Liahona
Ujasiri wa Kushiriki Kitu Ninachokithamini Zaidi
Julai 2024


“Ujasiri wa Kushiriki Kitu Ninachokithamini Zaidi,” Liahona, Julai 2024.

Ujasiri wa Kushiriki Kitu Ninachokithamini Zaidi

Nikifuata mfano wa askofu wangu na mke wake, nilikuwa na lengo la kushiriki Kitabu cha Mormoni kwenye kila safari ya kuongoza ushangiliaji niliyoifanya.

Picha
msichana akionyesha kwenye ukurasa katika kitabu kilichoshikiliwa na mvulana.

Wakati nikikua, nilipenda kuangalia jinsi kuku wa Bibi walivyokuwa wakikusanya pamoja vifaranga vyao chini ya mbawa zao wakati wa mvua kubwa ili kuwaweka salama na kuwalinda. Picha hii ilikuja kuwa muhimu sana kwangu baada ya kusoma kuhusu hilo katika Kitabu cha Mormoni (ona 3 Nefi 10:4–6). Kama kijana mkubwa, askofu wangu na mke wake, ambao walisafiri sana kwa ajili ya biashara yao, waliniambia kwamba walishiriki Kitabu cha Mormoni na mtu katika kila safari yao waliyoifanya.

Hiyo ilinivutia. Nilivutiwa nao, na mfano wao uligusa moyo wangu. Niliamua kwamba kama nitapata nafasi ya kusafiri nje ya Utah, Marekani, ningefuata mfano wao na kushiriki Kitabu cha Mormoni kila wakati nikisafiri.

Kama kiongozi wa washangiliaji wa Chuo Kikuu cha Brigham Young, nilisafiri mara kwa mara na timu ya ushangiliaji. Kabla ya safari yangu ya kwanza, nilinunua Kitabu cha Mormoni na nikaandika ushuhuda wangu ndani yake. Nilitaka kukuza ujasiri wa kushiriki kitu nilichokithamini zaidi kwa watu wengine: ushuhuda wangu na Kitabu cha Mormoni. Nilitaka kuwa kama askofu wangu na mke wake. Nilitaka niwe kama Yesu Kristo. Nilitaka kusaidia kuwakusanya wengine na kuwasaidia waje kwa Kristo.

Kwa haraka nilijifunza kwamba kama nitasali kabla ya kila safari ili niongozwe kwa mtu aliyekihitaji, mtu angejionyesha katika wakati sahihi na mahali sahihi kwangu mimi ili kufanya kushiriki Kitabu cha Mormoni kuwa rahisi na kawaida. Kadiri nilivyoendelea kufanya mazoezi, ndivyo rahisi zaidi ilivyokuwa kushiriki kwangu. Safari zangu zikawa za maana zaidi kwangu. Daima nilisisimka kupata mpokeaji ambaye Baba wa Mbinguni alimbariki kwa ushuhuda huu mtakatifu juu ya Kristo.

Niliposafiri, nilitafakari, “Niende wapi kupata mtu ambaye Baba wa Mbinguni amemtuma kwangu kwa wakati huu? Ninaweza kusema nini kwake ili kumwambia jinsi gani Kitabu cha Mormoni kilivyo cha thamani kwangu?” Mawazo na matendo yangu yakawa yamefokasi zaidi nje ya mahitaji na burudani yangu mimi mwenyewe, na nilihisi ongezeko la upendo kwa kila mtu niliyekutana naye. Nilijaribu kuwatazama kupitia macho ya Mwokozi. Nilisali kwa ajili yao ili wapokee zawadi hii ya kiungu ambayo Baba wa Mbinguni amenituma mimi niwape.

Nilihuzunika mwaka wangu wa mwisho ulipokuja kumalizika. Kuwa kiongozi wa ushangiliaji kwa BYU ilikuwa ndoto yangu ya maisha yote. Ningefurahia tukio la kupendeza la kushangilia bila kujali chochote, lakini fursa ya kushiriki Kitabu cha Mormoni katika kila safari ya kuongoza kushangilia lilistawisha maisha yangu katika njia za kupendeza na zisizotarajiwa.

Kushiriki Kitabu cha Mormoni ilikuwa njia ya thamani na rahisi ya kuongeza tabaka la ziada lenye maana kwenye uzoefu wangu wa chuo kikuu. Ninajua kwamba watu ambao nimeshiriki nao Kitabu cha Mormoni walikuwa wameongozwa mahususi ili kukipokea. Pia najua kwamba kwenye mfumo huu wa kushangaza wa maisha yangu, Baba wa Mbinguni alifuma upendo mwororo na wa kupendeza: Aliniruhusu niuhisi upendo Wake kwa watoto Wake katika njia maalumu kwa kila safari niliyoifanya.

Baada ya kuhitimu, niliamua siku zote kuendelea kutafuta mtu ambaye ninaweza kumtolea ushuhuda wangu. Baada ya muda, nilikuwa nimekuza uwezo mkubwa na faraja kwa kutoa ushuhuda wangu. Nilijifunza kutoogopa tena kuushiriki. Ninaamini kila mmoja anaweza kuwa na faraja zaidi kushiriki ushuhuda wake kwa kufanya mazoezi na kwa kuomba msaada wa kiungu.

Kuchagua kufuata mfano wa askofu wangu mwema na mke wake kulifanya maisha yangu kuwa na maana zaidi katika njia nyingi. Ilinifundisha kuona kwamba Bwana anamjua kila mmoja wa watoto Wake. Anatupenda na ana hamu ya kutukusanya wote chini ya mbawa Zake. Ni baraka iliyoje kuelewa picha hii ya kupendeza ambayo anaitumia wakati anapoelezea kukusanya Kwake. Yeye anatukusanya sisi kama kuku akusanyavyo na kwa upendo anavilinda vifaranga vyake.

Mwandishi anaishi Utah, Marekani.

Chapisha