Liahona
Usikose Misheni za Wakubwa
Julai 2024


“Usikose Misheni za Wakubwa,” Liahona, Julai 2024.

Kuzeeka kwa Uaminifu

Usikose Misheni za Wakubwa

Maagano yetu yanatualika kuhudumiana, kusimama kama mashahidi wa Mungu na kuwafariji wale wanaohitaji faraja. Kuhudumu kama wamisionari wakubwa ni njia mojawapo ya kutimiza mialiko hii, kubariki maisha yetu sisi wenyewe na ya wale tunaowahudumia.

Picha
wamisionari wanandoa wakiharakisha kupanda ndege

Kuna wamisionari wakubwa 34,000 wanaohudumu au walio kwenye misioni za huduma sasa hivi ambao, kama wale wenzao vijana, wanapata shangwe katika safari hiyo. Waseja na wanandoa wanaweza kuhudumu kama wamisionari katika kazi mbalimbali.

Na mahitaji ni ya muhimu. Katika mkutano mkuu wa Oktoba 2023, Mzee Ronald A. Rasband wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili aliwahimiza waumini wenye umri mkubwa kufikiria misioni za wakubwa. Aliuliza: “Mnafanya nini katika hatua hii ya maisha?’ Kuna njia nyingi sana wamisionari wakubwa wanaweza kufanya kile ambacho hakuna mtu mwingine anaweza kukifanya. Ninyi ni nguvu ya ajabu kwa ajili ya wema, mlioandaliwa katika Kanisa, na mko tayari kuwatia moyo na kuwaokoa watoto wa Mungu.”

Akielezea jinsi wamisionari wakubwa wanavyoitwa, Rais Russell M. Nelson alisema: “Fursa za wamisionari wakubwa zinatofautiana na ni pana. Miito yao ya kuhudumu hutolewa kwa utaratibu baada ya tafakuri ya sala na kulingana na historia ya shughuli za kazi katika maisha, uzoefu wa lugha na uwezo binafsi. Kati ya sifa zote za kuhudumu, ni hamu ya kuhudumu inaweza kuwa jambo la maana zaidi.” Pia alielezea michango ya wamisionari wakubwa kama “isiyo na mbadala.”

“Baadhi ya wamisionari wakubwa hufanya kazi katika ofisi ya misheni au na BYU–Pathway au miradi ya huduma za kibinadamu ambayo ina muundo ulioainishwa vyema sana,” mmisionari mkubwa alisema. “Sisi tumehudumu misioni kadhaa za aina hiyo. Hivyo, kidogo hatukuwa na uhakika tulipoitwa kwenye misioni ya MLS (msaada kwa viongozi na waumini). Mara tulipoanza, hakika tulipenda mnyumbuliko na ubunifu ambao misioni ya aina hiyo ulitupatia ili kuweza kuwatembelea waumini na kuimarisha matawi ya eneo hilo.”

Dada mkubwa anayehudumu katika kituo cha wageni alisema, “Wakati mume wangu alipofariki, sikuwa na uhakika nifanye nini kwa muda wangu. Sasa nina mambo ya kufanya, mahali pa kwenda, watu wa kuwaona. Ninao watu wanaonitegemea.”

“Hakuna haja ya kuwa na hofu hata kama hukuhudumu wakati ukiwa kijana,” dada mmoja alisema baada ya kurejea nyumbani kutoka misioni ya wakubwa. “Ni kazi mpya kwa kila mmoja. Sote tulijifunza pamoja kumtegemea Bwana kama vile tulivyotegemeana sisi kwa sisi na kuona kwamba ‘kutokana na vitu vidogo na rahisi mambo makubwa yalifanyika’ [Alma 37:6].”

Baraka kwa ajili ya Wamisionari

Misheni za wakubwa zinatofautiana kama vile wamisionari wakubwa. Kuna aina zote—kila moja na changamoto zake, shangwe na faida binafsi. Lakini kuna machache yanayofanana kwa kila aina ya misioni za wakubwa: kujifunza maandiko kwenye maana, sala za mara kwa mara na za dhati, kujiingiza kwenye huduma, mwongozo endelevu wa Roho Mtakatifu, fursa ya kipekee ya kuleta utofauti.

