2010–2019
Kufanyia Mazoezi Misuli Yetu ya Kiroho
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Kufanyia Mazoezi Misuli Yetu ya Kiroho

Kama vile kusoma na kujifunza tu kuhusu misuli hakutoshi kuijenga misuli, kusoma na kujifunza kuhusu imani bila kuongeza matendo hakutoshi kujenga imani.

Nina shukrani kwa baraka ya kuwa na mwili wa nyama na mifupa, ambao ni zawadi ya kustaajabisha kutoka kwa Baba yetu wa Mbinguni. Miili yetu ina zaidi ya misuli 600.1 Mingi ya misuli hiyo huitaji mazoezi ili iweze kuwa katika hali ya kufanya shughuli zetu za kila siku. Tungeweza kutumia juhudi kubwa kiakili kusoma na kujifunza kuhusu misuli yetu, lakini kama tunafikiri hii itaifanya iwe na nguvu zaidi, tutakatishwa tamaa. Misuli yetu hukua pale tu tunapoitumia.

Nimekuja kugundua kwamba karama za roho zina sifa sawa na hiyo. Nazo pia zinahitaji kufanyiwa mazoezi ili zikue. Karama ya roho ya imani, kwa mfano, si tu hisia au hali ya muda; ni kanuni ya matendo ambayo mara nyingi hutokea katika maandiko ikiunganishwa kwenye kitendo tumia.2 Kama vile kusoma na kujifunza tu kuhusu misuli hakutoshi kuijenga misuli, kusoma na kujifunza kuhusu imani bila kuongeza matendo hakutoshi kujenga imani.

Wakati nilipokuwa na miaka 16, kaka yangu mkubwa, Ivan ambaye alikuwa na miaka 22 wakati huo, siku moja alikuja nyumbani na kushiriki habari fulani na familia. Alikuwa ameamua kubatizwa katika Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Wazazi wetu walimwangalia kwa mashaka, na ninakumbuka sikuelewa kabisa kilichokuwa kikiendelea. Mwaka mmoja hivi baadaye, alitupatia habari ya kushangaza zaidi: alikuwa ameamua kutumikia kama mmisionari wa Kanisa, kitu ambacho kilimaanisha kwamba tusingemuona kwa miaka miwili. Wazazi wangu hawakufurahishwa na habari hii; hata hivyo, niliona nia ya dhati ambayo iliongeza kuvutiwa kwangu kwake na uamuzi aliokuwa amefanya.

Miezi baadaye, wakati Ivan akitumikia misheni yake, nilikuwa na fursa ya kuandaa mapumziko pamoja na baadhi ya wanafunzi wenzangu. Tulitaka kusherehekea mwisho wa miaka yetu ya shule ya upili na kutumia siku kadhaa ufukoni.

Niliandika barua kwa kaka yangu mmisionari, nikimwelezea kuhusu mapumziko yangu ya majira ya joto. Alinijibu kwamba mji aliokuwa akitumikia ulikuwa njiani kuelekea mahala nilipokuwa nikienda. Niliamua kwamba ilikuwa ni wazo zuri kupita na kumtembelea. Haikuwa hivyo mpaka baadaye nilipojua kwamba wamisionari hawakutakiwa kutembelewa na wanafamilia wao.

Niliandaa mipango yote. Nakumbuka nilipokaa kwenye basi nikifikiria nyakati zote nzuri mimi na Ivan tungekuwa nazo pamoja katika siku hii nzuri yenye jua. Tungepata kifungua kinywa, tungeongea, tungecheza kwenye mchanga, tungelala juani—ni jinsi gani tungeenda kuwa na wakati wa furaha!

Wakati basi lilipofika kituoni, nilimuona Ivan akiwa amesimama kando ya kijana mwingine, wote wakiwa katika shati nyeupe na tai. Nilishuka kutoka kwenye basi, tulikumbatiana, na akamtambulisha mwenzake. Bila kupoteza dakika nyingine, nilimwambia kaka yangu mipango yangu katika siku ile, lakini ni kidogo tu nilichojua kuhusu kipi Ivan alikuwa amepanga. Aliniangalia, akatabasamu, na kusema, “Sawa! Hata hivyo, tunahitaji kufanya baadhi ya majukumu kwanza. Je unaweza kuja pamoja nasi?” Nilikubali, nikifikiri tungekuwa na wakati wa kutosha kufurahia ufukoni baadaye.

Siku hiyo, kwa zaidi ya saa 10, nilitembea kupita mitaa ya mji ule pamoja na kaka yangu na mwenzake. Nilitoa tabasamu kwa watu siku nzima. Niliwasalimia watu ambao sikuwahi kuwaona maishani mwangu. Tuliongea na kila mtu, tuligonga hodi milangoni mwa watu wageni, na kuwatembelea watu ambao kaka yangu na mwenzake walikuwa wakiwafundisha.

Wakati wa moja ya matembezi hayo, kaka yangu na mwenzake walikuwa wakifundisha kuhusu Yesu Kristo na mpango wa wokovu. Ghafla, Ivan akaacha kuongea na kuniangalia. Kwa mshangao wangu, aliniomba kwa upole kushiriki mawazo yangu kuhusu kile kilichokuwa kikifundishwa. Chumba kilikuwa kimya, na macho yote yakawa kwangu. Kwa ugumu fulani, hatimaye nilipata maneno na kushiriki hisia zangu kuhusu Mwokozi. Sikujua kama nilichokishiriki kilikuwa sahihi au la. Kaka yangu kamwe hakunisahihisha; badala yake, alinishukuru kwa kushiriki mawazo na hisia zangu.

Wakati wa masaa yale pamoja, kaka yangu na mwenzake hawakutumia hata dakika moja kufundisha somo jipya kwangu, hata hivyo nilipata uelewa zaidi kuliko mazungumzo yangu yote ya awali pamoja na yeye. Nilishuhudia jinsi muonekano ulivyokuwa ukibadilika wakati watu walipopokea nuru ya kiroho katika maisha yao. Niliona jinsi baadhi yao walivyopata tumaini katika ujumbe, na nilijifunza jinsi ya kutumikia wengine na kusahau kuhusu nafsi yangu na matamanio yangu. Nilikuwa nikifanya kile mwokozi alichofundisha: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe.”3

Nikiangalia nyuma, nagundua kwamba imani yangu ilikua siku ile kwa sababu kaka yangu alinipa fursa ya kuiweka katika matendo. Niliitumia wakati tukisoma maandiko, tukitafuta watu wa kufundisha, tukishuhudia, tukitumikia wengine na mengineyo. Hatukuweza kwenda kulala kwenye jua siku ile, lakini moyo wangu ulifunikwa na nuru kutoka mbinguni. Sikuona hata punje moja ya mchanga ufukoni, lakini nilihisi imani yangu kukua kama punje ya haradali.4 Sikutumia siku yenye jua kama mtalii, lakini nilipata uzoefu wa kuvutia, na bila kutambua, nilikuwa mmisionari—bila hata kuwa muumini wa Kanisa!

Fursa za Kuimarisha Misuli ya Imani

Kwa sababu ya Urejesho wa injili, tunapata kuelewa jinsi Baba yetu wa Mbinguni anavyotusaidia kukuza karama za roho. Na inawezekana kwamba Atatupatia fursa za kukuza karama hizo kuliko kuzitoa tu kwetu bila juhudi za kiroho na kimwili. Kama tutakuwa kwenye tuni na Roho Wake, tutajifunza kutambua fursa hizo na kisha kuzitumia.

Kama tutatafuta uvumilivu zaidi, tutajikuta tukihitajika kuufanyia kazi wakati tukisubiri jibu. Kama tunataka kuwa na upendo zaidi kwa jirani yetu, tunaweza kuuongeza kwa kukaa karibu na mtu mgeni kanisani. Ni vivyo hivyo katika imani: wakati mashaka yanapokuja mawazoni mwetu, kuamini katika ahadi za Bwana kutahitajika ili kusonga mbele. Katika njia hii, tunafanyia mazoezi misuli ya kiroho na kuikuza kuwa chanzo cha nguvu katika maisha yetu.

Pengine haitakuwa rahisi mwanzoni, na inaweza hata kuwa changamoto kubwa. Maneno ya Bwana, kupitia nabii Moroni, yanatumika kwetu hivi leo: “Na ikiwa watu watakuja kwangu nitawaonyesha udhaifu wao. Ninawapatia watu udhaifu ili katika udhaifu wao wawe wanyenyekevu; na neema yangu inatosha watu wote ambao hujinyenyekeza mbele yangu; kwani wakijinyenyekeza mbele yangu, na kuwa na [au kutumia] imani ndani yangu, ndipo nitafanya vitu dhaifu kuwa vya nguvu kwao.”5

Nina shukrani kwa kaka Ivan, ambaye si tu alishiriki injili pamoja nami lakini pia kwa njia isiyo ya moja kwa moja alinialika kuiishi na kutambua udhaifu wangu. Alinisaidia kukubali mwaliko wa Bwana: “Njoo, unifuate”6—kutembea jinsi Mwokozi alivyotembea, kutafuta jinsi Mwokozi alivyotafuta, na kupenda jinsi Mwokozi anavyotupenda. Miezi baadaye, baada ya uzoefu wangu wa umisionari, niliamua kubatizwa na kutumikia misheni.

Acha tukubali mwaliko wa Rais Russell M. Nelson na kwa nia kuja kwa Mwokozi7 kwa kuitambua ile misuli ambayo inahitaji kazi ya kiroho zaidi na kuanza kuifanyia mazoezi. Hizi ni mbio za masafa marefu, maratoni, si tu za kasi kwa muda mfupi, hivyo usisahau zile shughuli ndogondogo lakini endelevu za kiroho ambazo zitaimarisha ile misuli muhimu ya kiroho. Kama tunataka kuongeza imani yetu, basi tufanye vitu vinavyohitaji imani.

Ninatoa ushahidi wangu kwamba sisi ni watoto wa Baba mpendwa wa Mbinguni. Mwana Wake, Yesu Kristo, Anatupenda. Alikuja katika ulimwengu huu kutuonyesha njia na kisha akatoa maisha Yake kwa hiari ili kutupatia tumaini. Mwokozi anatualika kufuata mfano Wake mkamilifu, kutumia imani yetu Kwake na katika Upatanisho Wake, na kukuza karama zote za roho ambazo tumebarikiwa kuwa nazo. Yeye ni njia. Huu ni ushuhuda wangu katika jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha