2010–2019
Upendo Mkuu kwa Watoto wa Baba Yetu
Mkutano Mkuu wa Aprili 2019


Upendo Mkuu kwa Watoto wa Baba Yetu

Upendo ni sifa ya msingi na motisha kwa malengo ya kiroho tuliyopewa jukumu kuchukua na nabii wetu mpendwa.

Wapendwa kaka zangu na dada zangu, huu ni muda wa kipekee na wa muhimu sana katika historia. Tumebarikiwa kuishi katika kipindi cha mwisho cha maongozi ya Mungu kabla ya Ujio wa Pili wa Mwokozi. Karibia na mwanzo wa kipindi hiki cha maongozi ya Mungu mnamo 1829, mwaka mmoja kabla ya Kanisa kuanzishwa, ufunuo wa kupendeza ulipokelewa, ukitangaza kwamba “kazi ya ajabu” ilikuwa “karibu kuja.” Ufunuo huu uliimarisha kwamba wale wenye tamaa ya kumtumikia Mungu wanastahili kwa huduma hiyo kupitia “imani, tumaini, hisani na upendo, na jicho likiwa kwenye utukufu wa Mungu pekee.”1 Hisani, ambayo ni “upendo msafi wa Kristo,”2 hujumuisha upendo wa milele wa Mungu kwa watoto Wake wote.3

Lengo langu asubuhi hii ni kusisitiza jukumu muhimu la aina hiyo ya upendo katika kazi ya umisionari, kazi ya hekaluni na historia ya familia, na kushika dini kifamilia kunakolenga nyumbani, kunakosaidiwa na Kanisa. Upendo kwa Mwokozi na upendo kwa wenzetu4 ni sifa ya msingi na motisha ya kuhudumu na malengo ya kiroho5 tuliyopewa jukumu kuchukua na nabii wetu mpendwa, Rais Russell M. Nelson, katika marekebisho yaliyotangazwa mnamo 2018.

Juhudi za Umisionari za Kukusanya Israeli Iliyotawanyika

Nilitambulishwa kwenye uhusiano kati ya kazi ya umisionari na upendo mapema katika maisha yangu. Nilipokuwa na miaka 11, nilipokea baraka ya baba mkuu kutoka kwa patriaki ambaye alikuwa babu yangu.6 Baraka hiyo kwa sehemu ilisema, “ninakubariki kwa upendo mkubwa kwa wanadamu wenzako, kwani utaitwa kuipeleka injili ulimwenguni … kuleta nafsi kwa Kristo.”7

Nilielewa hata katika umri ule mdogo kwamba kushiriki injili kulijengeka juu ya upendo mkubwa kwa watoto wote wa Baba yetu wa Mbinguni.

Viongozi Wakuu wenye Mamlaka walipopangiwa kufanyia kazi Hubiri Injili Yangu miaka 15 iliyopita, tulihitimisha kwamba sifa ya upendo ilikuwa muhimu kwenye kazi ya umisionari katika siku yetu, kama vile ambavyo daima imekuwa. Sura ya 6, kwenye sifa kama za Kristo, ikijumuisha hisani na upendo, imekuwa mara zote sura maarufu zaidi kwa wamisionari.

Kama wajumbe wa Mwokozi, wamisionari wengi huhisi aina hii ya upendo, na pale wanapohisi, juhudi zao hubarikiwa. Pale waumini wanapopata ono la aina hii ya upendo, ambao ni muhimu katika kumsaidia Bwana kwenye lengo Lake, kazi ya Bwana itafanikishwa.

Picha
R. Wayne Shute

Nilipata bahati ya kuwa na jukumu dogo katika mfano wa ajabu wa aina hii ya upendo. Wakati nilipokuwa nikitumikia kama Rais wa Eneo la visiwa vya Pacific, nilipokea simu kutoka kwa Rais R. Wayne Shute. Akiwa kijana mdogo alitumikia misheni yake kule Samoa. Baadaye, alirudi Samoa kama rais wa misheni.8 Aliponipigia simu, alikuwa rais wa Hekalu la Apia Samoa. Mmoja wa wamisionari wake vijana, wakati alipokuwa rais wa misheni, alikuwa Mzee O. Vincent Haleck, ambaye sasa ni Rais wa Eneo katika Pacific. Rais Shute alikuwa na upendo mkubwa na heshima kwa Vince na familia yote ya Haleck. Wengi wa wanafamilia walikuwa waumini wa Kanisa, lakini baba wa Vince, Otto Haleck, baba mkuu wa familia (wa ukoo wa Kijerumani na Samoa) hakuwa muumini. Rais Shute alijua nilikuwa nikihudhuria mkutano wa kigingi na mikutano mingine huko Samoa ya Amerika, na aliniuliza kama ningefikiria kukaa kwenye nyumba ya Otto Haleck kwa lengo la kushiriki injili pamoja naye.

Picha
Mzee O. Vincent Haleck kama mmisionari kijana

Mke wangu, Mary, pamoja nami tulikaa na Otto na mke wake, Dorothy, katika nyumba yao nzuri. Wakati wa kifungua kinywa nilishiriki ujumbe wa injili na kumualika Otto kukutana na wamisionari. Alikuwa mkarimu, lakini imara, katika kukataa mwaliko wangu. Alisema alifurahishwa kwamba wanafamilia wengi wa familia yake walikuwa Watakatifu wa Siku za Mwisho. Lakini kwa kulazimisha alionyesha kwamba baadhi ya mababu zake wa Kisamoa upande wa mama walikuwa wachungaji wa mwanzo wa Kikristo wa Samoa, na alihisi wajibu mkubwa kwa utamaduni wao wa imani ya Kikristo.9 Hata hivyo, tuliondoka kama marafiki wazuri.

Baadaye, wakati Rais Gordon B. Hinckley alipokuwa akijiandaa kuweka wakfu Hekalu la Suva Fiji, alimtaka katibu muhtasi wake, Kaka Don H. Staheli,10 anipigie simu huko New Zealand kufanya matayarisho. Rais Hinckley alitaka kusafiri kutoka Fiji kwenda Samoa ya Amerika kukutana na Watakatifu. Hoteli moja iliyotumika katika ziara ya nyuma ilipendekezwa. Niliuliza kama ningeweza kufanya mabadiliko. Kaka Staheli alisema, “Wewe ni Rais wa Eneo; hilo halina shida.”

Mara moja nilimpigia Rais Shute na kumwambia kwamba pengine tuna nafasi ya pili kwenye kumbariki kiroho rafiki yetu Otto Haleck. Wakati huu mmisionari angekuwa Rais Gordon B. Hinckley. Niliuliza kama alidhani ingekuwa sawa kwa Haleck kuwa mwenyeji wa kundi lote la safari la Rais Hinckley.11 Rais na Dada Hinckley, binti yao Jane, na Mzee na Dada Jeffrey R. Holland walikuwa pia sehemu ya kundi la safari. Rais Shute, akifanya kazi pamoja na familia, walifanya matayarisho yote.12

Tulipowasili kutoka Fiji baada ya kuweka wakfu hekalu, tulikaribishwa vizuri.13 Tulizungumza jioni ile na maelfu ya waumini wa Samoa na kisha kuelekea kwenye ua wa familia ya Haleck. Tulipokusanyika kwa ajili ya kifungua kinywa asubuhi iliyofuata, Rais Hinckley na Otto Haleck walikuwa tayari marafiki wazuri. Ilikuwa ya kupendeza kwangu kwamba walikuwa na mazungumzo mengi yaliyokuwa sawa na yale niliyofanya na Otto mwaka mmoja kabla. Wakati Otto alipoelezea kuvutiwa kwake na kanisa letu lakini kuhakikisha tena kujitolea kwake kwenye Kanisa lake la sasa, Rais Hinckley aliweka mkono wake kwenye bega la Otto na kusema, “Otto, hiyo si nzuri vya kutosha; unapaswa kuwa muumini wa Kanisa. Hili ni Kanisa la Bwana.” Ungeweza kistiari kuona ngao ya upinzani ikidondoka kutoka kwa Otto kwa uwazi kwenye kile Rais Hinckley alichosema.

Huu ulikuwa mwanzo wa mafundisho ya ziada ya umisionari na unyenyekevu wa kiroho ambao ulimruhusu Otto Haleck kubatizwa na kuthibitishwa zaidi kidogo ya mwaka baadaye. Mwaka mmoja baada ya hilo, familia ya Haleck iliunganishwa kama familia ya milele hekaluni.14

Picha
Familia ya Haleck imeunganishwa hekaluni

Kile kilichogusa moyo wangu kote katika uzoefu huu wa kupendeza ilikuwa ni upendo tele wa huduma uliooneshwa na Rais Wayne Shute kwa mmisionari wake wa zamani, Mzee Vince Haleck, na hamu yake ya kuona familia yote ya Haleck inaungana kama familia ya milele.15

Linapokuja suala ka kuikusanya Israeli, tunahitaji kufunganisha mioyo yetu na aina hii ya upendo na kusonga mbali na hisia za jukumu tu16 au hatia kwenye hisia za upendo na kushiriki katika wenza mtakatifu wa kushiriki ujumbe, huduma na misheni ya Mwokozi pamoja na ulimwengu.17

Kama waumini tunaweza kuonyesha upendo wetu kwa Mwokozi na akina kaka na dada zetu kote ulimwenguni kwa kufanya mialiko rahisi. Ratiba mpya ya mkutano wa Jumapili inawakilisha fursa ya kipekee kwa waumini kwa mafanikio na kwa upendo kualika marafiki na wenza kuja na kuona na kuhisi uzoefu wa Kanisa.18 Mkutano wa kiroho wa sakramenti, kwa matumaini ulio mtakatifu jinsi Mzee Jeffrey R. Holland alivyoelezea jana, utafuatiwa na mkutano wa dakika-50 uliofokasi kwenye Agano Jipya na Mwokozi au hotuba husika za mkutano pia zikiwa zimefokasi kwa Mwokozi na mafundisho Yake.

Baadhi ya akina dada wa Muungano wa Usaidizi wa akina mama wamejiuliza kwa nini wamepewa jukumu la “kukusanya” sambamba na washiriki wa akidi ya ukuhani. Kuna sababu kwenye hili, na Rais Nelson ametoa nyingi kwenye mkutano mkuu uliopita. Alihitimisha, “Hatuwezi kiurahisi kukusanya Israeli bila ninyi.”19 Katika siku yetu tumebarikiwa kwamba takriban asilimia 30 ya wamisionari wetu wa muda wote ni akina dada. Hii inatoa hitaji la ziada na kichocheo kwa akina dada wa Muungano wa Usaidizi wa akina mama kwa upendo kushiriki injili. Kinachohitajika ni dhamira ya kiroho ya upendo, ya huruma kwa kila mmoja wetu—wanaume, wanawake, vijana, na watoto— kushiriki injili ya Yesu Kristo. Tukionyesha upendo, ukarimu, na unyenyekevu, wengi watakubali mwaliko wetu. Wale wanaochagua kutokubali mwaliko wetu wataendelea kuwa rafiki zetu.

Juhudi za Hekaluni na Historia ya Familia kwenye Kukusanya Israeli

Upendo pia upo kwenye kiini cha juhudi yetu ya hekaluni na historia ya familia kwenye kukusanya Israeli upande mwingine wa pazia. Tunapojifunza juu ya majaribu na magumu waliyopata mababu zetu, upendo na shukrani zetu kwao vinaongezeka. Juhudi yetu ya hekaluni na historia ya familia imeimarishwa kwa kiwango muhimu kwa mabadiliko mapya kote kwenye ratiba ya mkutano wa Jumapili na kupanda kwa vijana katika madarasa na akidi. Mabadiliko haya yanatoa umakini wa mapema na wenye nguvu kwenye kujifunza kuhusu mababu zetu na kukusanya Israeli upande mwingine wa pazia. Vyote kazi ya hekaluni na historia ya familia vimeongezeka.

Intanenti ni nyenzo yenye nguvu; nyumbani sasa ni kituo chetu cha msingi cha historia ya familia. Waumini wetu vijana wanafunzwa kipekee katika utafiti wa historia ya familia na wamehamasika kiroho kufanya ubatizo kwa niaba ya mababu zao, ambao wamejifunza kuwapenda na kuwashukuru. Tangu badiliko la kuruhusu wengi wenye miaka 11 kufanya ubatizo kwa ajili ya wafu, marais wa mahekalu kote ulimwenguni wanaripoti ongezeko kuu la uhudhuriaji. Rais mmoja wa hekalu anatutaarifu kwamba “kumekuwa na ongezeko kubwa kwenye walezi wa ubatizo … na ongezeko la wenye miaka 11 kuleta familia zaidi. … Hata katika umri wao [mdogo], wanaonekana kuhisi heshima kuu na lengo la ibada wanayofanya. Ni nzuri kutazama!”20

Ninajua viongozi wetu wa msingi na wa vijana wanafanya na wataendelea kufanya historia ya familia na kazi ya hekaluni kuwa juhudi kuu. Akina dada wa Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama na akina kaka wa ukuhani wanaweza kwa upendo kutimiza jukumu lao la hekaluni na historia ya familia kibinafsi na pia kwa kuwasaidia na kuwatia msukumo watoto na vijana kukusanya Israeli upande mwingine wa pazia. Hili ni muhimu hasa nyumbani na katika siku ya Sabato. Ninaahidi kwamba kwa kufanya ibada kwa upendo kwa ajili ya mababu kutawaimarisha na kuwalinda vijana na familia zetu katika ulimwengu ambao unazidi kuwa mwovu. Pia binafsi ninashuhudia kwamba Rais Russell M. Nelson amepokea ufunuo muhimu sana kuhusiana na mahekalu na kazi ya hekaluni.

Tayarisha Familia za Milele na Watu Binafsi Kuishi na Mungu

Msisitizo mpya wa kujifunza na kuishi injili unaolenga nyumbani na nyenzo zinazotolewa na Kanisa ni fursa kuu ya kwa upendo kutayarisha familia za milele na watu binafsi kukutana na kuishi na Mungu.21

Wakati mwanaume na mwanamke wanaunganishwa hekaluni, wanaingia kwenye utaratibu mtakatifu wa ndoa kwenye agano jipya na lisilo na mwisho, utaratibu wa ukuhani.22 Kwa pamoja wanapata na kupokea baraka za ukuhani na nguvu za kuongoza mambo ya familia yao. Wanawake na wanaume wana majukumu ya kipekee kama ilivyoonyeshwa katika “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,”23 lakini usimamizi wao ni sawa katika thamani na umuhimu.24 Wana nguvu sawa ya kupokea ufunuo kwa ajili ya familia yao. Wanapofanya kazi pamoja kwa upendo na haki, maamuzi yao yanabarikiwa mbinguni.

Wale wanaotafuta kujua mapenzi ya Bwana kama watu binafsi na kwa ajili ya familia zao lazima wajitahidi kutafuta haki, upole, ukarimu, na upendo. Unyenyekevu na upendo ni sifa bainifu ya wale wanaotafuta mapenzi ya Bwana, hasa kwa familia zao.

Kujikamilisha, kujistahilisha kwa baraka za maagano, na kujitayarisha kukutana na Mungu ni jukumu la mtu binafsi. Tunapaswa kujitegemea na kujihusisha kwa shauku katika kufanya nyumba zetu kimbilio kutoka kwenye dhoruba zinazotuzunguka25 na “madhabahu ya imani.”26 Wazazi wana jukumu la kuwafunza watoto wao kwa upendo. Nyumba zilizojaa upendo kiuhalisia ni mbingu duniani zenye shangwe, za kupendeza.27

Wimbo alioupenda mama yangu ulikuwa “Upendo nyumbani.”28 Kila mara aliposikia ubeti wa kwanza, “Urembo ni nyumbani kwenye upendo,” aliguswa waziwazi na kulia. Kama watoto tulijua kwamba tuliishi katika aina ile ya nyumba; ilikuwa ni moja ya vipaumbele vyake vya juu.29

Kuongezea kwenye mazingira ya upendo nyumbani, Rais Nelson amefokasi kwenye kuzuia matumizi ya vyombo vya habari ambayo yanaingilia kati lengo letu la msingi.30 Moja ya badiliko ambalo litanufaisha karibia familia yoyote ni kufanya intaneti, mitandao ya kijamii, na televisheni mtumishi badala ya kitu kinachotuvuruga au, mbaya zaidi, bwana. Vita kwa nafsi za wote, lakini hasa watoto, mara nyingi iko nyumbani. Kama wazazi tunahitaji kuhakikisha kwamba maudhui ya vyombo vya habari ni yenye kuleta siha, sahihi kwa umri, na yenye muendelezo wa mazingira ya upendo tunayojaribu kujenga.

Mafundisho katika nyumba zetu yanahitaji kuwa wazi na yenye kuvutia31 lakini pia ya kiroho, shangwe, na yaliyojaa upendo.

Ninaahidi kwamba tunapofokasi kwenye upendo wetu kwa Mwokozi na Upatanisho Wake, tukimfanya Yeye kiini cha juhudi zetu za kukusanya Israeli pande zote za pazia, kuhudumia wengine, na kibinafsi kujitayarisha kukutana na Mungu, ushawishi wa mjaribu utafifishwa na shangwe, furaha, na amani ya injili itakuza nyumba zetu kwa upendo kama wa Kristo.32 Ninashuhudia juu ya ahadi hizi za maandiko na kutoa ushahidi wa hakika wa Yesu Kristo na dhabihu Yake ya upatanisho kwa niaba yetu, katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Mafundisho na Maagano 4:1, 5.

  2. Moroni 7:47.

  3. Ona “Hisani na Upendo,” Hubiri Injili Yangu:Mwongozo kwa ajili ya Huduma ya Kimisionari , rev. Ed. (2019), 124.

  4. Ona Kumbukumbu la Torati 6:5; Mathayo 22:36–40.

  5. Ona “Majukumu ya Urais wa Akidi ya Wazee na Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama katika Umisionari wa Muumini na Kazi ya Hekaluni na Historia ya Familia,” taarifa, Okt. 6, 2018.

  6. Babu yangu alipewa mamlaka ya kutoa baraka ya baba mkuu kwa wajukuu walioishi katika vigingi tofauti. Nilipewa katika umri wa miaka 11 kwa sababu alikuwa mgonjwa na ilikuwa kama angefariki.

  7. Baraka ya baba mkuu aliyopewa Quentin L. Cook, kutoka kwa Patriaki Crozier Kimball, Okt. 13, 1951, Draper, Utah.

  8. Rais R. Wayne Shute pia alitumikia na mke wake Lorna kwenye aina nyingine tofauti ya misheni huko Shanghai, China; Armenia; Singapore; na Ugiriki. Baada ya Lorna kufariki, alimuoa Rhea Mae Rosvall, na walitumikia Misheni ya Brisbane Australia. Saba kati ya watoto wake tisa wametumikia umisionari wa muda wote. Kipindi cha miaka miwili alipokuwa akitumikia kama rais wa misheni huko Samoa, Mzee John H. Groberg alikuwa akitumikia kama rais wa misheni huko Tonga. Uzoefu waliopata wote wawili ni wa hadithi za kale.

  9. Otto Haleck alikuwa kiongozi wa kawaida kwenye Kanisa la Mkusanyiko wa Kikristo la Samoa, ambalo lilikuwa na mizizi iliyochipuka kutoka Shirika la Umisionari la London. Baba yake alikuwa wa urithi wa Ujerumani kutoka Dessau, Ujerumani.

  10. Rais Don H. Staheli kwa sasa anatumikia kama rais wa Hekalu la Bountiful Utah.

  11. Rais na Dada Hinckley na binti yao Jane Hinckley Dudley, Mzee Jeffrey R. Na Dada Patricia T. Holland, Mzee Quentin L. Na Dada Mary G. Cook, na Kaka Don H. Staheli wote walikuwepo.

  12. Mzee O. Vincent Haleck ananitaarifu kwamba baba yake alimualika Vince na kaka yake David kurudi kutoka ughaibuni ili kukagua nyumba na kuwepo kwa ajili ya ziara ya Rais Hincley. Mzee Haleck alisema baba yake alitangaza, “Hawa wangeweza kuwa malaika mjue.” Aliwaambia wana wake kama walikuwa wanataka kuwa wenyeji wa nabii, wangetaka nyumba iwe bila kasoro.

  13. Rais Hincley alikaribishwa na uongozi wa taifa la Samoa ya Amerika na maelfu ya Wasamoa kwenye uwanja wa mpira wa miguu.

  14. Kuunganisha familia kupitia kazi ya bidii ya umisionari imekuwa sifa kuu ya wote Wasamoa na Wapolinisiani.

  15. Rais Shute alipendwa sana na kukubaliwa kiasi kwamba alialikwa kuzungumza kwenye ibada ya mazishi ya Otto Haleck mnamo 2006.

  16. “Wakati mwingine tunaweza hatimaye kutumikia kutokana na hisia ya wajibu au jukumu, lakini hata huduma hiyo inaweza kutuongoza kwenye kusogelea jambo kubwa … kutumikia katika ‘njia bora zaidi’ [1 Wakorintho 12:31].” (Joy D. Jones, “Kwa ajili Yake,” Liahona, Nov. 2018, 50).

  17. Ona Tad R. Callister, Upatanisho Usio na Mwisho (2000), 5–8.

  18. Waumini wa Kanisa wanapaswa kushirikiana na wamisionari wakati wowote wanapofanya mialiko.

  19. Russell M. Nelson, “Ushiriki wa Akina Dada katika Kukusanya Israeli,” Liahona, Nov. 2018, 70.

  20. Rais B. Jackson na Dada Rosemary M. Wixom, rais na matroni wa Hekalu la Salt Lake, ripoti kwa Urais Mkuu wa Msingi, Mar. 2019. Waligundua kwamba “wanaagiza zaidi saizi ndogo kabisa ya nguo za ubatizo ili kukidhi mahitaji!”

  21. Ona Russell M. Nelson, “Maneno ya Ufunguzi,” Liahona, Nov. 2018, 6–8.

  22. Ona Mafundisho na Maagano 131:1–4.

  23. Ona “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” Liahona, Mei. 2017, 145.

  24. “Kila baba kwa familia yake ni baba mkuu na mama ni mama mkuu kama wenza sawa katika majukumu yao ya kipekee ya wazazi” (James E. Faust, “Sauti ya Kinabii,” Ensign, May 1996, 6).

  25. Ona Mafundisho na Maagano 45:26–27; 88:91.

  26. Ona Russell M. Nelson, “Kuwa Mtakatifu wa Siku za Mwisho wa Mfano,” Liahona, Nov. 2018, 113.

  27. Ona “Home Can Be a Heaven on Earth,” Nyimbo za Kanisa, na. 298.

  28. “Love at Home,” Nyimbo za Kanisa, na. 294.

  29. Kama aina hii ya upendo inapaswa kufikiwa, maelekezo katika Mafundisho na Maagano 121:41–42 yanapaswa kuwa lengo:

    “Hakuna nguvu au uwezo unaoweza au upaswao kudumishwa kwa njia ya ukuhani, isipokuwa tu kwa njia ya ushawishi, kwa uvumilivu, kwa upole na unyenyekevu, na kwa upendo usio unafiki;

    “Kwa wema, na maarifa safi, ambayo yataikuza sana nafsi isiyo na unafiki, na isiyo na hila.”

    Ukosoaji uliovuka mipaka kwa watoto unapaswa kuepukwa. Kushinda makosa na kukosa hekima kunahitaji maelekezo, siyo ukosoaji. Dhambi inahitaji kukemewa (Ona Mafundisho na Maagano 1:25–27).

  30. Ona Russell M. Nelson, “Ushiriki wa Akina Dada katika Kukusanya Israeli,” 69; ona pia Russell M. Nelson, “Tumaini la Israeli” (ibada ya vijana ulimwenguni kote, Juni 3, 2018), TmainilaIsraeli.

  31. Kwa hisia, kufundisha nyumbani ni kama shule ya darasa moja kwa watoto wa umri wote. Tunapomfundisha mwenye miaka 11, hatuwezi kumpuuzia mwenye miaka 3.

  32. Ona Yohana 17: 3; 2 Nefi 31:20; Moroni 7:47.

Chapisha