2010–2019
Kusikia Sauti Yake
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Kusikia Sauti Yake

Katika ulimwengu wenye sauti nyingi zinazoshindana, Baba yetu wa Mbinguni amefanya iwezekane kwetu kusikia na kuifuata Yake.

Mapema asubuhi hii, kaka wa mke wangu amempa mke wangu ujumbe ambao mke wangu alimwandikia mama yake miaka mingi iliyopita. Wakati huo, Dada Homer alikuwa binti mdogo. Kwa sehemu, ujumbe wake ulisomeka, “Mama Mpendwa, samahani kwa kutotoa ushuhuda wangu leo—lakini nakupenda.” tulipokwenda kupata chakula cha mchana, niliwaza kwamba lile lilikuwa ni jambo la kuvutia. hivyo niliketi, na niliandika ujumbe uliosema, “Mpendwa Rais Nelson, samahani sikutoa hubiri langu leo—lakini nakupenda.” Kwa kiasi fulani hilo halikuonekana la kupendeza. hivyo tupo hapa, na nina furaha kuongeza maneno yangu kwenye yale ambayo yamezungumzwa katika kikao hiki leo.

Miaka mingi iliyopita, nilisafiri kwenye ndege ndogo pamoja na rubani mpya aliyethibitishwa kwenye mitambo. Mwishoni mwa safari yetu, tuliruhusiwa kutua. Lakini tulipokaribia ardhi, nilisikia kengele kwenye chumba cha rubani ikimtahadharisha rubani “kupaa juu.” Rubani alimtazama msaidizi wake mwenye uzoefu zaidi, ambaye alionyesha uelekeo wa chini, mbali na njia, na kusema, “Sasa!”

Ndege yetu kwa haraka ilisogea kushoto na chini, kisha kupaa kurudi kwenye mwinuko unaofaa, ikaingia tena katika mpangilio wa kutua, na kufika salama mwisho wa safari yetu. Tuligundua baadaye kwamba ndege nyingine ilikuwa imeruhusiwa kuondoka. Tungefuata maelekezo ya kengele, tungeielekea, badala ya kuiepuka, ndege iliyokuwa ikija mbele. Uzoefu huu ulinifundisha masomo mawili muhimu: Kwanza, katika hali za hatari katika maisha yetu, tutasikia sauti nyingi zikishindania usikivu wetu. Na pili, ni muhimu kwamba tusikilize sauti sahihi.

Sauti Zinazoshindana

Tunaishi katika ulimwengu wenye sauti nyingi zikitafuta usikivu wetu. Pamoja na habari zote mpya, tweets, blogs, podcasts, na ushauri wa kushawishi kutoka kwa Alexa, Siri, na wengine, inaweza kuwa vigumu kujua sauti ipi tuiamini. Wakati mwingine tunategemea halaiki kwa ajili ya mwongozo katika maisha yetu, tukidhani wingi wa watu utatupatia chanzo bora cha ukweli. Wakati mwingine “tunasita … kati ya mawazo mawili,”1 tukichagua kuwa “si baridi wala moto.”2 Bado wakati mwingine tunafuata kile kilicho rahisi, tukifokasi kwenye sauti moja au jambo moja kutuongoza, au kutegemea kila kitu kwenye uwezo wetu wenyewe wa kufikiri.

Wakati kila moja ya mbinu hizi inaweza kuwa yenye msaada, uzoefu unafundisha kwamba daima si za kutegemewa. Kile kilicho maarufu si daima kile kilicho bora. Kusita kati ya mawazo mawili hakuleti mwelekeo. Urahisi mara chache huongoza kwenye vitu vya muhimu. Uimara kwenye sauti moja au jambo moja unaweza kudhoofisha uwezo wetu wa kuona. Na kutegemea tu kwenye fikra zetu wenyewe kunaweza kutuongoza kwenye mzubao mkubwa wa mawazo kiakili. Kama hatuko makini, sauti zisizo sahihi zinaweza kutuvuta mbali kutoka kwenye kiini cha injili hadi mahali ambapo imani inakuwa ngumu kuendeleza, na tunapata kidogo zaidi ya utupu, uchungu, na kutoridhika.

Kusikiliza Sauti Isiyo Sahihi

Acha nionyeshe kile ninachomaanisha kwa kutumia analojia na mfano wa maandiko. Wapanda milima kwa kawaida huita mwinuko juu ya mita 8,000 kama “ukanda wa kifo” kwa sababu, katika urefu huo, hakuna oksijeni ya kutosha kuendeleza uhai. Kuna mfanano wa kiroho kwenye ukanda wa kifo. Kama tunatumia muda mrefu mahali pasipo na imani, sauti zinazoonekana zenye makusudio mazuri zinatunyima oksijeni ya kiroho tunayohitaji.

Katika Kitabu cha Mormoni, tunasoma juu ya Korihori, ambaye alikuwa na uzoefu huo. Alifurahia umaarufu mkubwa kwa sababu mafundisho yake yalikuwa “yanapendeza [kwa] akili ya kimwili.”3 Alisema kwamba wazazi na manabii wanafundisha tamaduni za kipumbavu zilizokusudiwa kuzuia uhuru na kudumisha ujinga.4 Alitaka kwamba watu wawe huru kufanya chochote wanachochagua kwa sababu amri si kitu zaidi ya vizuizi rahisi vilivyobuniwa.5 Kwake, imani katika Upatanisho wa Yesu Kristo ilikuwa “matokeo ya akili yenye wazimu,” iliyotengenezwa kwa kuamini katika kiumbe ambacho hakiwezi kuwepo kwa sababu Yeye hawezi kuonekana.6

Korihori alitengeneza vurugu nyingi kwamba aliletwa mbele ya mwamuzi mkuu na kuhani mkuu. Hapo, aliinuka “juu kwa maneno ya majivuno makubwa,” akiwakosoa viongozi na kutaka ishara. Ishara ilitolewa. Alipigwa ili kwamba asiweze kuongea. Korihori kisha akatambua alikuwa amedanganywa, na alipofikiria kweli za thamani alizozikataa, aliomboleza, “nilikuwa kila siku najua.”7

Korihori kisha aliomba chakula mpaka alipokanyagwa hadi kufa na kundi la Wazoramu.8 Mstari wa mwisho katika hadithi yake una kumbukumbu hii ya kuhuzunisha: “Na hivyo tunaona kwamba ibilisi hatasaidia watoto wake siku ya mwisho, lakini anawachukua kwa mbio hadi jahanamu.”9

Sauti Sahihi

Kwa sababu Baba yetu wa Mbinguni anataka kilicho kizuri kwetu, Yeye hufanya iwezekane kwetu kusikia sauti Yake. Mara nyingi, tunamsikia Yeye kupitia misukumo inayotolewa na Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu ni mshiriki wa tatu wa Uungu. Anashuhudia juu ya Baba na Mwana,10 alitumwa “kutufundisha [sisi] yote,”11 na “atatuonyesha [sisi] vitu vyote ambavyo [sisi] tunastahili kutenda.”12

Roho huzungumza na watu tofauti kwa njia tofauti, na anaweza kuzungumza na mtu mmoja katika njia tofauti kwa nyakati tofauti. Kama matokeo, kujifunza njia nyingi Anazozungumza nasi ni jitihada ya maisha yote. Wakati mwingine, Yeye huzungumza kwenye “akili na mioyo [yetu]”13 kwa sauti ambayo ni ndogo, lakini yenye nguvu ikiwapenya “wale … wanaoisikia hadi moyoni.”14 Nyakati zingine, misukumo Yake “hutawala akili [zetu]” au “kujisukuma kwenye hisia [zetu].”15 Nyakati zingine, mioyo yetu “itawaka ndani [yetu].”16 Bado nyakati zingine, Yeye hujaza nafsi zetu kwa shangwe, huangaza akili zetu,17 au huzungumza amani kwenye mioyo yetu yenye hofu.18

Kuipata Sauti Yake

Tutaipata sauti ya Baba yetu katika sehemu nyingi. Tutaipata tunaposali, tunaposoma maandiko, na tunapohudhuria kanisani, tunapojihusisha katika mijadala ya kweli, au kwenda hekaluni. Hakika, tutaipata katika mkutano mwisho wa wiki hii.

