2010–2019
Kama Alivyofanya
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Kama Alivyofanya

Tunapotafuta kuhudumu jinsi Yeye Alivyofanya, tutapatiwa fursa ya kusahau ubinafsi wetu na kuwainua wengine.

Takriban miezi 18 iliyopita, katika majira ya majani kupukutika mwaka 2017 kaka yangu wa miaka 64 Mike alinijulisha kwamba alikuwa amepatikana na saratani ya kongosho. Aliniambia pia kwamba alikuwa amepata baraka ya ukuhani kutoka kwa mwalimu wake wa nyumbani na kwamba alikuwa amekutana na askofu wake. Baadaye alinitumia picha ya Hekalu la Oakland California iliyopigwa kutoka hospitali ambayo alikuwa akipokea matibabu, ikiwa na maelezo “Angalia kile ninachoweza kuona kutoka chumba changu hospitalini.”1

Nilishangazwa na maoni yake kuhusu walimu wa nyumbani, baraka za ukuhani, maaskofu, na mahekalu jinsi nilivyoshangazwa kuhusu saratani. Unaona, Mike, kuhani katika Ukuhani wa Haruni, hakuwa ameshiriki kikamilifu kanisani karibia miaka 50.

Kama familia, tulivutiwa na maendeleo yake ya kiroho kama jinsi ambavyo tulivutiwa na maendeleo yake ya kupigana dhidi ya saratani, kwa kiasi kikubwa kwa sababu ya maswali yake ya kila mara kuhusu Kitabu cha Mormoni, na nguvu ya kuunganisha, na maisha baada ya kifo. Wakati miezi ilipokuwa ikisonga na saratani kuenea, kuhitajika kwa matibabu zaidi na maalumu kulimleta Mike Utah na katika Kituo cha Saratani cha Huntsman.

Muda mfupi baada ya kuwasili kwake, Mike alitembelewa na John Holbrook, kiongozi wa kata wa umisionari wa kata ambayo ilihudumia kituo cha uangalizi ambapo alikuwa akiishi kwa wakati huu. John alisema kwamba “ilikuwa dhahiri kwangu kwamba Mike alikuwa mwana wa Mungu” na kwamba baada ya muda mfupi walikuza muungano na urafiki, ambao ulipelekea John kuwa kaka mhudumu wa Mike bila kupingwa. Kulikuwa na mwaliko wa moja kwa moja kwa wamisionari kumtembelea, ambao kaka yangu kwa upole aliukataa, lakini mwezi mmoja ndani ya urafiki wao, akimwelezea Mike, “Nafikiri ungefurahi kusikiliza ujumbe wa injili.”2 Wakati huu mwaliko ulikubaliwa, na kupelekea kwenye mikutano ya mara kwa mara na wamisionari, vile vile matembezi kutoka kwa Askofu Jon Sharp, ambaye mazungumzo yake hatimaye yalipelekea Mike kupokea baraka yake ya baba mkuu, miaka 57 baada ya kubatizwa kwake.

Mapema Desemba mwaka uliopita, baada ya utaratibu wa miezi mingi, Mike aliamua kuacha matibabu ya saratani, ambayo yalikuwa yakisababisha athari kali, na kuruhusu mambo yatokee jinsi yalivyo. Tulijulishwa na daktari wake kwamba Mike alikuwa na takribani miezi mitatu ya kuishi. Wakati ule ule, maswali ya injili yaliendelea—pamoja na matembezi na msaada wa viongozi wake wa ukuhani wa eneo. Tulipomtembelea Mike, mara nyingi tuliona nakala ya Kitabu cha Mormoni kilichofunguliwa kwenye meza iliyokuwa pembeni ya kitanda tulipokuwa tukijadiliana Urejesho wa injili, funguo za ukuhani, ibada za hekaluni, na asili ya milele ya mwanadamu.

Kufikia katikati ya mwezi Desemba, akiwa na baraka yake ya baba mkuu mkononi, Mike alionekana kupata nguvu, na ubashiri wa angalau miezi mitatu zaidi ulionekana kuwezekana. Tulifanya mipango kwa ajili ya yeye kujiunga nasi wakati wa Krismasi, Mwaka Mpya, na zaidi ya hapo. Mnamo Desemba 16, nilipokea simu ambayo sikuwa naitarajia kutoka kwa Askofu Sharp, ambaye alinijulisha kwamba yeye na rais wa kigingi walikuwa wamemfanyia usaili Mike, wakakuta kwamba anastahili kupokea Ukuhani wa Melkizedeki, na kuuliza wakati ambapo ningekuwa na muda ili nishiriki. Tulipanga kufanya ibada hiyo Ijumaa , Desemba 21.

Siku hiyo ilipofika, mke wangu, Carol, na mimi tuliwasili katika kituo cha uangalizi na mara moja tulilakiwa njiani karibu na chumba chake na kufahamishwa kwamba Mike hakuwa na pigo la moyo. Tuliingia ndani ya chumba na kuwakuta baba mkuu, askofu wake, na rais wake wa kigingi wakisubiri tayari—kisha Mike akafungua macho yake. Alinitambua na kukiri kwamba alikuwa ananisikia na alikuwa tayari kupokea ukuhani. Miaka hamsini baada ya Mike kutawazwa kuhani katika Ukuhani wa Haruni, nilipata fursa, nikisaidiwa na viongozi wake wa eneo, kumtunuku Ukuhani wa Melkizedeki na kumtawaza kaka yangu katika ofisi ya mzee. Masaa matano baadaye, Mike alifariki, akivuka pazia kukutana na wazazi wetu kama mwenye Ukuhani wa Melkizedeki.

Mwaka mmoja tu uliopita, mwito ulitolewa na Rais Russell M. Nelson kwa kila mmoja wetu kuwajali kaka zetu na dada zetu kwa “njia ya juu zaidi, na takatifu zaidi.”3 Akizungumza juu ya Mwokozi, Rais Nelson alifundisha kwamba, “kwa sababu ni Kanisa Lake, sisi kama watumishi Wake tutamhudumia kila mmoja, kama Yeye Alivyofanya. Tutahudumu katika jina Lake, kwa nguvu Zake na mamlaka yake, na kwa huruma Zake za upendo.”4

Katika kujibu mwaliko huu kutoka kwa nabii wa Mungu, juhudi za kusifika za kumhudumia kila mmoja zinafanyika kote ulimwenguni, katika juhudi zote mbili zilizoratibiwa, wakati waumini kwa uaminifu wanapotimiza majukumu yao ya kuhudumu, vile vile na kile nitakachokiita kuhudumu kwa “papohapo”, wakati watu wengi wanapoonyesha Upendo kama wa Kristo katika kuitikia nafasi zisizotarajiwa. Katika familia yetu, tulishuhudia, kwa karibu, aina hii ya kuhudumu.

John, ambaye alikuwa rafiki wa Mike, kaka mhudumiaji, na rais wa zamani wa misheni, alikuwa akiwaambia wamisionari wake kwamba “ikiwa mtu yuko kwenye orodha inayosema ‘hataki,’ usikate tamaa. Watu hubadilika.” Kisha alituambia, “Mike alibadilika kwa njia kuu.”5 John alikuwa kwanza rafiki, akitoa tumaini na msaada wa mara kwa mara—lakini kuhudumu kwake hakukuishia kwenye matembezi ya kirafiki. John alifahamu kwamba mtumishi ni zaidi ya rafiki na kwamba urafiki unakuzwa wakati tunapohudumu.

Si lazima mtu awe anaugua, kama kaka yangu, kutokana na maradhi yanayotishia maisha ili ahitaji kuhudumiwa na kutumikiwa. Mahitaji hayo huja katika aina nyingi ya maumbo, ukubwa, na hali. Mzazi asiye na mwenza; wenza wasioshiriki kikamilifu; kijana aliye na matatizo; mama mwenye majukumu mengi; jaribio la imani; au la kifedha, la kiafya, au changamoto za ndoa—orodha hiyo haina mwisho. Hata hivyo, kama Mike, hakuna mtu aliyepotea kupita kiasi, na haujachelewa kufikiwa na upendo wa Mwokozi.

Tunafundishwa kwenye tovuti ya kuhudumu ya Kanisa kwamba “wakati kuna malengo mengi ya kuhudumu, juhudi zetu zinapaswa kuongozwa na nia ya kuwasaidia wengine wafikie uongofu binafsi wa kina na kuwa zaidi kama Mwokozi.”6 Mzee Neil L. Andersen alisema hilo kwa namna hii:

“Mtu mwenye moyo mwema anaweza kumsaidia mtu fulani kufunga tairi, kumpeleka mkaazi mwenza kwa daktari, kula chakula cha mchana na mtu fulani mwenye huzuni, au kutabasamu na kusema halo kuifanya siku iwe njema.

“Lakini mfuasi wa amri ya kwanza kwa kawaida ataongeza kwenye matendo haya muhimu ya huduma.”7

Katika kuiga mfano Yesu Kristo wa kuhudumu, ni muhimu kukumbuka kwamba juhudi Zake za kupenda, kuinua, kutumikia , na kubariki zilikuwa na lengo la juu zaidi kuliko kutosheleza hitaji la mara moja. Kwa hakika alijua mahitaji yao ya kila siku na alikuwa na huruma juu ya mateso yao ya sasa Alipoponya, kulisha, kusamehe, na kufundisha. Lakini Alitaka kufanya zaidi kuliko kushughulikia leo. Aliwataka wale waliokuwa karibu Naye wamfuate Yeye, wamjue Yeye, na wafikie uwezo wao wa kiungu.8

Tunapotafuta kuhudumu “kama Yeye Alivyofanya,9 tutapatiwa fursa kusahau ubinafsi wetu na kuwainua wengine. Fursa hizi mara nyingi zinaweza kuwa usumbufu na zenye kupima hamu yetu ya kweli ya kuwa kama Bwana, ambaye huduma yake kubwa kuliko zote, Upatanisho Wake usio na mwisho, haukuwa kitu kingine chochote bali wenye manufaa. Katika Mathayo sura ya 25, tunakubushwa kuhusu jinsi Bwana anavyohisi juu yetu, wakati, kama Yeye, sisi ni wepesi wa kuhisi mapambano, majaribu, na changamoto zinazowakabili wengi lakini mara nyingi zinapuuzwa:

“ Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu:

“Kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula: nalikuwa na kiu, mkaninywesha: nalikuwa mgeni, mkanikaribisha. …

“Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha? au una kiu, tukakunywesha?

“Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha? …

“Na Mfalme atajibu, akiwaambia, amin nawaambia, kadiri mlivyo mtendea mmoja wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”10

Iwe tunahudumu kama kaka au dada wahudumiaji, au kwa urahisi wakati ambapo tunajulishwa kuhusu mtu anayehitaji msaada, tunashauriwa kutafuta mwongozo na maelekezo ya Roho—na kisha kutenda. Tunaweza kuwaza njia bora ya kutumikia, lakini Bwana anajua, na kupitia Roho Wake tutaongozwa katika juhudi zetu. Kama Nefi, ambaye “aliongozwa na Roho, bila kujua kimbele vitu ambavyo angefanya,”11 sisi pia tutaongozwa na Roho tunapojitahidi kuwa vyombo katika mikono ya Bwana ili kubariki watoto Wake. Tunapotafuta mwongozo wa Roho na kumwamini Bwana, tutawekwa katika mazingira na hali ambapo tunaweza kutenda na kubariki—kwa maneno mengine, kuhudumu.

Kunaweza kuwa na nyakati zingine tunapotambua hitaji lakini tunahisi hatustahili kuitikia, tukidhania kwamba kile ambacho tunakitoa hakitoshelezi. Kufanya kama Alivyofanya,12 hata hivyo, ni kuhudumu kwa kutoa kile ambacho tunaweza kutoa na kuamini kwamba Bwana atatukuza juhudi zetu za kubariki “wasafiri wenzetu katika hii safari ya mauti.”13 Kwa baadhi, yaweza kuwa kutoa zawadi ya muda na talanta; kwa wengine, yaweza kuwa neno la ukarimu, au mgongo imara. Ingawa tunaweza kuhisi kwamba juhudi zetu ni pungufu, Rais Dallin H. Oaks alishiriki kanuni muhimu kuhusu “vidogo na rahisi.” Alifundisha kwamba vitendo vidogo na rahisi vina nguvu kwa sababu vinaalika “wenza wa Roho Mtakatifu,”14 mwenza anayewabariki wote wawili anayetoa na anayepokea.

Akifahamu kwamba alikuwa karibu kufa, kaka yangu Mike alisema, “Ni ajabu jinsi saratani ya kongosho inavyoweza kukufanya ufokasi kwenye kile ambacho ni muhimu zaidi.”15 Shukrani kwa wanaume na wanawake wa ajabu ambao waliona hitaji, hawakuhukumu, na walihudumu kama Mwokozi, Mike hakuwa amechelewa sana. Kwa baadhi, badiliko linaweza kuja mapema; kwa wengine; pengine upande mwingine wa pazia. Hata hivyo, ni lazima tukumbuke kwamba hatujachelewa na hakuna aliyepotea mbali na njia kiasi cha kutoweza kufikiwa na Upatnisho wa Yesu Kristo usio na mwisho, ambao hauna mipaka katika muda na uwezo wake.

Katika mkutano mkuu wa Oktoba iliyopita, Mzee Dale G. Renlund alifundisha kwamba “haijalishi kwa muda gani tumetoka kwenye njia … , wakati tunapoamua kubadilika, Mungu hutusaidia kurudi.”16 Uamuzi huo wa kubadilika, hata hivyo, mara nyingi ni matokeo ya mwaliko, kama vile “Nafikiri utafurahia kusikiliza ujumbe wa injili.” Jinsi ambavyo hakuna kuchelewa kwa Mwokozi, si mapema sana kwetu kualika.

Msimu huu wa Pasaka, kwa mara nyingine, unatupatia nafasi ya kipekee kutafakari kuhusu dhabihu kuu ya upatanisho ya Mwokozi wetu, Yesu Kristo, na kile Alichofanya kwa niaba ya kila mmoja wetu kwa gharama kubwa mno—gharama ambayo Yeye Mwenyewe alisema “yaliyosababisha [Yeye], mkuu kuliko wote, kutetemeka kwa sababu ya maumivu.” “Hata hivyo,” Anasema, “Mimi nikachukua na kukamilisha maandalizi yangu kwa wanadamu.”17

Ninashuhudia kwamba kwa sababu “Alikamilisha,” daima kuna tumaini. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha