2023
Baba wa Kupendeza wa Magnolia
Julai 2023


“Baba wa Kupendeza wa Magnolia,” Rafiki, July 2023, 40–41.

Baba wa Kupendeza wa Magnolia

“Baadhi ya watoto walisema sisi siyo familia kwa sababu Baba si muumini wa kanisa letu.”

Hadithi hii ilitokea huko Marekani.

Picha
Familia ikisoma kutoka kwenye Biblia

“Magnolia! Lily!” Baba aliita. “Muda wa maandiko na sala!”

Magnolia aliketi sakafuni pembeni ya mbwa wao, Raindrop. Lily aliingia ndani ya blanketi lake pendwa.

Muda wa familia wa maandiko ulikuwa wa kuleta burudani. Wakati fulani waliigiza hadithi za maandiko pamoja. Ilimsaidia Magnolia kupata taswira za hadithi. Pia, Raindrop daima alisaidia wakati kulipokuwa na wanyama kwenye hadithi!

Baba alifungua maandiko yake na kusoma mstari. Kisha alimpa Magnolia Biblia kubwa, nzito. Kila mmoja alifanya zamu kusoma.

“Iweni wafadhili ninyi kwa ninyi,” Magnolia alisoma.*

Alikunja uso. Watu hawakuwa mara zote wakarimu kwake kanisani.

“Mama, Baba, naweza kuzungumza nanyi kuhusu jambo fulani?” aliuliza.

“Bila shaka,” Mama alisema. “Ni jambo gani hilo?”

“Jana katika Msingi, baadhi ya watoto waliniambia sisi siyo familia nzuri kwa sababu Baba si muumini wa kanisa letu.”

Baba wa Magnolia alikuwa wa kanisa tofauti. Alikwenda kwenye mkutano wa sakramenti pamoja na familia yao siku za Jumapili. Alitoa mahubiri kuhusu Roho Mtakatifu kwenye ubatizo wa Lily na Magnolia. Kila mmoja alisema alifanya vizuri sana. Alikuwa baba wa mwema.

“Kile walichokisema kilinifanya nitake kulia.” Magnolia alivuta kamasi. “Kwa nini watu wanakuwa wakatili kiasi hiki?”

Mama na Baba waliangaliana.

“Nafurahi umetuambia kilichotokea,” Baba alisema. “Mimi na mama tunapendana sana. Na familia yetu ni muhimu sana kwetu.”

Mama alikubali kwa kichwa. “Na familia yetu ni muhimu pia kwa Baba wa Mbinguni. Yeye anawapenda watoto Wake wote.”

Raindrop alisonga karibu na Magnolia. Alikwaruza masikio yake.

“Baba wa Mbinguni anatujua na anajua tunapendana,” Baba alisema. “Hakuna familia iliyo kamilifu, lakini tunaweza kujaribu kadiri tunavyoweza.”

“Lakini bado inauma wakati watu wanaposema mambo ya ukatili kuhusu familia yetu,” Magnolia alisema. Yesu alitufundisha kuwa wakarimu kwa kila mmoja. Kusema maneno ya ukatili haionekani kama kumfuata Yesu.”

“Uko sahihi,” alisema Baba. “Pengine wakati unapohisi kusema jambo la kikatili, unaweza kukumbuka vile ulivyohisi wakati wengine walipokuwa wakatili kwako. Kisha unaweza kusema jambo lenye ukarimu kama mbadala.”

Magnolia alivuta pumzi ndefu. “SAWA.” Alifurahi kwamba aliweza kuzungumza na Mama na Baba.

“Muda wa kumbatio la familia!” Baba aliwavuta Lily na Magnolia kwenye kumbatio kubwa na akawabana pamoja kwa nguvu. Mama alikunja mikono yake kuwazunguka wote watatu. Raindrop alikimbia katika duara kumzunguka kila mtu.

Picha
Familia ikiwa katika kumbatio la familia

“Siwezi kupumua!” alitania Lily. Magnolia alicheka.

“Sasa nikumbusheni—ni zamu ya nani kufundisha?” Baba aliuliza. Aliwaachia wasichana na kuchukua maandiko yake.

“Zamu yangu!” alisema Lily. “Na ni zamu ya baba kutoa sala.”

Walipomaliza kusoma, kila mmoja alipiga magoti kusali. Magnolia alihisi amani pale alipomsikiliza Baba akitoa sala. Alijua Baba wa Mbinguni aliipenda familia yake.

Picha
Alt text

Vielelezo na Constanza Basaluzzo

Chapisha