Leo tunawaidhinisha wanaume 15 kama manabii, waonaji, na wafunuzi. Mambo yao ya kiroho na uzoefu wao unawapa mtazamo wa kipekee ambao tunauhitaji kwa kiasi kikubwa. Jumbe zao ni rahisi kupata na zinatolewa kwa usahihi thabiti. Wanatuambia kile Mungu anachotaka tujue, bila kujali kina umaarufu au la.19

Kutafuta sauti yake katika moja ya maeneo haya ni vizuri, lakini kuitafuta katika mengi ya maeneo hayo ni vizuri zaidi. Na pale tunapoisikia, tunahitaji kufuata mwelekeo ambao unatolewa. Mtume Yakobo alisema, “Kuweni watendaji wa neno na si wasikiaji tu.”20 Na Rais Thomas S. Monson wakati mmoja alifundisha: “Tunatazama. Tunasubiri. Tunasikiliza ile sauti ndogo, tulivu. Wakati inapozungumza, wanaume na wanawake wenye busara hutii.”21

Wakati Mwongozo Unapochelewa Kuja

Mapema katika maisha yangu ya kazi ya kuajiriwa, Dada Homer na mimi tuliombwa kukubali badiliko katika kazi. Wakati huo, ilionekana kwetu ni uamuzi mkubwa. Tulisoma, tulifunga, na tulisali, lakini jibu lilikawia kuja. Hatimaye, tulifanya uamuzi na kusonga mbele. Tulipofanya hivyo, tulihisi kutulia na punde tulijifunza kwamba ilikuwa ni moja ya maamuzi mazuri zaidi tuliyowahi kufanya.

Kama matokeo, tumejifunza kwamba majibu wakati mwingine huja kwa kukawia. Hii inaweza kuwa kwa sababu si muda sahihi, kwa sababu jibu halihitajiki, au kwa sababu Mungu anatuamini sisi kufanya uamuzi peke yetu. Mzee Richard G. Scott wakati mmoja alifundisha kwamba tunapaswa kuwa na shukrani kwa nyakati kama hizo na alitoa ahadi hii: “Wakati unapoishi kwa haki na uchaguzi wako ni endelevu katika mafundisho ya Mwokozi na unahitaji kutenda, endelea kwa kuamini. … Mungu hatakuacha uendelee mbali zaidi bila msukumo wa onyo kama umefanya uamuzi mbaya.”22

Lazima Tuchague

Na hivyo, tunahitaji kuamua ipi, kati ya sauti zote tofauti, tutaitii. Je tutafuata sauti zisizo za kutegemewa zinazotetewa na ulimwengu, au tutafanya kazi inayotakiwa kuruhusu sauti ya Baba yetu kutuongoza katika maamuzi yetu na kutulinda kutokana na hatari? Kadiri tunavyotafuta sauti Yake kwa bidii zaidi, ndivyo inavyokuwa rahisi kusikia. Si kwamba sauti Yake inakuwa kubwa bali kwamba uwezo wetu wa kuisikia umeongezeka. Mwokozi ameahidi kwamba kama “tutasikiliza kanuni [Zake], na kutii mashauri [Yake],” Yeye [atatupatia] zaidi.”23 Ninashuhudia kwamba ahadi hii ni ya kweli—kwa kila mmoja wetu.

Takriban mwaka mmoja uliopita, tulimpoteza kaka yangu kwenye ajali mbaya ya gari. Miaka ya mwanzo ya John ilikuwa imejaa ahadi na mafanikio. Lakini alipozidi kukua, mwili uliovunjika na akili isiyo na ushirikiano vilifanya maisha kuwa magumu sana. Wakati uponyaji alioutumainia haukuja katika maisha haya, John hata hivyo alishikilia imani yake, akidhamiria kuvumilia, vizuri kadiri ambavyo angeweza, mpaka mwisho.

Ninajua John hakuwa mkamilifu, lakini nimejiuliza kilikuwa nini hasa kilichompa uvumilivu kama huo. Sauti nyingi zilimwalika kwenye ubeuzi usio muhimu sana, lakini alichagua kutokwenda. Badala yake, alifanya kila aliloweza kukita maisha yake kwenye kiini cha injili. Aliishi maisha yake pale, kwa sababu alijua angepata sauti ya Bwana wake pale; aliishi maisha yake pale, kwa sababu alijua ilikuwa pale ambapo angeweza kufunzwa.

Hitimisho

Akina kaka na akina dada, katika ulimwengu wenye sauti nyingi zinazoshindana, ninashuhudia kwamba Baba yetu wa Mbinguni amefanya iwezekane kwetu kusikia na kuifuata Yake. Tukiwa wenye bidii, Yeye na Mwana Wake watatupatia mwongozo tunaotafuta, nguvu tunayohitaji, na furaha sote tunayotamani. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha