2010–2019
Furaha ya Huduma Isiyo ya Ubinafsi
Oktoba 2018


Furaha ya Huduma Isiyo ya Ubinafsi

Tumemuahidi Baba yetu wa Mbinguni kwamba tutamtumikia Yeye na wengine kwa upendo na kufanya mapenzi Yake katika vitu vyote.

Baada ya mkutano mkuu uliopita, watu wengi walinijia na swali lilelile: “viti hivyo vina raha?” Jibu langu lilikuwa lilelile kila wakati: “Viti hivyo vina raha sana kama hutakuwa unazungumza.” Ni kweli, sivyo? Kiti changu hakijawa chenye raha mkutano huu, lakini kwa kweli nina shukrani kwa ajili ya baraka na heshima ya kuzungumza nanyi jioni hii.

Wakati mwingine tunapotumikia, tunapata kukaa katika viti tofauti. Baadhi vina raha sana na baadhi havina, lakini tumemuahidi Baba yetu wa Mbinguni kwamba tutamtumikia Yeye na wengine kwa upendo na kufanya mapenzi yake katika vitu vyote.

Miaka michache iliyopita, vijana katika Kanisa walijifunza kwamba “wakati ‘mnapoingia katika utumishi wa Mungu’ [Mafundisho na Maagano 4:2], mnajiunga daima na safari kubwa mno. Mnamsaidia Mungu kuharakisha kazi yake, na ni uzoefu mkubwa sana, wenye furaha, na wa ajabu.”1 Ni safari inayopatikana kwa wote—wa umri wowote—na pia ni safari ambayo inatuchukua kukubaliana na kile nabii wetu mpendwa alichokiita kama “njia ya agano.”2

Kwa bahati mbaya, hata hivyo, tunaishi katika ulimwengu usio na hisani ambako watu siku zote wanauliza, “kuna nini ndani yake kwa ajili yangu?” badala ya kuuliza, “Nani ninayeweza kumsaidia leo?” au “Jinsi gani ninaweza kumtumikia vizuri zaidi Bwana katika wito wangu?” au “Je ninatoa vyangu vyote kwa Bwana?”

Picha
Dada na Kaka Antonietti
Picha
Victoria Antonietti

Mfano mkubwa katika maisha yangu wa huduma isiyo ya kibinafsi ni Dada Victoria Antonietti. Victoria alikuwa mmoja wa walimu wa Msingi katika tawi langu wakati nikikua nchini Argentina. Kila Jumanne mchana, wakati tulipokusanyika kwa ajili ya Msingi, Alituletea keki ya chokoleti. Kila mtu aliipenda keki hiyo—vyema, kila mmoja isipokuwa mimi. Sikupenda keki ya chokoleti! Na hata kama angejaribu kugawana keki na mimi, mara zote nilikataa ombi lake.

Siku moja baada ya kugawana keki ya chokoleti na watoto wote, nilimuuliza, “Kwa nini huleti ladha tofauti—kama machungwa au vanila?”

Baada ya kucheka kidogo, aliniuliza, “Kwa nini wewe usijaribu kipande kidogo? Keki hii imetengenezwa na kiambato maalum, na ninaahidi kwamba kama utaijaribu, utaipenda!”

Nilitazama kuzunguka, na kwa mshangao wangu, kila mtu alionekana kuifurahia keki. Nilikubali kujaribu. Unaweza kubahatisha nini kilitokea? Niliipenda! Ile ilikuwa ni mara ya kwanza kabisa kuifurahia keki ya chokoleti.

Haikuwa mpaka miaka mingi baadae kwamba niligundua kile kiambato cha siri kilichokuwa kwenye keki ya chokoleti ya Dada Antonietti. Watoto wangu na mimi tulimtembelea mama yangu kila wiki. Katika moja ya matembezi haya, Mama na mimi tulikuwa tunafurahia kipande cha keki ya chokoleti, na nilimwelezea jinsi gani nilikuja kuipenda keki ya chokoleti kwa mara ya kwanza kabisa. Kisha alinielimisha na hadithi yote.

“Unaona, Cris,” mama yangu alisema, “Victoria na familia yake hawakuwa na rasilimali nyingi, na kila wiki alipaswa achague kati ya kulipia basi kumchukua yeye na watoto wake wanne kwenda darasa la Msingi au kununua viambato kutengeneza keki ya chokoleti kwa ajili ya darasa la Msingi. Mara zote alichagua keki ya chokoleti badala ya basi, na yeye na watoto wake walitembea zaidi ya maili mbili [3 km], kwenda na kurudi, bila kujali hali ya hewa.”

Siku ile nilikuwa na shukrani zaidi kwa ajili ya keki yake ya chokoleti. Muhimu zaidi, nilijifunza kwamba kiambato cha siri katika keki ya Victoria kilikuwa ni upendo aliokuwanao kwa ajili ya wale aliowatumikia na dhabihu yake isiyo na ubinafsi kwa niaba yetu.

Kufikiria nyuma juu ya keki ya Victoria kunanisaidia kukumbuka dhabihu isiyo na ubinafsi katika somo la milele lililofundishwa na Bwana kwa wanafunzi wake alipokuwa anatembea kuelekea hazina ya hekalu. Mnaijua hadithi. Mzee James E. Talmage alifundisha kwamba kulikuwa na makasha 13, “na katika haya watu walitumbukiza michango yao kwa ajili ya azma [tofauti] zilizooneshwa na maandishi kwenye masanduku.” Yesu aliangalia mistari ya wahisani, iliyotokana na aina tofauti za watu. Baadhi walitoa zawadi zao kwa “azma za ukweli” wakati wengine walitumbukiza “kiasi kikubwa cha fedha na dhahabu,”wakitegemea kuonekana, kujulikana, na kusifiwa kutokana na michango yao.

“Miongoni mwa wengi alikuwepo mjane masikini, ambaye … alitumbukiza kwenye moja ya makasha-ya hazina sarafu mbili za shaba zinazojulikana kama msaada mdogo; mchango wake ulikuwa chini ya nusu senti ya hela ya marekani. Bwana aliwaita wafuasi wake karibu Naye, akaelekeza usikivu wao kwenye mjane masikini na tendo lake, na akasema: ‘Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina: Maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia’ [Marko 12:43–44].”3

Picha
Sarafu za Mjane

Mjane hakuonekana ana nafasi ya kuonekana katika jamii ya wakati wake. Kwa kweli alikuwa na kitu fulani muhimu zaidi: dhamira zake zilikuwa safi, na alitoa vyote alivyokuwa navyo vya kutoa. Pengine alitoa kidogo kuliko wengine, kwa ukimya zaidi kuliko wengine, kitofauti kuliko wengine Katika macho ya wengine, kile alichotoa kilikuwa hakina maana, lakini katika macho ya mwokozi, ”mtambuzi wa mawazo na dhamira za moyo,”4 alitoa vyote avyokuwanavyo.

Akina Dada, je, tunatoa vyote kwa Bwana bila kusita? Je, tunatoa dhabihu muda wetu na vipaji vyetu ili uzao unaochipukia uweze kujifunza kumpenda Bwana na kutii amri zake? Je, tunawahudumia wote wanaotuzunguka na wale tuliopangiwa kwa kuwatunza na kwa bidii—tukitoa dhabihu muda na nguvu ambavyo vingeweza kutumika katika njia zingine? Je, tunaishi amri mbili zilizo kuu—kumpenda Mungu na kuwapenda watoto Wake?5 Mara nyingi upendo huo hudhihirika kama huduma.

Rais Dallin H. Oaks alifundisha: “Mwokozi wetu alijitoa mwenyewe katika huduma isiyo na ubinafsi. Alifundisha kwamba kila mmoja wetu anapaswa kumfuata Yeye kwa sisi kujinyima matamanio yetu ili kuwatumikia wengine.”

Aliendelea:

“Mfano ulizoeleka wa kujitoa wenyewe katika huduma ya wengine … ni dhabihu wazazi hufanya kwa ajili ya watoto wao. Akina mama wanateseka kwa maumivu na kupoteza vipaumbele vyao binafsi na faraja ili kubeba na kulea kila mtoto. Akina baba wanarekebisha maisha yao na vipaumbele vyao kusaidia familia. …

“… Pia tuna furaha katika hao wanaowatunza wanafamilia wasiojiweza na wazazi wazee. Hakuna katika huduma hii anaeyeuliza, kuna nini ndani yake kwa ajili yangu? Yote hiyo huitaji kuweka pembeni mambo binafsi kwa ajili ya huduma isiyo na ubinafsi. …

“[Na] yote hii inaonyesha kanuni ya milele kwamba tuna furaha zaidi na kujazwa zaidi wakati tunapofanya na kutumikia kwa kile tunachotoa, sio kwa kile tunachopata.

“Mwokozi wetu anatufundisha kumfuata kwa kutoa dhabihu iliyo muhimu ya kujitoa wenyewe katika huduma isiyo na ubinafsi kwa wengine.”6

Rais Thomas S. Monson vilevile alifundisha kwamba “labda wakati tutakapokuwa uso kwa uso na Muumba wetu, hatutaulizwa, ‘Ni nafasi gani tulizokuwa nazo?’ isipokuwa , ‘Ni watu wangapi uliowasaidia?’ Kiukweli, huwezi kumpenda Bwana mpaka pale utakapomtumikia Yeye kwa kuwatumikia wengine.”7

Kwa maneno mengine, akina dada, si muhimu kama tutakaa kwenye viti vya raha au kama tulijitahidi sana kufanya mikutano kwenye viti vya kukunja vyenye kutu katika safu ya mwisho. Si muhimu hata kidogo kama sisi, kwa umuhimu, tutaingia kwenye ukumbi kumfariji mtoto anayelia. Kile kitakachokuwa cha muhimu ni kwamba tulikuja na hamu ya kutumikia, kwamba tuliwaona wale ambao tunawatumikia na kuwaamkia kwa furaha, na kwamba tulijitambulisha kwa wale wanaoshiriki safu yetu ya viti vya kukunja—tukiwafikia kwa urafiki hata kama hatukupangiwa kuwatumikia. Na kwa hakika itakuwa muhimu kwamba tufanye yote tunayofanya na kiambato maalumu cha huduma iliyounganishwa na upendo na dhabihu.

Nimekuja kujua kwamba hatuhitaji kutengeneza keki ya chokoleti ili kuwa mwalimu wa Msingi mwenye ufanisi au mwenye bidii, kwa sababu haikuwa ni kuhusu keki tu. Ilikuwa ni upendo unaosababisha kitendo.

Ninashuhudia kwamba upendo huo hufanywa mtakatifu kupitia dhabihu—dhabihu ya mwalimu na hata zaidi kupitia dhabihu ya mwisho na ya milele ya Mwana wa Mungu. Ninatoa ushuhuda kwamba Anaishi. Ninampenda na ninatamani kuacha matamanio ya ubinafsi ili kupenda na kutumikia kama anavyofanya. Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha