2021
Vaha’i Tonga
Julai/Agosti 2021


Waanzilishi katika Kila Nchi

Vaha’i Tonga

Mfano huko Tonga

Waandishi wanaishi Waikato, New Zealand na Utah, Marekani.

Vaha’i aliendelea kusali na siku moja mambo yakawa tofauti.

Picha
A group of Tongan Young Men

Vaha’i alipiga magoti kando ya kitanda chake kusali. Ulikuwa usiku wake wa kwanza kwenye shule ya bweni na alishiriki chumba na wavulana wengine wengi. Hakuna kati yao aliyekuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, kama yeye.

“Baba wa Mbinguni …” Vaha’i alianza kusali kimoyomoyo. Lakini haikuwa rahisi. Wavulana wengine walikuwa wakizungumza na kucheka kwa sauti.

“Tazama!” mmoja wa wenzake chumbani, Akau, alipaza sauti. “Anasali!”

Vaha’i alisonga kwa kutoridhika. Alijua kuwa Akau alikuwa akimfanyia mzaha. Lakini alijifanya kutomsikia. Aliendelea kusali.

Wakati Vaha’i alipojifunza kuhusu injili kwa mara ya kwanza, babu na bibi yake hawakuwa wamelipenda Kanisa pia. Vaha’i alikuwa amehudhuria Msingi na mjomba au marafiki zake.

Alipofikisha miaka 12, aliamua kubatizwa. Babu na bibi yake hawakufurahia sana mara ya kwanza. Lakini baadaye bibi yake akasema, “Kuanzia wakati huu na kuendelea, wewe ni muumini wa kanisa hilo. Tunataka uendelee kuwa mwaminifu.”

Sasa kwa kuwa Vaha’i hakuwa shuleni, alikuwa amenuia kufanya hivyo. Kwa hivyo, aliendelea kusali. Hata wakati wavulana wengine walipomfanyia mzaha.

Usiku mmoja wakati Vaha’i alipopiga magoti, akasikia kitu tofauti.

“Nyie, kaeni kimya! Vaha’i anasali,” mtu fulani alisema.

Vaha’i alikamilisha sala yake na akafungua macho yake.

Akau alikuwa amekaa kitandani pake. “Ni muhimu sana kwako, sivyo?”

Vaha’i alikubali kwa kichwa. “Ndiyo, ni muhimu.”

Baada ya hayo, wavulana wengine walikuwa kimya kila wakati Vaha’i aliposali. Punde Akau alianza kupiga magoti pamoja naye. Wavulana wengine wakajiunga pia. Baadaye, wavulana wote katika chumba wakapiga magoti kusali pamoja na Vaha’i kila usiku.

Vaha’i alifurahi sana. Hakuwahi kuwa na sala ya familia nyumbani. Lakini sasa angeweza kufanya sala ya familia na wanafunzi wenzake!

Siku moja Vaha’i alikuwa na wazo. Mkutano mkubwa wa Kanisa ulikuwa unakaribia. Angeweza kuwaalika marafiki zake!

Baada ya sala, Vaha’i alimwambia kila mtu kuhusu mkutano huo. “Unaitwa mkutano wa wilaya,” alisema. “Watu huja kujifunza kuhusu Yesu. Nyote mnakaribishwa, ikiwa mnataka!”

Kwa kuwa ingewabidi kuondoka shuleni kuhudhuria mkutano, kila mvulana alihitajika kutia saini karatasi ili kupata ruhusa. Vaha’i alishangaa sana alipoona karatasi. Kulikuwa na majina 77 kwenye orodha!

Moyo wa Vaha’i ulichangamka sana alipokaa na wanafunzi wenzake katika safu na kusikiliza hotuba kwenye mkutano. Akau na baadhi ya wengine lazima pia walihisi uchangamfu ndani ya mioyo yao. Mwishoni mwa mkutano, saba kati yao walitaka kubatizwa!

Usiku ule baada ya sala na marafiki zake, Vaha’i alisali sala yake. “Asante kwa kunibariki kwa marafiki wazuri,” alimwambia Baba wa Mbinguni. “Na kwa kunisaidia kuwa mfano mzuri.”

Tonga inaundwa na takribani visiwa 170 katika Bahari ya Pasifiki.

Leo, watu sita kati ya kumi huko Tonga ni waumini wa Kanisa.

Tonga pia inajulikana kama “Visiwa vya Kirafiki.”

Vaha’i na mkewe, Sela, walikuwa wanandoa wa kwanza kuunganishwa kwenye Hekalu la Hamilton New Zealand.

Alitumikia kama rais wa Hekalu la Nuku’alofa Tonga.

Alikuwa mwalimu kwenye Chuo cha Liahona, shule ya upili inayomilikiwa na Kanisa huko Tonga.

Picha
Friend, July 2021 Tier 2

Vielelezo na Susan Keeter

Chapisha