“Sijawahi kuhisi kuwa karibu zaidi na Bwana kuliko wakati tulipokuwa tukihudumu kama wamisionari wakubwa,” mmisionari mkubwa alisema. “Nilijua baadhi ya vitu vilikuwa nje ya udhibiti wangu, hususani nyumbani na watoto na wajukuu. Hivyo niliyaweka mambo hayo mikononi mwa Bwana. Na akaibariki familia yetu. Hatukuwa karibu zaidi na wajukuu wetu zaidi ya kuwatembelea kila wiki kwa njia ya Zoom. Tulizungumza kuhusu mambo ambayo kamwe hawangeyapenda kabla. Wakati haitokei kwa kila mmoja, katika hali yetu, mwana wetu mmoja alirejea Kanisani wakati tukihudumu, na mwana wetu mwingine akaoa tena na baadaye kuunganishwa hekaluni.”

Mmisionari mwingine mkubwa alisema, “Kujifunza kwetu maandiko matakatifu kama wenzi kukawa kwa maana zaidi kwa sababu tulikuwa tukitafuta njia za kuyatumia maandiko, siyo tu kuyasoma. Sikuwa tu nikienda kwa ajili ya ‘idadi ya kilomita,’ kama nilivyokuwa nimefanya hapo awali. Katika huduma yetu, ilionekana kwamba mara kwa mara nilikuwa nikirejelea maandiko tuliyoyasoma siku hiyo au wiki hiyo, hivyo nilianza kutegemea kutumia maandiko ya hivi karibuni niliyoyasoma kila siku. Niliacha kuwa mzembe katika kujifunza kwangu maandiko, nikitegemea kwamba ningerejelea kitu fulani nilichokisoma siku hiyo.

“Kuhudumu misioni kumenipa mkataba mpya wa kupanga katika maisha,” dada mkubwa alisema. “Kumenipatia dhumuni lenye maana, dhamira mpya ya kuishi na kitu cha kufanya zaidi ya kucheza golfu au kulea wajukuu.”

“Huduma ni mtaa wenye njia mbili,” mmisionari mkubwa mwingine alieleza. “Tulipofikiria—kidogo kuhusu kimbelembele chetu—kuhusu kiasi gani tulikuwa tukiwafanyia watu wengine, hatukufanikiwa sana. Lakini tulipotambua kiasi gani tulikuwa tunajifunza na kukua sisi wenyewe, siyo tu tulibadilika bali wengine pia walionekana kupenda zaidi katika kile tulichokuwa tukikisema na kukifanya. Tunatupa mkate wetu kwenye maji, na ilionekena kana kwamba ulirudishwa ukiwa umepakwa siagi.”

Uhusiano Imara

Watu wanapohudumu kama wamisionari wakubwa, wanakuza uhusiano wa kina ambao utadumu maisha yote. Wengi wanakua karibu zaidi na watu wanaowahudumia. Pia wanajenga uhusiano imara na wamisionari wengine na viongozi wenyeji. “Sisi tulijenga urafiki na wamisionari vijana, wanandoa wengine na watu ambao kamwe tusingekutana nao kama tungekaa nyumbani,” mmisionari mkubwa mmoja alisema. “Bado tunawasiliana. Wakati nilipodhani kila siku ingekuwa sawa, kwenda misioni kumenipa mwanzo mpya na marafiki wapya wa kushiriki safari pamoja nasi.”

Misheni za wakubwa zinaweza kuwasaidia wanandoa waimarishe ndoa zao pia. Watu wanapostaafu au kupunguza saa za kufanya kazi, wanandoa wanaweza kupata uhitaji wa kufikiri upya dhumuni lao la pamoja kwa vile yawezekana hawana watoto wa kuwalea katika nyumba yao. Yawezekana kuwa wamezoea kuwa katika himaya yao wenyewe na ratiba zao. Uzee au kustaafu vinaweza kubadilisha hilo. Kuanza upya, kushiriki uzoefu wa pamoja, iwe kuhudumu kutoka nyumbani au muda wote kwenye misioni za wakubwa, kunaweza kusaidia kujenga dhumuni jipya kwa wanandoa na kuimarisha kutegemeana kwao.

“Kuna msemo wa kale unaosema kwamba katika kustaafu ‘unapata nusu ya pato na mara mbili ya mume wako kama mwanzoni,’” dada mmoja alisema huku akicheka. “Kuhudumu misioni katika mahali mbali na nyumbani kulituruhusu sisi kuzungumzia mabadiliko haya katika njia ambayo kamwe tusingefanya kabla ya misioni yetu. Baada ya mume wangu kustaafu, tuliumia tu ndani ya mioyo yetu wakati tulipokuwa na mzozo wowote. Sasa, badala ya kwenda njia yetu na kupuuziana, hatutaki kuwa na matokeo hasi kwenye kazi ya Bwana, hivyo tunazungumzia lile linalotusumbua.”

“Mimi na mke wangu tulianza kuzungumza kila usiku kuhusu huruma nyororo tuliyokuwa nayo kila siku wakati tukihudumu misioni yetu,” mmisionari mkubwa mmoja alisema. “Siyo tu ilitusaidia tufokasi zaidi juu ya kile kilichotokea na kufokasi kidogo juu yetu wenyewe, lakini pia ilitupatia nafasi ya kuuona wema uliotuzunguka hata wakati ambapo vipengele vya siku hiyo havikwenda vyema.”

“Na kwa sababu ndicho kilikuwa kitu cha mwisho tulichofanya kila usiku,” mke wake aliongeza, “tulienda kitandani tukiwa tumeondoa msongo wa mawazo na tumeridhika zaidi kuliko tulivyokuwa kwa miaka mingi. Ilinisaidia mimi kulala vizuri zaidi!”

Baraka kwa Wale Wanaohudumu

Maisha yana milima na mabonde—siku nzuri na siku mbaya. Hivyo hudumu misioni. Lakini kumtumikia Bwana kuna thawabu nyingi za ndani, siyo tu baada ya kumalizika kwa misioni bali wakati wa misioni vile vile. Kama vile binamu Modekai alivyosema kwa Esta, “walakini ni nani ajuaye kama wewe hukuujia ufalme kwa ajili ya wakati kama huu?” Esta 4:1; msisitizo umeongezwa). Wakitazama nyuma kwenye huduma yao, wamisionari wakubwa wengi wamehisi walikuwa wamepangiwa kufanya kazi au kwenye eneo ambalo kipekee walistahili kujaza hitaji maalumu.

Nimeshuhudia kwa macho yangu wema wenye nguvu ambao wanandoa wamisionari wakubbwa wanaweza kufanya wakati nikiishi huko Lousiana, Marekani. Mara tu baada ya kuitwa kuhudumu katika baraza kuu la Kigingi cha New Orleans Louisiana, nilipangiwa kusaidia Tawi la Port Sulphur. Kulikuwa na akina kaka wenye ukuhani wachache tu waliokuwa wakishiriki kikamilifu. Nafasi nyingi za kufundisha na uongozi zilijazwa na wanawake ambao waume zao hawakuwa waumini. Mara chache, wamisionari wakubwa au viongozi wa kigingi walipangiwa kwenye tawi, lakini walikuwa na mafanikio kidogo katika kuwafikia waumini hawa ambao si familia nzima walikuwa waumini.

Kisha wamisionari wanandoa kutoka Wyoming, Marekani, walipangiwa kusaidia tawi hilo. Walikuwa wamekuwa wakulima kwa miaka mingi na walifanya kazi katika kiwanda cha jibini jirani na nyumba yao. Kwa sababu ya historia yao ya nyuma na uzoefu, walihusiana kwa urahisi na watu wengi huko Port Sulphur ambao walifanya kazi katika kiwanda cha mafuta. Wanandoa wale wakubwa walitumia muda mwingi sana kujenga uhusiano na kuzihudumia familia ambazo baadhi tu ni waumini katika tawi. Kwa sababu ya huduma yao na upendo, wakati wa muda wao huko Port Sulphur kwa namna ya kipekee tawi liliimarishwa na kubarikiwa kupitia huduma yao ya uaminifu. Wanaume kadhaa kutoka familia hizi ambazo baadhi si waumini walijiunga na Kanisa, wakaimarisha akidi za wazee na tawi.

Wamisionari wakubwa wanabariki maisha—yao wenyewe na pia ya wengine’. Usikose fursa hii ya kupendeza ya kuhudumu na kukua!

Muhtasari

  1. Ronald A. Rasband, “Shangwe Yako Itakuwa Kuu Jinsi Gani,” Liahona, Nov. 2023, 53.

  2. Russell M. Nelson, “Wamisionari Wakubwa na Injili,” Liahona, Nov. 2004, 81.

  3. Russell M. Nelson, “Kuhubiri Injili ya Amani,” Liahona, Mei 2022, 7.

  4. “Shangwe. Tumaini. Nguvu saidizi kutoka kwa Mungu. Kulindwa dhidi ya majaribu. Uponyaji. Hivi Vyote—na zaidi (ikijumuisha msamaha wa dhambi)—vinatonatona juu yetu kutoka mbinguni tunaposhiriki injili” (Marcus B. Nash, “Inua Juu Nuru Yako,” Liahona, Nov. 2021, 72).

Chapisha