2010–2019
Uchungaji wa Watu
Oktoba 2018


Uchungaji wa Watu

Tunawafikia wengine kwa upendo kwa sababau ndicho kile Mwokozi wetu ametuamuru kufanya.

Katika mazungumzo ya karibuni na rafiki yangu, aliniambia kwamba alipokuwa muumini wa Kanisa, kijana aliyekuwa amebatizwa karibuni, ghafla alijihisi kwa kiasi fulani hakufaa tena katika kata yake. Wamisionari waliomfundisha walikuwa wamehamishwa, na alihisi kana kwamba alikuwa ukingoni. Bila marafiki katika kata, alikutana na rafiki zake wa zamani na kujiunga nao katika shughuli ambazo zilimtoa kwenye kushiriki kanisani—kiasi kwamba alianza kupotea kutoka kundini. Kwa machozi machoni mwake, alielezea jinsi gani alikuwa na shukrani nyingi wakati muumini mwenza wa kata alipomnyoshea mkono wa huduma na kumualika kurudi katika njia ya upendo na mjumuisho. Ndani ya miezi michache, alikuwa amerudi katika usalama wa kundi, akiwaimarisha wengine na kujiimarisha mwenyewe. Je, hatuna shukrani kwa mchungaji wa Brazil ambaye alimtafuta mvulana huyu, Mzee Carlos A. Godoy, ambaye sasa anaketi nyuma yangu kama mshiriki wa Urais wa Sabini?

Ni ya kusifika jinsi juhudi ndogo kama hizo zinavyoweza kuwa na matokeo ya milele? Ukweli huu uko katika kiini cha juhudi za Kanisa za kuhudumu. Baba wa Mbinguni anaweza kuchukua juhudi zetu rahisi, za kila siku na kuzigeuza kuwa kitu cha kustaajabisha. Imekuwa miezi sita tu tangu Rais Russell M. Nelson alipotangaza kwamba “Bwana amefanya marekebisho muhimu kwenye jinsi ya sisi kujaliana,”1 akielezea, “Tutafanyia kazi mtazamo mpya, mtakatifu wa kuwajali na kuwahudumia wengine. Tutaziita juhudi hizi kwa urahisi kama ‘kuhudumu.’”2

Rais Nelson pia alieleza: “Sifa bainifu ya Kanisa la kweli na lililo hai la Bwana siku zote litakuwa lenye utaratibu, lenye juhudi zilizoelekwezwa kuwahudumia watoto binafsi wa Mungu na familia zao. Kwa sababu ni Kanisa lake, sisi kama watumishi Wake tutahudumia kila mmoja, kama Yeye alivyofanya. Tutahudumu katika jina Lake, kwa nguvu Zake na mamlaka, na kwa huruma Zake za upendo.”3

Tangu tangazo hilo, mwitikio wenu umekuwa wa ajabu! Tumepokea ripoti zenye mafanikio makubwa katika kutekeleza mabadiliko haya karibia katika kila kigingi ulimwenguni kama ilivyoelekezwa na nabii anayeishi. Kwa mfano, akina kaka na akina dada wa kuhudumu wamepangiwa familia, wenza—ikijumuisha wavulana na wasichana—wamepangwa, na usahili wa kuhudumu unafanyika.

Sidhani kuwa ni kwa nasibu kwamba miezi sita kabla ya tangazo la kifunuzi la jana—”usawa mpya na muunganiko kati ya maelekezo ya injili nyumbani na Kanisani”4—tangazo la kifunuo juu ya kuhudumu lilitolewa. Kuanzia Januari, tunapotumia saa moja pungufu katika ibada zetu za kanisa, yale yote tuliyojifunza katika kuhudumu yatatusaidia kufanya sawa uwazi ule katika uzoefu wa juu na mtakatifu wa siku ya Sabato iliyolenga nyumbani pamoja na familia na wapendwa wetu.

Muundo huu wa utaratibu ukiwa umewekwa, tunaweza kuuliza, “Tunawezaje kujua tunahudumia katika njia ya Bwana? Je, tunamsaidia Mchungaji Mwema katika njia Anazokusudia?”

Katika mjadala wa karibuni, Rais Henry B. Eyring aliwasifu Watakatifu katika kuzoea mabadiliko haya ya kupendeza lakini pia alitoa tumaini lake la dhati kwamba waumini wanatambua kwamba kuhudumu ni zaidi ya “kuwa tu wema.” Hiyo si kusema kwamba kuwa wema si muhimu, lakini wale wanaoelewa roho ya kweli ya kuhudumu wanagundua kwamba kunaenda mbali zaidi ya kuwa tu wema. Kukifanywa katika njia ya Bwana, kuhudumu kunaweza kuwa na ushawishi mkubwa kwa wema ambao husambaa milele yote, kama ambavyo imekuwa kwa Mzee Godoy.

“Mwokozi alionyesha kwa mfano kile inachomaanisha kuhudumu pale Alipotumikia kwa upendo. … Yeye … alifundisha, aliombea, alifariji, na alibariki wale waliomzunguka, akiwaalika wote kumfuata Yeye. … Waumini wa Kanisa wanapohudumu [katika njia ya juu na takatifu], wanatafuta kwa sala kutumikia kama ambavyo Yeye angefanya— … ‘kuliangalia kanisa daima, na kuwa nalo na kuwaimarisha; ‘kutembelea nyumba ya kila muumini,’ na kumsaidia kila mmoja kuwa mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo.”5

Tunaelewa kwamba mchungaji wa kweli anawapenda kondoo wake, anawajua kila mmoja kwa jina, na “ana mvuto binafsi” kwao.6

Picha
Kondoo milimani

Rafiki wa miaka mingi aliishi maisha yake kama mfugaji, akifanya kazi ngumu ya kutunza ng’ombe na kondoo katika Milima ya Rocky yenye miamba ya mawe. Wakati fulani alishiriki nami changamoto na hatari zinazohusiana na kufuga kondoo. Alielezea kwamba mapema katika majira ya kuchipua, wakati theluji juu ya safu za milima ya kutanuka karibu yote ikiwa imeyeyuka, aliweka mifugo ya familia takriban kondoo 2,000 milimani kwa ajili ya kiangazi. Hapo, aliwalinda kondoo mpaka mwisho wa majira ya majani kupukutika, ambapo walihamishwa kutoka kwenye safu za kiangazi kwenda safu za baridi jangwani. Alielezea jinsi kuhudumia kundi kubwa la kondoo kulivyo kugumu, ikihitaji mapema mno na kuchelewa mno—kuamka kabla ya jua kuchomoza na kumaliza kwa kuchelewa baada ya giza kuingia. Asingeweza kufanya hilo peke yake.

Picha
Msaidizi wa ranchi pamoja na kondoo

Wengine walisaidia kuhudumia mifugo, ikijumuisha mchanganyiko wa mikono ya mifugo wazoefu wakisaidiwa na mikono michanga ambayo ilinufaika kutokana na hekima ya wenzao. Alitegemea pia farasi wawili wakubwa, farasi wawili wadogo kwenye mafunzo, mbwa wawili wakubwa, na mbwa wadogo wawili au watatu. Wakati wa baridi, rafiki yangu na kondoo wake walikabiliana na upepo na dhoruba, ugonjwa, majeraha, ukame, na kila aina ya ugumu mtu anaoweza kufikiria. Baadhi ya miaka iliwabidi kukokota maji wakati wote wa kiangazi ili tu kuwaweka kondoo hai. Kisha, kila mwaka mwishoni mwa majira ya majani kupukutika, wakati hali ya baridi ilipotishia na kondoo kuondolewa mlimani na kuhesabiwa, kulikuwa mara kwa mara zaidi ya 200 waliokuwa wamepotea.

Picha
Kuchunga kondoo
Picha
Kundi la kondoo

Kundi la mifugo 2,000 lililowekwa milimani mapema majira ya kuchipua lilipungua kufikia chini ya 1,800. Wengi wa kondoo ambao hawakuonekana hawakuwa wamepotea kwenye ugonjwa au kifo cha asili bali kwa wanyama kama vile simba wa mlimani au mbwa mwitu. Wanyama hawa mara nyingi walipata kondoo ambao walikuwa wamejitenga kutoka kwenye usalama wa kundi, wakijitoa wenyewe kutoka kwenye ulinzi wa mchungaji wao. Ungeweza kutafakari kwa muda kile ambacho nimeelezea, katika muktadha wa kiroho? Mchungaji ni nani? Kundi ni nani? Wale wanaomsaidia mchungaji ni kina nani?

Picha
Mchungaji Mwema

Bwana Yesu Kristo mwenyewe alisema, “Mimi ndimi mchungaji mwema, nao walio wangu nawajua, … Nami nautoa uhai wangu kwa ajili ya kondoo.”7

Picha
Yesu akiwalisha kondoo Wake

Nabii Nefi hali kadhalika alifundisha kwamba Yesu “atalisha kondoo wake, na kwake watapata malisho.”8 Ninapata amani ya kudumu katika kujua kwamba “Bwana ndiye mchungaji wangu”9 na kwamba kila mmoja wetu anajulikana Kwake na yuko kwenye ulinzi wake. Tunapokabiliana na upepo na dhoruba za maisha, ugonjwa, majeraha, na ukame, Bwana—Mchungaji wetu—atatuhudumia. Yeye atarejesha nafsi zetu.

Katika njia sawa na ile rafiki yangu alivyohudumia kondoo wake kwa usaidizi wa mikono michanga na yenye uzoefu ya mifugo, farasi, na mbwa walinzi, Bwana pia anahitaji usaidizi katika kazi yenye changamoto ya kutunza kondoo katika kundi Lake.

Picha
Yesu Kristo akihudumu

Kama watoto wa Baba mpendwa wa Mbinguni na kama kondoo kwenye kundi Lake, tunafurahia baraka za kuhudumiwa kibinafsi na Yesu Kristo. Wakati huo huo, tunao wajibu wa kutoa msaada wa huduma kwa wengine wanaotuzunguka kama wachungaji sisi wenyewe. Tunaitikia maneno ya Bwana ya “nitumikie na kuendelea mbele kwa jina langu, na … kusanya pamoja kondoo wangu.”10

Mchungaji ni nani? Kila mwanamume, mwanamke, na mtoto katika ufalme wa Mungu ni mchungaji. Hakuna wito unaohitajika. Tangu wakati tunapotoka nje ya maji ya ubatizo, tunapewa wajibu kwenye kazi hii. Tunawafikia wengine kwa upendo kwa sababau ndicho kile Mwokozi wetu ametuamuru kufanya. Alma alisisitiza: “Kwani ni mchungaji gani … ambaye ana kondoo wengi na hawachungi, ili mbwa mwitu wasiingie na kuwararua mifugo yake? … Je, hamfukuzi nje?”11 Popote majirani zetu wanapokuwa katika dhiki kimwili au kiroho, tunakimbia kuwapa msaada. Tunabeba mizigo ya mmoja na ya mwingine ili iwe miepesi. Tunaomboleza na wale wanaoomboleza. Tunawafariji wale ambao wanahitaji kufarijiwa.12 Bwana kwa upendo anategemea hili kutoka kwetu. Na siku itafika ambapo Atatuwajibisha kwa matunzo tunayotoa katika kuhudumia kundi Lake.13

Rafiki yangu mchungaji alishiriki elementi nyingine muhimu katika kulinda kondoo juu ya safu. Alielezea kwamba kondoo waliopotea walikuwa hasa si salama kwa hatari za wanyama. Kwa kweli, mpaka asilimia 15 ya jumla ya muda wake na wasaidizi wake ulitumika kutafuta kondoo waliopotea. Kadiri mapema walivyomtafuta kondoo aliyepotea, kabla kondoo hajaenda mbali zaidi kutoka kwenye kundi, ndivyo ungekuwa uwezekano mdogo wa kondoo kudhuriwa. Kumrudisha kondoo aliyepotea huitaji uvumilivu mkubwa na nidhamu.

Miaka kadhaa iliyopita, nilipata makala katika gazeti ambayo ilikuwa ya kuvutia sana kiasi kwamba niliitunza. Kichwa cha habari cha mbele kinasomeka, “Mbwa Aliyedhamiria Hawezi Kuwaacha Kondoo Waliopotea.”14 Makala hii inaelezea idadi ndogo ya kondoo iliyomilikiwa na kampuni iliyo karibu na miliki ya rafiki yangu ambao kwa kiasi fulani waliachwa nyuma katika safu zao za baridi. Miezi miwili au mitatu baadaye, walikuwa wamekwama na kuzungukwa na theluji milimani. Wakati kondoo walipoachwa nyuma, mbwa mlinzi alikaa nao, kwani lilikuwa jukumu lake kuwaangalia na kuwalinda kondoo. Asingeweza kuondoa ulinzi wake! Pale alibakia—akiwazunguka kondoo waliopotea kwa miezi kwenye hali ya hewa ya baridi na theluji, akitumikia kama mlinzi dhidi ya mbwa mwitu, simba wa mlimani, au mnyama mwingine yoyote ambaye angewadhuru kondoo. Alibakia pale mpaka alipoweza kuwaongoza kondoo kurudi kwenye usalama wa mchungaji na kundi. Taswira iliyonaswa kwenye ukurasa wa mbele wa makala hii inamruhusu mtu kuona sifa machoni na nidhamu ya mbwa huyu mlinzi.

Picha
Sifa katika macho na nidhamu ya mbwa mlinzi

Katika agano jipya, tunapata mfano na maelekezo kutoka kwa Mwokozi ambayo yanatoa umaizi wa ziada kuhusiana na jukumu letu kama wachungaji, akina dada na akina kaka wahudumiaji, wa kondoo waliopotea:

“Ni nani kwenu, mwenye kondoo mia, akipotewa na mmojawapo, asiyewaacha wale tisini na kenda nyikani, aende akamtafute yule aliyepotea, hata amwone?

“Naye akiisha kumwona, humweka mabegani pake, akifurahi.

“Na afikapo nyumbani kwake, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, furahini pamoja nami; kwa kuwa nimekwisha kumpata kondoo wangu aliyepotea.”15

Tunapofupisha somo lililofundishwa katika mfano, tunapata ushauri huu wa thamani:

  1. Tunapaswa kuwatambua kondoo waliopotea.

  2. Tunawatafuta mpaka wapatikane.

  3. Wanapopatikana, tunaweza kuhitajika kuwaweka mabegani mwetu kuwaleta nyumbani.

  4. Tunawazunguka kwa marafiki pale wanaporudi.

Akina kaka na kina dada, changamoto yetu kubwa na zawadi yetu kubwa vinaweza kuja pale tunapowahudumia kondoo waliopotea. Waumini wa Kanisa katika Kitabu cha Mormoni “waliwalinda watu wao, na kuwalisha vitu vilivyohusu utakatifu.”16 Tunaweza kufuata mfano wao tunapokumbuka kwamba kuhudumu kunapaswa “kuongozwa na Roho, … rahisi kubadilishwa, na … kunakokidhi mahitaji ya kila muumini.” Pia ni muhimu kwamba “tutafute kuwasaidia watu binafsi na familia kujiandaa kwa ibada zao zijazo, kutunza maagano [yao] … , na kuwa wenye kujitegemea.”17

Kila nafsi ni ya thamani kwa Baba yetu wa Mbinguni. Mwaliko wake binafsi wa kuhudumu ni wa thamani ya juu na muhimu Kwake, kwani ni kazi na utukufu Wake. Kweli ni kazi hasa ya milele. Kila mmoja wa watoto Wake ana uwezekano usiopimika mbele Zake. Yeye anakupenda wewe kwa upendo usioweza hata kuanza kufikiria. Kama vile mbwa mlinzi aliyedhamiria, Bwana atabaki mlimani kukulinda hadi mwisho wa upepo, dhoruba, theluji, na mengineyo.

Rais Russell M. Nelson alitufundisha kwenye mkutano uliopita: “Ujumbe wetu kwa ulimwengu [na ngoja niongeze, “kwa kundi letu la kuhudumu”] ni rahisi na wa kweli: tunawaalika watoto wa Mungu wote kutoka pande zote mbili za pazia waje kwa Mwokozi wao, wapokee baraka za hekalu takatifu, wawe na furaha ya kudumu, na kustahili uzima wa milele.”18

Acha tuinue uoni wetu kwenye ono hili la kinabii, ili tuweze kuchunga watu kuelekea hekaluni na hatimaye kwa Mwokozi wetu, Yesu Kristo. Yeye hatarajii sisi kutenda miujiza. Anaomba tu kwamba tuwalete kaka na dada zetu Kwake, kwani Yeye ana nguvu za kukomboa nafsi. Tunapofanya hivyo, tunaweza na tutapata ahadi hii: “Na mchungaji mkuu atakapodhihirishwa, mtaipokea taji ya utukufu ile isiyokauka.”19 Juu ya hili ninashuhudia—na juu ya Yesu Kristo kama Mwokozi wetu na Mkombozi wetu—katika jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha