2019
Jiwe Kuu la Pembeni la Imani Yetu
Oktoba 2019


Neno la Mwisho

Jiwe Kuu la Pembeni la Imani Yetu

Kutoka katika hotuba ya mkutano mkuu wa Oktoba 1984.

Katika kila hekalu jipya tuna sherehe ya jiwe la pembeni ikienda sambamba na utamaduni ambao una kiini katika nyakati za kale. Kabla ya matumizi ya jumla ya saruji, kuta za msingi wa jengo ziliwekwa kwa mawe makubwa. Mtaro ungechimbwa, na mawe yangewekwa kama msingi imara. Kuanzia kwenye alama ya mwanzo, ukuta wa msingi ungejengwa katika uelekeo mmoja kuelekea jiwe la pembeni; kisha pembe ingekunjwa na ukuta kujengwa kuelekea pembe inayofuata, ambapo kutoka hapo jiwe lingine lingewekwa, ambapo kutoka hapo ukuta ungejengwa kuelekea pembe inayofuata, na kutoka hapo kuelekea sehemu ya mwanzo. … Jiwe la mwisho lilisemekana kuwa jiwe kuu la pembeni, na uwekwaji wake ulikuwa sababu ya kusheherekea sana. Jiwe hili la pembeni likiwa mahala pake, msingi ulikuwa tayari kwa ajili ya jengo kusimama. Hivyo analojia ambayo Paulo aliitumia kuelezea Kanisa la kweli:

“Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu;

“Na mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni;

“Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana” (Waefeso 2:19–21).

Tunayo mawe ya pembeni ya msingi ambayo juu yake Kanisa hili kuu la siku za mwisho limeanzishwa na Bwana na kujengwa, “likikaa barabara pamoja.” Mawe hayo ni muhimu hasa kwa kazi hii, msingi hasa, nanga ambazo juu yake linasimama. … [Lakini] ninataja jiwe kuu la pembeni, ambaye tunamtambua na kumheshimu kama Bwana Yesu Kristo. …

Yeye ni jiwe kuu la pembeni la Kanisa ambalo linabeba jina Lake, Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Hapana jina jingine walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo (ona Matendo ya Mitume 4:12). Yeye ni sababu ya wokovu wetu, mtoaji wa uzima wa milele (Ona Waebrania 5:9). Hakuna yeyote aliye sawa Naye. Kamwe hajawahi kuwepo. Kamwe hatakuwepo. Shukrani ziwe kwa Mungu kwa ajili ya zawadi ya Mwana Wake Mpendwa, ambaye aliutoa uhai Wake kwamba sisi tuweze kuishi, na ambaye ni jiwe la pembeni, lisilohamishika la imani yetu na Kanisa Lake.

Chapisha