2019
Jinsi Nilivyojifunza Kujibu Wakati Mtu fulani Anapokiri Wanapambana na Ponografia
Oktoba 2019


Kidijitali Pekee: Vijana Wakubwa

Jinsi Nilivyojifunza Kujibu Wakati Mtu fulani Anapokiri Wanapambana na Ponografia

Mwandishi anaishi Utah, Marekani.

Nilijua kwa miezi kwamba kuna kitu kilichokuwa kinaendelea, lakini haikuwa mpaka wakati huu ambapo rafiki yangu alikiri ukweli kwangu: amekuwa akipambana na ponografia kwa miaka, kwa ujumla muda wote niliofahamiana naye.

Nikiwa nimekaa ndani ya gari nikisikiliza kuungama kwake, nilikuwa na shukrani. Usinielewe vibaya—inaumiza sana kujua amekuwa akipambana kwa muda mrefu bila mimi kujua—lakini nilikuwa na furaha nilikuwa mahali ambapo ningeweza kujibu kwa upendo badala ya kuhukumu.

Kutokuwa Mkarimu Daima Hakuhalalishwi

Wakati mwingine ufahamu kwamba ponografia ni uovu unaweza kuchuruzika kwenye mitazamo yetu kwa wengine. Ninajua ilikuwa hivyo kwangu wakati mmoja. Nilipokuwa mdogo, niliweza kusikia kuhusu watu ambao walipambana na ponografia na mjibizo wangu wa ndani ilikuwa hasira na hata maudhi. Lakini wakati rafiki yangu aliponiambia kuhusu mapambano yake, nilikuwa mahala pazuri kumfariji kwa sababu nilikuwa nimejenga uelewa zaidi wa dhambi na udhaifu wangu mwenyewe kwa miaka mingi.

Ninajua sasa kwamba kutokuwa mkarimu kamwe hakuhalalishwi. Yesu Kristo, ambaye ni mfano wetu mkamilifu, aliwatafuta watu ambao walikuwa wamedharauliwa na wengine. Yeye alizungumza pamoja na Wasamaria na wenye dhambi. Kristo, ambaye “hawezi kuiangalia dhambi na kuivumilia hata kidogo” (Mafundisho na Maagano 1:31), anatutazama “sisi, pamoja na mapungufu yetu, bila kurejea machukizo na maudhi.”1 Hivyo kuwa na mazungumzo hayo ya kina na rafiki yangu, nilijaribu kufikiria jinsi ambavyo Yesu angejibu. Hadithi ya mwanamke aliyeshikwa kwenye uzinzi ilinisaidia kujua jinsi ya kujibu.

Kujibu kwa Huruma

Wayahudi walioishi sheria ya Musa hawakuwa na huruma nyingi. Kulikuwa na adhabu maalumu, mara nyingi za kikatili, zilizotolewa kwa dhambi, na uzinzi ulihitaji kupigwa kwa mawe. Lakini wakati mzinzi alipoletwa kwa Yesu, Yeye hakuudhika—alimwonyesha huruma. Badala ya kuwapongeza washitaki kwa kumpata mtu aliyeshikwa kwenye tukio, Yeye aliwakumbusha washitaki juu ya dhambi zao wenyewe (ona Yohana 8:3–7). Hata hivyo, “wote tumetenda dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu” (Warumi 3:23). Kristo hakumhukumu mtenda dhambi, na sisi hatupaswi pia kufanya hivyo (ona Yohana 13:34–35).

Wakati washitaki walipoondoka, wakisutwa na dhamiri zao zenye hatia, Kristo alizungumza na mwanamke. Maneno yake yalikuwa machache lakini mazito. Kwanza Aliuliza, “Mwanamke, wako wapi washitaki wako? Je, hakuna aliyekutuhumu kuwa na hatia?” Na wakati alipojibu kwamba hawakuwepo, Yeye kwa urahisi alisema, “Wala mimi sikuhukumu: enenda zako; wala usitende dhambi tena” (Yohana 8:10–11).

Hukumu isingeweza kumsaidia mwanamke huyu kubadilika, lakini Mwokozi alijua kwamba upendo ungeweza.

Enenda zako, wala Usitende Dhambi Tena

Upendo kiurahisi ni hatua ya kwanza katika kumsaidia mtu kushinda ponografia. Mchakato wa uponyaji mara zote ni wa kipekee kama alivyo mtu binafsi, lakini kuna hatua za msingi ambazo kila mtu anayepambana anahitaji kuchukua. Wahimize kukutana na askofu wao; yeye atakuwa na rasilimali na nyenzo za kusaidia. Pale ambapo ni sahihi, wasaidie kutambua vichocheo na kutengeneza mpango wa kuwasaidia kuviepuka. Wahimize kumwona mtaalamu au kujiunga na kundi la kusaidia. Na endelea kuwapenda na kuwaunga mkono kila hatua wanayopitia.

Kristo alionyesha upendo kwa mwanamke na kuhakikisha kwamba mwanamke alijua kwamba Yeye hakumtaka kutenda dhambi tena. Hisani halisi haimaanishi kwamba tusitilie maanani makosa ya wengine; bali, inatusababisha sisi kuona uwezekano wao na kutuhimiza kuwasaidia kusonga mbele.

Safari ya Imani

Nilikuwa tayari nampenda rafiki yangu, lakini nilimpenda zaidi baada ya kufichua siri yake. Bila kujali kile wewe au mtu unayempenda amefanya, “Haiwezekani kwako kuzama chini zaidi ya kule nuru isiyokoma ya Upatanisho wa Kristo inapoangaza.”2

Ikiwa unamfahamu mtu anayepambana na ponografia, usikate tamaa juu yao! Fikia kwa upendo na huruma kama vile ambavyo Mwokozi angefanya. Haitakuwa rahisi daima; mapambano haya hayakomi kwa usiku mmoja. Kuwa na subira kwa wale uwapendao na kwako mwenyewe. Kujifunza kumpenda na kumuelewa mtu anayepitia jambo gumu si mara zote rahisi au ya kupendeza. Lakini ninaamini kwamba upendo wote tunaotoa hautakuwa bure, licha ya urefu au matokeo ya safari ya wapendwa wetu.

Muhtasari

  1. Dale G. Renlund, “Mchungaji Wetu Mwema,” Ensign au Liahona, Mei 2017, 30.

  2. Jeffrey R. Holland, “Wafanyakazi katika Shamba,” Ensign au Liahona, Mei 2012, 33.

Chapisha