2019
Kuwalinda Watoto
Oktoba 2019


Kuwalinda Watoto

Nini tunaweza kufanya ili kuwalinda vyema na kuwawezesha watoto katika maisha yetu?

Picha
mother with baby and crying child

Kielelezo cha Picha na Linda Lee

Kati ya makundi yote ya watu Yesu aliowafundisha, tunajua Aliwapenda hasa watoto. Aliwapa umakini watoto hata wakati hali haikuwa ya kufaa. Aliwaalika watoto kupokea baraka binafsi kutoka Kwake. Aliwashutumu wale waliowaumiza watoto. Na Alifundisha kwamba tunapaswa kuwa zaidi kama watoto ili kuingia ufalme wa mbinguni.1

“Tazama wachanga wenu,” Yeye aliwaambia wale waliokuwa bara la Amerika baada ya Ufufuo Wake. Mbingu zilifunguka, na malaika walinzi, wenye upendo waliteremka kutoka mbinguni na kuzunguka wale wachanga, na walizungukwa na moto. (Ona 3 Nefi 5:23–24.)

Pamoja na hatari zote ulimwenguni leo, tungetamani kuwa watoto wetu wangekuwa daima wamezungukwa na moto wa mbinguni. Inakadiriwa kuwa mmoja kati ya watu wanne ulimwenguni amenyanyaswa akiwa mtoto, na wastani huo unaongezeka unapotazama makundi ya waathirika, kama vile wale wenye ulemavu.2 Habari njema ni kwamba kuna mengi tunayoweza kufanya kuwa wenye kujihusisha kuhusu kuwalinda watoto.

“Pata taswira akilini mwako ya mtoto unayempenda,” alisema Rais Mkuu wa Msingi. “Unapomwambia mtoto huyu, ‘ninakupenda,’ hiyo ina maana gani? … Tunatoa ulinzi ili kwamba tuweze kuwasaidia wale tunaowapenda kuwa bora na kukabiliana na changamoto za maisha.”3

Pengine kutazama kwa karibu zaidi kwenye mfano wa Mwokozi kunaweza kuchochea mawazo kuhusu jinsi tunavyoweza kuwalinda vizuri watoto katika maisha yetu.

Yesu Alitenga Muda kwa Ajili Yao

Picha
Jesus with children

Tazama Wachanga Wenu na David Lindsley © 1983

Yesu alitenga muda kuwapa umakini watoto na wenye kuteseka (ona Mathayo 19:14). Sisi pia tunaweza kutenga muda kuwasikiliza watoto wetu na kujaribu kuelewa changamoto zao.

“Kadiri mtoto anavyohisi upendo mwingi, ndivyo inavyokuwa rahisi kwake kufunguka,” Dada Jones alisema. “… Sisi tunapaswa kuanzisha mazungumzo na si kusubiri watoto waje kwetu.”4

Mama mmoja aliona ni msaada kuwauliza watoto wake kila jioni, “Je, mlisikia maneno yoyote leo ambayo hamkuyaelewa?”

Silika ya kwanza ya watoto wetu inaweza kuwa kutazama mtandaoni kutafuta majibu kwa sababu mtandao unatoa msaada wa haraka na hauhukumu, lakini tunahitaji kuwashawishi kwamba sisi ni chanzo cha kuaminika zaidi cha taarifa. Na hilo linajumuisha kutokujibu kwa hasira wakati watoto wetu wanapotuambia kitu ambacho si cha kuleta hisia nzuri. Kwa mfano, ikiwa tumekuwa na hisia za hasira wakati mtoto wetu alipokiri kwamba wametafuta ponografia, wanaweza wasirudi kwetu tena kwa ajili ya usaidizi. Lakini ikiwa tutajibu kwa upendo, tuna fursa ya kutuma ujumbe wa wazi—kwamba tunawataka kuzungumza nasi kuhusu kitu chochote.

Dada Jones alisema, “Matatizo madogo yakizungumzwa katika njia ya upendo yanatengeneza msingi wa mjibizo wenye afya ili kwamba matatizo makubwa yanapokuja, mawasiliano yanaendelea kuwa wazi.”5

Baadhi ya mazungumzo ya muhimu, yenye ulinzi ambayo wazazi wanaweza kuwa nayo pamoja na watoto wao ni kuhusu miili yao. Mazungumzo haya yanajumuisha maneno sahihi ya sehemu za mwili, taarifa kuhusu usafi, na mabadiliko ya kutarajia katika miaka ya usoni. Tunapaswa kuzungumza kuhusu kujamiiana na jinsi vitendo vya kimapenzi vya kimwili na kihisia ni sehemu muhimu ya mpango wa Baba wa Mbinguni. Tungeweza pia kuzungumzia mada kama vile unyanyasaji na ponografia. Mazungumzo haya yanahitaji kuwa sahihi-kwa umri na yanayoongozwa na maswali waliyo nayo watoto wetu. Kwa hakika, tungekuwa na mazungumzo baada ya muda, tukiongeza taarifa pale watoto wetu wanapokua na ufahamu wao kuongezeka. (Ona mwisho wa makala hii kwa nyenzo zenye kutoa usaidizi.)

Yesu Aliweka Mfano kwa ajili Yetu

Yesu aliweka mfano mkamilifu kwa ajili ya kila mtu (ona Yohana 8:12). Kama watu wazima, tuna fursa na wajibu wa kuwa mifano. Moja ya njia bora ambazo kwazo tunaweza kuwasaidia watoto wetu kuwa salama ni kwa kufanya chaguzi salama sisi wenyewe. Watoto wanagundua jinsi wazazi wao wanavyowatendea wengine na wanavyowaruhusu wengine kuwatendea wao. Tafadhali, ikiwa upo katika mahusiano au unapambana na uraibu unaokuweka wewe na familia yako hatarini, pata msaada. Tafuta mamlaka za kiraia na wataalamu wa ushauri, vilevile askofu wako au rais wa Muungano wa Usaidizi wa akina Mama, ambao wanaweza kukuunganisha na nyenzo sahihi za Kanisa na jamii. Unastahili usalama na heshima.

Tunapaswa pia kuwa mfano wa kujali kwa ajili ya nguvu yetu ya kiroho. Je, watoto wetu wanatuona tukisali? Je, wanajua kuwa tunasoma maandiko? Je, wamewahi kusikia shuhuda zetu? Je tunavaa “silaha zote za Mungu” kama familia asubuhi kabla ya kutoka kwenda ulimwenguni? (ona Waefeso 6:11–18; Mafundisho na Maagano 27:15–18).

Yesu Alizungumza kwa ajili Yao

Mwokozi alizungumza dhidi ya wale waliowaumiza watoto (ona Mathayo 18:6). Sisi pia tunaweza kuwa mawakili kwa ajili ya watoto katika maisha yetu.

“Watoto wanahitaji wengine kuzungumza kwa ajili yao,” alifundisha Rais Dallin H. Oaks, Mshauri wa Kwanza katika Urais wa Kwanza, “na wanahitaji wafanya-maamuzi wanaoweka maslahi yao mbele ya maslahi ya kibinafsi ya watu wazima.”6

Wakati hatupaswi kuwa waoga kupitiliza au kuwa na mashaka juu ya wengine, tunapaswa kujua vitisho vinavyowezekana na kufanya maamuzi ya busara na salama. Viongozi wa msingi wanapaswa kufuata miongozo ya kuzuia-unyanyasaji7—kuna ulinzi kwenye kuwa na walimu wawili darasani na mtu kutoka kwenye urais akiangalia darasa.

Wazazi na viongozi wanapaswa kushauriana pamoja na kuamua ikiwa kuna tahadhari zaidi wanaweza kuchukua ili kupunguza vitisho mahususi. Kwa mfano, majengo mengi ya Kanisa yana madirisha kwenye milango ya madarasa. Ikiwa jengo lako halina, unaweza kufikiria kuacha mlango wazi kidogo wakati wa madarasa na kuzungumza na mwakilishi wako wa utawala wa-nyenzo katika eneo lako kuona ikiwa kuweka dirisha ni mbadala. Licha ya miito yao, watu wazima wote wanaweza kuweka umakini kanisani na kusaidia inapohitajika, kama vile kuwakaribisha wageni ambao wararandaranda ukumbini, au kumuhimiza mtoto anaezagaa nje kurudi darasani.

Kwa huzuni, wakati mwingine watoto wanaumizwa na watoto wenzao. Ikiwa tunatambua aina yoyote ya uonevu au mgusano wa kimwili usio sahihi kanisani au mahala popote, tunapaswa kuingilia kati haraka. Kama sisi ni viongozi, tunahitaji kuwa radhi kuzungumza na familia inayohusika—hata kama mazungumzo hayaleti hisia nzuri—kuhakikisha kwamba watoto wote wako salama. Zungumza kwa huruma na uwazi kusaidia kujenga utamaduni wa ukarimu.

Ikiwa tunaamini kwamba mtoto ananyanyaswa, tunapaswa kutolea taarifa wasiwasi huo kwa mamlaka ya kiraia mara moja. Katika nchi nyingi, simu za dharura zinapatikana ambazo hutoa huduma za kuingilia janga, taarifa, na msaada. Tunapaswa pia kumwambia askofu juu ya unyanyasaji unaodhaniwa, hasa unaomhusisha yeyote anayeweza kuwafikia watoto kupitia Kanisa. Kwa kuongezea kwenye kuchukua hatua kuzuia ufikiaji wa baadaye wa wakosaji kwa watoto, askofu anaweza kutoa faraja na msaada kwa wahanga na kuwasaidia kuunganika na nyenzo za ziada kutoka Huduma za Familia.

Yesu Aliwabariki Mmoja Mmoja

Picha
Primary teacher hugging child with Down syndrome

Kielelezo cha Picha na Shanea Janese Acebal

Yesu aliwajua na aliwabariki watoto mmoja mmoja (ona 3 Nefi 17:21). Vivyo hivyo, tunapaswa kumfahamu kila mtoto na kujaribu kumsaidia yeye mahususi.

Ni kwa jinsi gani tunaweza kufanya kanisa kuwa salama kwa ajili ya watoto wenye hali za tiba? Je, tuna mpango kwa ajili ya kuwasaidia watoto wa Msingi wenye ulemavu? Je, masomo ya Msingi tunayofundisha yanaangalia hali tofauti za nyumbani? Nini kingine tunaweza kufanya kuwa wenye kujihusisha zaidi?

Maoni ya kibaguzi, maneno ya kushusha hadhi kuhusu tamaduni zingine, na mitazamo ya kushutumu kwa waumini wa imani zingine vinapaswa kutokuwa na nafasi katika ujumbe tunaoshiriki. Katika darasa moja la msingi, mvulana hakuzungumza lugha vizuri kama watoto wenzake. Kumsaidia ahisi kukaribishwa, walimu walihakikisha wanachapisha vipeperushi katika lugha zote. Matendo rahisi ya kujali huwaonesha watoto kwamba tunawajua na tunawajali kibinafsi, na matendo haya yanaweza kuweka mfano kwa ajili yao kufuata.

Tunaweza kugundua kwamba baadhi ya watoto wanahitaji msaada katika njia ya dharura. Kwa mfano, japokuwa kuwa na sununu ni sehemu ya kawaida ya ukuaji, ikiwa mtoto ana hasira, anajitenga, au ana huzuni kwa wiki kadhaa, kunaweza kuwa na tatizo kubwa zaidi ambalo linahitaji msaada wa kitaalamu. Wakati tabia za uadilifu kama sala na kusoma maandiko ni muhimu, mara nyingi msaada zaidi unahitajika kwa wale wanaopitia ugonjwa wa akili unaoibuka au kuvumilia kiwewe cha siri. Kupuuzia hali hakutafanya mambo kuwa mazuri. Katika maeneo mengi, askofu anaweza kutoa usaidizi wa kifedha kwa watu binafsi na familia kwa ajili ya ushauri kupitia Huduma za Familia au watoa huduma wengine.

Yesu Aliwawezesha

Picha
father helping son ride bicycle

Kielelezo cha Picha na Angalee Jackson

Wakati akiwalinda watoto, Yesu pia aliwawezesha. Aliwaonyesha watoto kama mifano (ona Mathayo 18:3). Baada ya kuzuru Kwake Amerika, watoto wadogo waliweza kuwafundisha watu wazima “vitu vya kustaajabisha” (3 Nefi 26:16).

Tunaweza kuwawezesha watoto tunaowafahamu kwa kuwafundisha kutambua jinsi Roho anavyozungumza na kisha kumfuata Roho wakati wa kufanya maamuzi—kuwasaidia kujenga chujio la ndani la kulinda matendo yao. Kama Dada Jones alivyofundisha, “Kuwasaidia watoto kujenga mantiki yao wenyewe ya ndani ya kutaka [kufanya maamuzi salama] ni muhimu.”8 Hapa kuna baadhi ya mawazo ambayo yamewezesha familia zingine:

  • Mama mmoja aliwafundisha watoto wake kuwa makini kwenye “hisia zao za “uh-oh” na kuwa makini kati ya watu wanaoonekana “wenye hila.” Hii ilifanya kazi wakati baadhi ya watu walipojaribu kumshawishi kijana wake kuwafuata maliwatoni, na alisikiliza hisia zake za kuonya na akakataa.

  • Baadhi ya familia hutengeneza mpango wa njia ya uzio kabla ya muda ili kutumika wakati wanapokutana na jambo la kudhuru. Kwa mfano, mpango wa njia ya uzio wa familia moja uliitwa “angamiza na sema” na ulijumuisha kuzima kompyuta na kumwambia mzazi mara moja ikiwa picha mbaya imetokea. Watoto wao kamwe hawakujiuliza kuhusu jinsi ya kushughulikia vyombo vya habari visivyofaa—walijua nini cha kufanya!

  • Familia nyingine ilitengeneza mfumo wa neno ambalo watoto wao wangeweza kutuma arafa kwa wazazi wao au kusema kwenye simu ikiwa walihitaji kufuatwa mara moja.

  • Ungeweza kuwasaidia watoto wako kufanya mazoezi kusema, “Hapana!” wakati mtu anapojaribu kufanya jambo ambalo linawapa hisia mbaya. Kila mtoto anapaswa kujua kwamba wanaweza kuomba msaada, na wanapaswa kuendelea kuomba mpaka wanapokuwa salama.

Jukumu Letu kama Watu Wazima

Hebu turejee tena tukio katika 3 Nefi 17, wakati Yesu alipochukua watoto wao wachanga, mmoja mmoja, na kuwabariki, na kuomba kwa Baba juu yao. … Na walizungukwa na moto; na malaika waliwahudumia” (mistari ya 21, 24). Pengine kipengele muhimu cha hadithi hii si tu kutufundisha sisi jinsi watoto walivyo muhimu bali pia kuelezea nini jukumu letu linapaswa kuwa, kama watu wazima. Sisi ni walinzi wa kizazi kijacho. Sisi tunapaswa kuwa malaika ambao wanawazunguka na kuwahudumia watoto. Acha tuendelee kumtazama Yesu kama mfano wetu mkamilifu na kisha kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwazunguka wachanga wetu kwa upendo na ulinzi.

Muhtasari

  1. Ona marejeleo ya maandiko chini ya kichwa cha habari cha kila kipengele katika makala hii ili kupata hadithi hizi katika maandiko.

  2. Ona “Child Maltreatment (Child Abuse),” World Health Organization, who.int/violence_injury_prevention/violence/child/en.

  3. Joy D. Jones, “Kuzungumzia Ponografia: Linda, Itikia, na Ponya,” Liahona, Okt. 2019, 38.

  4. Joy D. Jones, “Kuzungumzia Ponografia,” 39, 40.

  5. Joy D. Jones, “Kuzungumzia Ponografia,” 39.

  6. Dallin H. Oaks, “Kuwalinda Watoto,” Liahona, Nov. 2012, 43.

  7. Ona “Preventing and Responding to Abuse,” newsroom.ChurchofJesusChrist.org.

  8. Joy D. Jones, “Kuzungumzia Ponografia,” 40.

Chapisha