2010–2019
Kula na Kusherehekea Maneno ya Kristo
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Kula na Kusherehekea Maneno ya Kristo

Kula na kusherehekea maneno ya Kristo kunaweza kutokea wakati wowote ikiwa tutatayarisha mioyo yetu.

Baba yetu wa Mbinguni anatupenda. Yeye ametoa mpango kamili kwa ajili yetu kufurahia baraka Zake. Katika maisha haya, wote tumealikwa kuja kwa Kristo na kupokea injili ya urejesho ya Yesu Kristo kupitia ubatizo, kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu, na kuishi injili kwa uaminifu. Nefi anaelezea kujitolea kwetu kwa ajili ya kubatizwa kama kuingia “njia nyembamba na iliyosonga” na anatukumbusha tuendelee “kusonga mbele tukiwa na imani imara katika Kristo, … tukila na kusherehekea neno la Kristo, kuvumilia hadi mwisho,” ili tuweze kupokea baraka zote ambazo Baba wa Mbinguni ameweka kwa ajili yetu (2 Nefi 31:19–20).

Nefi anatukumbusha zaidi kwamba kama “tutashiriki maneno ya Kristo,” “yatatuelezea [sisi] vitu vyote ambavyo [sisi] tunastahili kutenda” (2 Nefi 32:3) na kwamba tutakuwa na uwezo wa kushinda “mishale ya moto ya adui” (1 Nefi 15:24).

Kula Na Kusherehekea Ni Nini?

Wakati nilipokuwa mdogo, nilidhani kula na kusherehekea ilikuwa kwa urahisi kula mlo mkubwa wenye wali, sushi, na mchuzi wa soya. Sasa ninajua kwamba kula na kusherehekea kwa kweli ni zaidi ya kufurahia chakula kitamu. Ni uzoefu wa shangwe, kustawisha, kusherehekea, kushiriki, kuonyesha upendo kwa familia na wapendwa, kutoa shukrani zetu kwa Mungu, na kujenga mahusiano wakati ukifurahia chakula kingi, kitamu sana. Ninaamini wakati tunakula na kusherehekea maneno ya Kristo, tunapaswa kuwa tunafikiria kuhusu uzoefu kama huo. Kula na kusherehekea maandiko si tu kuyasoma. Kunapaswa kutuletea shangwe ya kweli na kujenga uhusiano wetu na Mwokozi.

Hili linafundishwa wazi kabisa katika Kitabu cha Mormoni. Kumbuka ndoto ya Lehi ambapo aliona mti, “ambao matunda yake ya[na]tamanika kumfurahisha mwanadamu.” Matunda haya yanawakilisha upendo wa Mungu, na Lehi anapoonja tunda, “lilikuwa … tamu, zaidi ya yote ambayo [a]likuwa ameonja.” “Lilijaza nafsi [yake] na shangwe tele” na ni kitu ambacho anataka kushiriki na familia yake (1 Nefi 8:10–12).

Wakati tunapokula na kusherehekea, pia tunaweza kugundua kwamba kiasi au aina ya chakula tulicho nacho si muhimu ikiwa mioyo yetu imejazwa na upendo. Familia ya Lehi iliishi kwa kula nyama mbichi nyikani, lakini Nefi alielezea majaribu haya magumu, akisema, “Na baraka kuu za Bwana zilikuwa nasi” kwamba “bibi zetu … walikuwa na nguvu” na waliweza “kusafiri bila kunung’unika” (1 Nefi 17:1–2).

Kula na kusherehekea wakati mwingine kunajumuisha kufanya majaribio na kuonja. Alma anazungumza kuhusu mbegu nzuri kupandwa katika mioyo yetu. Tunapoifanyia majaribio, tutagundua kwamba mbegu inaanza “kuwa nzuri” (ona Alma 32:28–33).

Kula na kusherehekea Maneno ya Kristo

Baraka za kula na kusherehekea maneno ya Kristo ni za nguvu na zenye kubadili maisha. Kuna tatu hasa ambazo ningependa kuwaalika mzitumie katika maisha yenu.

Kwanza, maneno ya Kristo yanaweza kutusaidia “kuongeza uwezo [wetu] wa kiroho wa kupokea ufunuo” (Russell Nelson, “Ufunuo kwa ajili ya Kanisa, Ufunuo kwa ajili Ya Maisha Yetu,” Liahona, Mei 2018, 96) na kutuongoza salama katika maisha yetu yote. Mormoni anafundisha kwamba maneno ya Kristo yana “maelekezo makubwa ya kuongoza watu kufanya yale ambayo [ni] haki,” na kwamba yana nguvu zaidi ya kitu chochote “upanga” unachoweza kutimiza (Alma 31:5). Wakati nilipotafuta busara ya Mungu katika kukabiliana na changamoto zangu mwenyewe, daima wakati ambapo nimejaribu “uwezo wa neno la Mungu” (Alma 31:5), nimehisi kutiwa msukumo na kuwezeshwa kufanya maamuzi ya busara, kushinda majaribu, na kubariki maisha yangu kwa ongezeko la imani katika Kristo na upendo kwa wale wanaonizunguka. Nabii wetu, Rais Russell M. Nelson amefundisha kwamba “katika siku zijazo, haitawezekana kunusurika kiroho bila uzoefu wa kuongoza, kuelekeza, kufariji na ushawishi endelevu wa Roho Mtakatifu.” (“Ufunuo kwa ajili ya Kanisa, Ufunuo kwa ajili Ya Maisha Yetu,” 96). Ufunuo unaohitajika utakuja wakati tunapojaribu “uwezo wa neno,” na neno hilo litakuwa na nguvu zaidi ya kitu chochote ambacho tunaweza kujaribu au kufikiria.

Pili, wakati tunapambana na utambulisho wetu wenyewe na kukosa kujiamini, “neno la kupendeza la Mungu” (Yakobo 2:8) katika maandiko litatusaidia kujua sisi hasa ni kina nani na kutupatia nguvu zaidi ya zile tulizonazo. Kutambua utambulisho wangu kama Mtoto wa Mungu ilikuwa mojawapo ya nyakati nzuri zaidi ambazo nimewahi kuwa nazo. Mapema katika miaka yangu ya ujana, sikufahamu chochote kuhusu mafundisho ya Mwokozi. Mara ya kwanza niliposoma Agano Jipya, maneno ya Kristo kwa kweli yaliiponya nafsi yangu iliyojeruhiwa. Niligundua ya kwamba sikuwa peke yangu na kwamba mimi ni mtoto wa Mungu. Nilipotambua utambulisho wangu wa kweli mbele za Mungu, niligundua uwezo wangu usio na kikomo kupitia Upatanisho wa Kristo.

Enoshi vile vile alishiriki uzoefu wake binafsi kuhusu kuelimika kunakotokana na kutafakari maneno ya Kristo. Enoshi aliporuhusu maneno ambayo baba yake alimfundisha kuhusu “uzima wa milele, na shangwe ya watakatifu, [kupenya] ndani ya moyo [wake],” nafsi yake “ilipata njaa; na [yeye] alipiga magoti mbele ya Muumba [wake] … kwa sala kuu” (Enoshi 1:3–4). Katika sala hiyo alikuja kumjua Mwokozi na kujifunza kwamba tuna thamani kubwa, tunapendwa, na tunaweza kusamehewa makosa yetu, na kwa kweli sisi ni watoto wa Mungu.

Tatu, tunaweza kuinua maisha ya wengine kupitia maneno ya Kristo. Jinsi ambavyo Enoshi alikuwa na wakati na mahali pake ambapo maneno ya Kristo yaligusa moyo wake, Bwana atafanya sehemu Yake kugusa mioyo ya wale ambao pamoja nao tungependa kushiriki injili. Wengi wetu twaweza kuwa tumehisi kufa moyo wakati tulipojaribu kumwalika mtu fulani kusikiliza injili kwa sababu matokeo tuliyotarajia hayakufuata. Bila kujali matokeo, Bwana anatualika tufungue vinywa vyetu na kushiriki ujumbe wa injili pamoja na wengine.

Miaka miwili iliyopita, Bwana aligusa moyo wa mama yangu mpendwa, ambako kulimsaidia kupokea ibada ya ubatizo. Nilikuwa nimesubiri kwa ajili ya siku hiyo kufika kwa takriban miaka 35. Ili aweze kufanya uamuzi huo, waumini wengi wa Kanisa kwa kweli walimhudumia jinsi ambavyo Kristo angefanya. Jumapili moja, alihisi kwamba alihitaji kwenda kanisani. Alifuata msukumo huo. Alipokuwa ameketi kwenye safu ya mbele akisubiri kuanza kwa huduma ya sakramenti, mvulana wa miaka minne alisimama mbele yake na kumtazama. Alimsalimia kwa tabasamu. Mvulana huyo mdogo aliondoka katika uwepo wake ghafla na kurudi kwenye kiti chake, ambacho kilikuwa upande mwingine wa safu ambapo mama yangu alikuwa ameketi. Mvulana huyu mdogo alichukua kitu kutoka kwenye kiti chake akarudi na kumpatia mama yangu kitabu cha nyimbo za kanisa na kurudi kwenye kiti chake. Mama yangu aligundua kitabu cha nyimbo za kanisa kilikuwa kimewekwa kwenye kila kiti katika nyumba ya mkutano. Angeweza kwa urahisi kuchukua kimoja kutoka kwenye kiti kando yake. Hata hivyo, alivutiwa sana na kitendo cha ukarimu na kisicho na ubaya cha mvulana, ambacho alijifunza nyumbani na kanisani. Ulikuwa wakati mwororo kwake. Alikuwa na msukumo wenye nguvu kwamba Mungu alikuwa anamwalika aje amfuate Mwokozi. Alihisi kwamba alihitaji kubatizwa. Mvulana huyu mdogo hakutafuta kutambuliwa kwa kile alichofanya, lakini kwa urahisi alifanya kila awezalo kuishi neno la Mungu na kumpenda jirani yake. Ukarimu Wake ulisababisha badiliko muhimu sana la moyo ndani ya mama yangu.

Maneno ya Kristo yatagusa mioyo kwa kina na kufungua macho ya wale ambao bado Hawamuoni. Katika njia ya kuelekea Emau, wanafunzi wawili walitembea na Yesu. Walikuwa na huzuni na hawakuelewa kwamba Mwokozi alikuwa ameshinda mauti. Katika huzuni yao, hawakutambua kwamba Kristo aliye hai alikuwa akitembea pamoja nao. Ingawaje Yesu “aliwaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe,” bado hawakumtambua Yeye kama Mwokozi aliyefufuka hadi walipoketi na kumega mkate pamoja Naye. Kisha “macho” yao yakafunguliwa. Wakati sisi—au rafiki zetu, washiriki, na majirani—tunapokula na kusherehekea na kumega mkate pamoja Naye, macho ya ufahamu wetu yatafunguliwa. Wakati wanafunzi waliokuwa Emau walipotafakari kuhusu wakati walipokuwa na Mwokozi, walisema kwamba mioyo yao iliwaka ndani yao wakati alipowafunulia maandiko (ona Luka 24:27–32). Hili litakuwa kweli kwa kila mmoja wetu.

Hitimisho

Kwa kuhitimisha, ninashuhudia ya kwamba kula na kusherehekea maneno ya Kristo kunaweza kutokea wakati wowote ikiwa tutatayarisha mioyo yetu kuyapokea. Kula na kusherehekea maneno ya Kristo kutaleta ufunuo unaoendeleza maisha, kuthibitisha upya utambulisho wetu wa kweli na thamani yetu mbele ya Mungu kama mtoto wake, na kuwaongoza rafiki zetu kwa Kristo na uzima wa milele. Acha nitamatishe kwa kurudia mwaliko wa Nefi wakati aliposema: “Lazima msonge mbele mkiwa na imani imara katika Kristo, mkiwa na mng’aro mkamilifu wa tumaini, na upendo kwa Mungu na wanadamu wote. Kwa hiyo, kama mtasonga mbele, mkila na kusherehekea neno la Kristo na mvumilie hadi mwisho, tazama, hivi ndivyo asema Baba: Mtapokea uzima wa milele” (2 Nefi 31:20). Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha