Liahona
Ujumbe Wangu kutoka kwa Mungu
Julai 2024


“Ujumbe Wangu kutoka kwa Mungu,” Liahona, Julai 2024.

Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho

Ujumbe Wangu kutoka kwa Mungu

Sikuwa na ushuhuda juu ya Kitabu cha Mormoni hadi Bwana aliposema nami kupitia kitabu cha Helamani.

Picha
mwanamume akitabasama huku mikono ameikunja

Picha kwa hisani ya mtunzi

Wakati rafiki aliponialika kwenye Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho mwaka 2020, nilikubali kwa shingo upande. Mwanzoni, sikujisikia kama palikuwa mahali pa kwenda, lakini niliendeea kuhudhuria mkutano wa sakramenti. Mwishowe, nilibatizwa.

Sikuwa nimeelewa, hata hivyo, wazo la kuwa na ushuhuda kama lilivyosemwa na waumini wengine wa Kanisa. Akina dada wamisionari na mimi tulisoma baadhi ya mistari ya maandiko pamoja, lakini kamwe sikuwahi kufunua Kitabu cha Mormoni peke yangu. Licha ya juhudi kubwa za waumini wa Kanisa kunikaribisha na kunifanya niwe mshiriki anayehudhuria kikamilifu, punde nikaanza kuja Kanisani kwa kuchelewa, kutofika kwenye baadhi ya mikutano, na kurudi nyuma kwenye hali ya ulimwengu.

Ndipo siku moja ikafika wakati nilipohisi hali fulani na moyo kutatizika. Nilihisi nimekuwa kigeugeu, wa kiulimwengu zaidi, na mpinzani wa mambo ya Mungu. Nilitambua kwamba sikuwa kwenye njia sahihi. Nikiwa katika hali hiyo, nilitupa jicho kwenye maandiko yaliyokuwa juu ya kitanda changu.

Nilimlilia Mungu aseme kitu kwangu. Nilisema sala fupi na nikasubiri ili nisikie kitu chochote. Nilihitaji faraja na uwazi.

Halafu nikasiki kitu fulani. Sijui kama sauti ile ilikuja kutoka mawazoni mwangu au ndani ya masikio yangu, lakini nilisikia maneno “Helamani 3:27.” Nilijua kile kitabu cha Helamani kilikuwa katika Kitabu cha Mormoni, hivyo nilichukua maandiko na nikaenda kwenye ukurasa wa yaliyomo ili nikipate kitabu hicho.

Nilichokisoma hapo ulikuwa ujumbe kutoka kwa Mungu maalumu kwa ajili yangu kwa wakati huo katika maisha yangu, “Hivyo tunaweza kuona kwamba Bwana ana huruma kwa wote ambao, kwa uaminifu wa mioyo yao, wanaliitia jina lake takatifu.”

Kifungu hiki cha maneno kilibadilisha mtazamo wangu kuhusu matendo yangu na kuhusu Kitabu cha Mormoni. Nilitambua kwamba matendo yangu na kutokuwa kwangu kwa dhati kwa Mungu kumekuwa ni makosa na kwamba nilihitaji kumlilia Mungu na kutubu. Ninajua kwamba Mungu hataninyima rehema Zake na baraka ilimradi nikiwa kwa dhati naliitia jina Lake na kumfuata Yeye.

Hivyo ndivyo ushuhuda wangu juu ya Kitabu cha Mormoni ulivyokuja—kitabu ambacho sikuonyesha hamu ya kukisoma. Ninajua kwamba Mungu yu hai, kwamba Yeye anasema nasi leo, na kwamba Kitabu cha Mormoni ni cha kweli.

Chapisha