi sote tutampenda na kumtumikia Yeye, katika jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha