2010–2019
Jicho la Imani
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Jicho la Imani

Kama tutachukua na kuchagua kile tunachokubali katika tangazo, tunatia wingu mtazamao wetu wa milele, na kuweka umuhimu mkubwa katika uzoefu wetu wa hapa na sasa.

Muda mfupi kabla ya Kusulubiwa Kwake, Yesu Alipelekwa mbele ya Pilato kwenye ukumbi wa hukumu. “Je wewe ni mfalme wa Wayahudi?” Pilato aliuliza kwa kejeli. Yesu Akajibu: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu. … mimi [nalikuja] ulimwenguni, ili niishuhudie kweli. Kila aliye wa hiyo kweli hunisikia sauti yangu.”

Pilato akajibu kwa shaka, “Kweli ni nini?”1

Katika ulimwengu wa leo swali “Kweli ni nini?” linaweza kuwa lenye utata wa kuumiza kwa akili ya kidunia.

Utafutaji kwa Google wa “Kweli ni nini?” huleta majibu zaidi ya milioni. Tuna habari zaidi kwenye simu zetu kuliko kwenye vitabu vyote kwenye maktaba iliyojengwa kwa matofali na chokaa. Tunaishi na habari na maoni mengi kupita kiasi. Sauti za kushawishi na kuvutia zinatuandama katika kila kona.

Tukiwa tumetekwa kwenye mkanganyiko wa hivi leo, si ajabu kuwa wengi wanajipeleka wenyewe kwenye maneno yaliyonenwa miaka 2500 iliyopita na Pythagoras kwa Socrates mdogo: “Kilicho kweli kwako”, alisema, “ni kweli kwako, na kilicho kweli kwangu, ni kweli kwangu”2

Ukweli kupitia Injili Iliyorejeshwa ya Yesu Kristo

Tukiwa tumebarikiwa na injili iliyorejeshwa ya Yesu Kristo, tunatangaza kwa unyenyekevu kuwa kuna baadhi ya vitu ambavyo ni kweli kabisa na kikamilifu. Kweli hizi za milele ni sawa kwa kila mwana na binti wa Mungu.

Maandiko yanafundisha, “Na ukweli ni maarifa ya mambo kama yalivyo, na kama yalivyokuwa, na kama yatakavyokuwa.”3 Ukweli unatazama mbele na nyuma, ukipanua mtazamo wetu wa sehemu yetu ndogo kulingana na muda.

Yesu alisema, “Mimi ndimi njia, na kweli na uzima.”4 Ukweli hutuonyesha njia kuelekea uzima wa milele, na huja tu kupitia Mwokozi wetu, Yesu Kristo. Hakuna njia nyingine.

Yesu Kristo anatufundisha jinsi ya kuishi, na, kupitia Upatanisho na Ufufuko Wake, hutupa msamaha wa dhambi zetu na kutokufa milele. Hii ni kweli kabisa.

Yeye hutufundisha kuwa haijalishi kama sisi ni matajiri au masikini, wenye kuheshimika au kutojulikana, wenye kwenda na wakati au watu wa kawaida. Badala yake, hamu yetu ya maisha ya duniani ni kuimarisha imani yetu katika Yesu Kristo, kuchagua mema badala ya mabaya, na kushika amri Zake. Wakati tukisherehekea ugunduzi wa kisayansi na dawa, kweli za Mungu zinapita ugunduzi huu.

Katika kupinga kweli za milele, kila mara kumekuwa na kweli bandia ili kuwachanganya watoto wa Mungu kutoka katika ukweli. Hoja za adui kila mara ni zile zile. Sikiliza hizi, zilizotolewa miaka 2,000 iliyopita:

“Hamwezi kujua vitu ambavyo hamvioni. … [Chochote ambacho mtu anafanya] si jinai.”

“[Mungu hakubariki, lakini] kila mtu [hufanikiwa] kulingana na akili zake [mwenyewe].”5

“Haileti maana kwamba kiumbe kama … Kristo … [angekuwa] Mwana wa Mungu.”6

“[Kile unachoamini ni tamaduni za upumbavu na ni upungufu wa [akili].”7 Inasikika kama leo, si ndiyo?

Pamoja na Urejesho wa Injili, Mungu ametupa njia ya kujifunza na kujua kweli muhimu za kiroho: tunajifunza kupitia maandiko matakatifu, sala zetu binafsi na uzoefu wetu binafsi, kupitia ushauri wa manabii na mitume walio hai, na kupitia mwongozo wa Roho Mtakatifu, ambaye anaweza kutusaidia “kujua ukweli wa vitu vyote.”8

Ukweli Unatambulika Kiroho

Tunaweza kujua vitu vya Mungu tunapovitafuta kiroho. Paulo alisema: “Mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. … [Kwa kuwa] yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. .”9

Angalia picha hii ya Michael Murphy. Kutoka katika mtazamo huu, ungepata ugumu kuamini kwamba ni muundo wa kisanaa wa jicho la binadamu. Hata hivyo, unapoangalia nukta kutoka katika mtazamo mwingine, unaona uzuri wa uumbaji wa msanii.

Vivyo hivyo, tunaona kweli za kiroho za Mungu kupitia mtazamo wa jicho la imani. Paulo alisema: “mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu: maana kwake huyo ni upuzi: wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni. .”10

Maandiko, sala zetu, uzoefu wetu binafsi, manabii wa leo, na karama ya Roho Mtakatifu vinatuletea mtazamo wa kiroho wa ukweli muhimu kwa ajili ya safari yetu hapa duniani.

Tangazo kupitia Jicho la Imani

Hebu tutazame Tangazo Kuhusu Familia kwa jicho imani.

Rais Gordon B. Hinckley alitambulisha “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu” kwa kauli hii: “Pamoja na ujanja mwingi unaopitishwa kama ukweli, kwa udanganyifu mwingi kuhusu viwango na thamani, pamoja na uvutiaji na ushawishi mwingi wa kuchukua mtazamo wa kidunia, tumehisi [kuwa]onya.”11

Tangazo linaanza: “Wanadamu wote—wanaume na wanawake—wameumbwa katika mfano wa Mungu. Kila mmoja ni mwana na binti mpendwa wa wazazi wa mbinguni, na hivyo basi, kila mmoja ana asili ya kiungu na takdiri.”

Hizi ni kweli za milele. Wewe na mimi si kama janga la asili.

Ninayapenda maneno haya, “Katika ulimwengu kabla ya maisha haya, wana na mabinti wa kiroho walimjua na kumwabudu Mungu kama Baba yao wa Milele na kukubali mpango wake.”12

Tuliishi kabla ya kuzaliwa kwetu. Utambulisho wetu binafsi umetiwa muhuri kwetu milele. Kwa njia tusizoelewa kikamilifu, ukuaji wetu wa kiroho huko katika maisha kabla ya haya unashawishi jinsi tulivyo hapa.13 Tuliukubali Mpango wa Mungu. Tulifahamu kuwa tungekumbana na ugumu, maumivu, na huzuni tukiwa duniani.14 Tulifahamu pia kuwa Mwokozi angekuja na kwamba wakati tunapothibitisha kustahili, tungeinuka katika Ufufuko, tukiwa na “utukufu juu ya vichwa [vyetu] milele na milele.”15

Tangazo ni la moja kwa moja: “Tunatangaza njia ambayo maisha ya dunia yanaumbwa imechaguliwa kitakatifu. Tunathibitisha utakatifu wa uhai na umuhimu wake katika mpango wa milele wa Mungu.”

Mpango wa Baba Yetu unahimiza waume na wake kuwaleta watoto ulimwenguni na kutupa jukumu la kuzungumza katika kuwalinda wale ambao hawajazaliwa.

Kanuni za Tangazo Zimeungana Vyema

Kama tutachukua na kuchagua kile tunachokubali katika tangazo, tunatia wingu mtazamao wetu wa milele, na kuweka umuhimu mkubwa katika uzoefu wetu wa hapa na sasa. Kwa kulitafakari kwa dhati tangazo kupitia jicho la imani, tunaelewa vyema zaidi jinsi kanuni zinavyoungana vyema, zikisaidizana, zikifunua mpango wa Baba juu ya watoto Wake.16

Je, tunapaswa kushangaa wakati manabii wa Bwana walio hai wanapotangaza nia Yake na, kwa baadhi, kubaki na maswali? Ndiyo, Baadhi hukataa sauti ya manabii papohapo,17 wakati wengine kwa dhati hutafakari maswali yao ya dhati—maswali ambayo yatajibiwa kupitia uvumilivu na jicho la imani. Kama tangazo lingekuwa limefunuliwa katika karne tofauti, bado kungekuwa na maswali, maswali tofauti na yale ya leo. Dhumuni mojawapo la manabii ni kutusaidia sisi katika kutatua maswali ya dhati.18

Kabla ya kuwa Rais wa Kanisa, Rais Russell M. Nelson alisema: “Manabii huona mbele. Wanaona hatari za kuumiza ambazo adui ameweka, au ataweka kwenye mapito yetu. Manabii pia wanaona uwezekano mkuu na fursa zinazowangoja wale wanaosikiliza kwa nia ya kutii.19

Ninashuhudia ukweli na nguvu ya kiroho ya sauti ya pamoja ya Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili.

Ulimwengu Unaondoka

Kipindi cha maisha yangu, tumeona mabadiliko makubwa katika mtazamo wa ulimwengu juu ya kanuni nyingi zilizofundishwa kwenye Tangazo. Wakati wa ujana wangu na miaka ya mapema ya ndoa, wengi duniani waliacha kiwango cha Bwana tunachokiita sheria ya usafi wa kimwili, ambapo mahusiano ya kimwili yanapaswa kuwa kati ya mume na mke waliooana kisheria. Kwenye umri wa miaka yangu ya 20 na 30, wengi waliacha ulinzi mtakatifu wa yule ambaye bado hajazaliwa, ambapo kutoa mimba kulikuwa ni jambo la kukubalika zaidi. Katika miaka ya hivi karibuni, wengi wameacha sheria ya Mungu kwamba ndoa ni muungano mtakatifu kati ya mume na mke.20

Kuwatazama wengi wakiondoka kutoka kwenye mipaka ambayo Bwana ameiweka inatukumbusha kuhusu siku ile Kapernaumu wakati Mwokozi alipotangaza utakatifu wake na kwa huzuni “wengi wa wanafunzi wake … [hawakuambatana] Naye.”

“Kisha Yesu akawaambia wale Kumi na Wawili, Je, Ninyi nanyi mwataka kuondoka?”

Petro akajibu:

“Bwana, twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.

“Na sisi tunaamini na tunajua kwamba wewe ndiye yule Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”21

Si wote Wanafaa Kikamilifu ndani ya Tangazo

Kuna wengi, vijana na watu wazima, walio waaminifu na wakweli katika injili ya Yesu Kristo, ingawa uzoefu wao wa sasa hauko sawia na tangazo la familia: watoto ambao maisha yao yametetemeshwa kwa talaka; vijana ambao marafiki zao wanakejeli sheria ya usafi wa kimwili; wanaume na wanawake waliotalikiwa ambao wameumizwa sana na mwenza asiye mwaminifu; waume na wake wasioweza kupata watoto; wanaume waliooa au wanawake walioolewa na mwenza asiyeshiriki imani yao katika injili ya urejesho; wanawake na wanaume waseja ambao, kwa sababu tofauti tofauti, hawajaweza kuoa au kuolewa.

Rafiki yangu mmoja kwa karibu miaka 20, ambaye napendezwa naye sana, hajaoa kwa sababu ya hali ya kuvutiwa na jinsia moja. Amekuwa mkweli kwa maagano yake ya hekaluni, amepanua ubunifu na vipaji vya kikazi, na amehudumu kwa heshima Kanisani na kwenye jamii. Hivi karibuni aliniambia, “Ninaweza kuona huruma kwa wale walio kwenye hali yangu wanaochagua kutotii sheria ya usafi wa kimwili katika dunia tunamoishi. Lakini si Kristo aliyetuamuru Tusiwe wa ulimwengu huu? Ni dhahiri kuwa viwango vya Mungu ni tofauti na vile vya ulimwengu.”

Sheria za mwanadamu mara nyingi huenda nje ya mipaka ya sheria za Mungu. Kwa wale wanaotamani kumpendeza Mungu, imani, uvumilivu na bidii kwa hakika vinahitajika.22

Mke wangu, Kathy pamoja nami tumemjua dada mseja, sasa akiwa katikati ya miaka ya 40, ambaye ana vipaji katika uwezo wake wa kikazi na hutumikia vyema katika kata yake. Yeye pia ametii sheria za Mungu. Aliandika:

“Ninatazamia siku ambayo nitabarikiwa kuwa na mume na watoto. Bado ninasubiri. Kuna nyakati, hali yangu huleta hisia za kusahaulika na kuwa peke yangu, lakini ninajaribu kutotazama kile nisicho nacho na badala yake kutazama kile nilichonacho na vile ninavyoweza kuwasaidia wengine.

“Huduma kwa familia yangu, kwenye kata yangu, na kwenye hekalu imenisaidia. Sijasahaulika wala kuwa peke yangu kwani mimi ni sehemu ya, na sisi sote ni sehemu ya, familia moja kubwa.”

Kuna Mmoja Anayeelewa

Wengine watasema, “Huelewi hali yangu.” Ninaweza nisielewe, lakini ninashuhudia kwamba kuna Mmoja ambaye anaelewa.23 Kuna Mmoja ambaye anajua mizigo yako kwa sababu ya dhabihu Yake aliyotoa katika bustani na msalabani. Unapomtafuta Yeye na kutii Amri Zake, ninaahidi kwamba Atakubariki na kuinua mizigo iliyo mizito kubeba peke yako. Atakupa marafiki wa milele na nafasi za kuhudumu. Muhimu zaidi, Atakujaza na roho yenye nguvu ya Roho Mtakatifu na kumulika kukubali kwake juu yako. Hakuna uchaguzi, wala mbadala ambao unapinga wenzi wa Roho Mtakatifu au baraka za milele, ni wa thamani kwetu.

Ninajua kwamba Mwokozi anaishi. Ninashuhudia kuwa yeye ni chanzo cha ukweli wote ulio muhimu na kuwa atatimiza baraka zote Alizoahidi kwa wale wanaotii amri zake. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Yohana 18:33, 36–38.

  2. William S. Sahakian and Mabel Lewis Sahakian, Ideas of the Great Philosophers (1966), 28.

  3. Mafundisho na Maagano 93:24.

  4. Yohana 14:6.

  5. Alma 30:15, 17.

  6. Helamani 16:18.

  7. Ona Alma 30:14, 23, 27.

  8. Moroni 10:5.

  9. Tafsiri ya Joseph Smith, 1 Wakorintho 2:11 [katika 1 Wakorintho 2:11, marejeo c]; 1 Wakorintho 2:14.

  10. 1 Wakorintho 2:14.

  11. Gordon B. Hinckley, “Simama Imara dhidi ya Hila za Ulimwengu,” Ensign, Nov. 1995, 100. Rais Russell M. Nelson hivi karibuni alielezea baadhi ya historia ya tangazo, kama ilivyofanyiwa ufupisho na Sheri Dew katika Umaizi kutoka kwenye Maisha ya Nabii: Russell M. Nelson (2019), 208:

    “Siku moja mnamo 1994, Akidi ya Mitume kumi na wawili walitumia siku yao kwenye chumba chao cha baraza kwenye Hekalu la Salt Lake wakijadili masuala ya familia. Walifikiria kila jambo kuhusu ongezeko la ueneaji wa ngono mpaka sheria za kila aina zinazoweza kupinga familia. Huu Haukuwa mjadala mpya, lakini siku hiyo ajenda nzima ilijikita kwenye mada hii muhimu.

    “Wale kumi na Wawili walitathmini vyote mafundisho na sera, wakitilia maanani yale mambo yasiyoweza kubadilishwa—mafundisho— na yale mambo ambayo pengine yangeweza kubadilishwa—sera. Walijadili masuala waliyoona yakija, pamoja na kuzidishwa kwa msukumo wa jamii wa ndoa za jinsia moja na haki za waliobadilisha jinsia. ‘Lakini haya hayakuwa mwisho wa yale tuliyoyaona’, Mzee Nelson Alielezea. ‘Tuliweza kuona juhudi za jamii tofauti kuondoa viwango vyote na vizuizi kwenye tendo la ngono. Tuliona mkanganyiko wa jinsia. Tuliyaona yote yakija.’

    “Mjadala huu wa muda mrefu, pamoja na mingine kwa muda, ilipelekea kwenye uamuzi kuwa Kumi na Wawili walipaswa kuandaa hati, au pengine Tangazo, likitoa muhtasari wa msimamo wa Kanisa juu ya familia na kuliwasilisha kwa Urais wa Kwanza kwa ajili ya kufikiriwa.”

  12. Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” Liahona, Mei 2017, 145.

  13. Rais Dallin H Oaks alisema: “Wanadamu wote waliowahi kuzaliwa hapa duniani walichagua mpango wa Baba na kuupigania. Wengi wetu pia tulifanya maagano na Baba Kuhusu kile ambacho tungefanya hapa duniani. Katika njia ambazo hazijafunuliwa, matendo yetu katika ulimwengu wa roho yanatushawishi katika maisha ya duniani. ” (“Mpango Mkuu wa Furaha,” Ensign, Nov. 1993, 72).

  14. Ona Dallin H. Oaks, “Ukweli na Mpango,” Liahona, Nov. 2018, 25–28.

  15. Ibrahimu 3:26.

  16. Rais Dallin H. Oaks amesema:

    “Mtakatifu wa Siku za Mwisho aliyeongoka huamini kwamba tangazo la familia, lililotolewa karibu robo karne iliyopita na sasa kutafsiriwa katika lugha nyingi, ni msisitizo wa Bwana wa ukweli wa injili tunaohitaji kutupitisha katika changamoto za sasa kwenye familia. …

    “Ninashuhudia kwamba tangazo juu ya familia ni maelezo ya ukweli wa milele, mapenzi ya Bwana kwa watoto Wake wanaotafuta uzima wa milele. Limekuwa ni msingi wa mafundisho na utamaduni wa Kanisa kwa miaka 22 iliyopita na itaendelea hivyo kwa baadaye. Lifikirie hivyo, lifundishe, liishi, na utabarikiwa unaposonga mbele kuelekea Uzima wa milele. ...

    “... Ninaamini mtazamo wetu kwa na matumizi ya tangazo la familia ni moja ya majaribu hayo kwa kizazi hiki. Ninaomba kwa ajili ya Watakatifu wote wa Siku za Mwisho kusimama imara katika jaribu hilo” (“Mpango na Tangazo,” Liahona, Nov. 2017, 30–31).

  17. Rais Russell M. Nelson amesema: “Kuna wale wanaotuita wabaguzi, lakini wabaguzi ni wale wasioturuhusu sisi kuhisi tunavyohisi lakini wanaotaka sisi tuwaruhusu wao kuhisi wanavyohisi. Msimamo wetu hatimaye unahusu sheria ya usafi wa kimwili. Hizi Amri Kumi bado ni halali leo. Hazijafutwa. ... Si jukumu letu kubadili sheria ambazo Mungu ameamuru” (katika Dew, Umaizi kutoka katika Maisha ya Nabii: Russell M. Nelson, 212).

  18. “Huku familia ikiwa chini ya shambulizi kote ulimwenguni, kweli za tangazo la familia zitakuimarisha.

    “Ninyi vijana wazuri wa uzao wa kifalme, mnahitaji kuelewa matokeo ya kina ya maelezo yaliyokanganywa ya jamii kuhusu maana hasa ya ndoa. Mjadala wa sasa unajumuisha swali la ikiwa watu wawili wa jinsia moja wanaweza kuoana. Ikiwa una swali kuhusu msimamo wa Kanisa juu ya hili au jambo lingine muhimu, tafakari kwa maombi, na kisha sikiliza jumbe za kinabii wakati wa Mkutano Mkuu ujao wa Kanisa wa Oktoba. Hotuba hizo zenye mwongozo, pamoja na msukumo kutoka kwa Roho Mtakatifu, vitaleta uelewa kamili na wa kweli akilini mwako.” (Russell M. Nelson, “Vijana wa Uzao Mteule: Ni nini Mtachagua?” [Church Educational System devotional for young adults, Sept. 6, 2013], broadcasts.

  19. Russell M. Nelson, “Stand as True Millennials,” Liahona, Oct. 2016, 53.

  20. Rais Nelson Amesema: “Serikali za kiraia zinaathiriwa sana na mitindo ya kijamii na falsafa za kidunia zinapoandika, kuandika tena na kutekeleza sheria. Licha ya kile sheria za kiraia inaweza kuwekwa, mafundisho ya Bwana kuhusu ndoa na maadili hayawezi kubadilishwa. Kumbuka: dhambi, hata ikihalalishwa na mwanadamu, bado ni dhambi machoni pa Mungu!”(“Maamuzi ya Milele,” Liahona, Nov. 2013, 108).

  21. Yohana 6:66–69.

  22. ona Alma 32:41–43; Nimevutiwa kila mara kwamba katika sura hii kuu juu ya kukuza imani yetu, wema wa imani, uvumilivu, na bidii vinatajwa pamoja katika kila moja ya mistari mitatu ya mwisho.

  23. Ona Alma 7:12; Yesu Kristo aliteseka si tu kwa ajili ya dhambi zetu bali kwa unyonge wetu vilevile: “Na atajichukulia kifo, ili afungue kamba za kifo ambazo zinafunga watu wake; na atajichukulia unyonge wao, ili moyo wake ujae rehema, kulingana na mwili, ili ajue kulingana na mwili jinsi ya kuwasaidia watu wake kulingana na unyonge wao.” (Visawe vya magonjwa vingekuwa ugonjwa, udhaifu, taabu, upungufu.) Ona Mafundisho na Maagano 88:6: “Alishuka chini ya vitu vyote, kiasi kwamba alielewa vitu vyote, ili aweze kuwa katika vyote na ndani ya vitu vyote, nuru ya ukweli;”

Chapisha