Mkutano Mkuu
Uwezo wa Neno
mkutano mkuu wa Oktoba 2022


Uwezo wa Neno

Kuna uwezo katika maneno ya manabii wa kale na wa leo kwa usahihi kwa sababu maneno yao ni maneno ya Bwana.

Katika Kitabu cha Mormoni, tunasoma juu ya uamuzi muhimu uliofanywa na nabii Alma katika mstari pendwa wa maandiko. Kabla ya kupitia maneno hayo yanayofahamika, tafadhali zingatia pamoja nami hali ngumu ambazo kwazo uamuzi huo ulifanywa.

Kundi dogo la watu, wakijiita Wazoramu, walikuwa wamejitenga kutoka kwa Wanefi1 na kukusanyika kwenye mipaka ya nchi karibu na Walamani.2 Wanefi walikuwa punde tu wamewashinda Walamani kwenye vita kuu ambayo makumi elfu walikuwa wameuwawa,3 na ilikuwa ya “kutia hofu sana kwamba Wazoramu wangeingia kwenye makubaliano na Walamani na kwamba ingekuwa chanzo cha upotevu mkubwa.”4 Zaidi ya wasiwasi wa vita, Alma alikuwa amepata habari kwamba Wazoramu, ambao “walikuwa wamehubiriwa neno la Mungu,”5 walikuwa wakigeukia kuabudu miungu na “kupotosha neno la Bwana.”6 Yote haya yalimzidia Alma na yalikuwa “chanzo cha huzuni kuu.”7

Akijikuta katika hali hizi ngumu na zenye changamoto, Alma alitafakari nini kifanyike. Kwenye uamuzi wake, tunasoma maneno ambayo yalihifadhiwa ili kutupatia msukumo na kutuelekeza pale tunapopitia hali ngumu na zenye changamoto za siku yetu.8

“Na sasa, kwa vile kuhubiri kwa neno kulikuwa na maelekezo makubwa ya kuongoza watu kufanya yale ambayo ni haki—ndiyo, ilikuwa na matokeo ya nguvu zaidi kwa akili za watu kuliko upanga, au kitu chochote kingine, ambacho kiliwahi kufanyika kwao—kwa hivyo Alma alifikiri ilikuwa bora kwamba wangejaribu matokeo ya uwezo wa neno la Mungu.”9

Kati ya masuluhisho mengi yanayowezekana, imani ya Alma iliwasukuma kutegemea uwezo wa neno la Mungu. Si kwa bahati kwamba baadhi ya mahubiri yenye nguvu sana yanayopatikana kwenye maandiko yalihubiriwa punde tu kufuatia uamuzi huo. Katika sura za 32 na 33 za Alma, tunasoma mahubiri yake yenye ustadi juu ya imani katika Bwana Yesu Kristo na kwenye sura ya 34 tunapata mafundisho ya semina ya Amuleki juu ya Upatanisho wa Yesu Kristo.

Vielelezo vya Uwezo wa Neno

Hakika, kote katika maandiko tunasoma juu ya baraka za kimiujiza zilizomiminwa juu ya wale waliochagua kujaribu uwezo wa neno la Mungu kwenye maisha yao.10 Ninawaalika mtafakari pamoja nami mifano mitatu wakati tunapoelekeza fokasi yetu kwenye Kitabu cha Mormoni—kitabu ambacho Rais Russell M. Nelson alikielezea kama “mwongozo wetu kwa ajili ya kunusurika siku za mwisho.”11

Kwanza, akiwakumbusha watu wake jinsi Bwana alivyowakomboa baba zao, Alma alifundisha: “Tazama, aliibadilisha mioyo yao; ndio, aliwaamsha kutoka katika usingizi mzito na wakaamka katika Mungu. Tazama, walikuwa katikati ya giza; walakini, nafsi zao ziliangazwa na nuru ya neno lisilo na mwisho.”12 Pengine unahisi kana kwamba ulikuwa katikati ya giza. Je, nafsi yako inatamani kuangazwa? Kama ndivyo, jaribu uwezo wa neno la Mungu.

Pili, akitafakari uongofu wa Walamani kwa Bwana, ambao aliushuhudia kama mmisionari, Amoni alisema, “Tazama, ni maelfu mangapi ya ndugu zetu ambao amewaachilia kutoka kwa uchungu wa jehanamu; na wamefanywa kuimba upendo ukomboao, na haya kwa sababu ya uwezo wa neno lake ambao uko ndani yetu.13 Akina kaka na akina dada, kuna wengi kati yetu ambao wanatamani mtu tunayempenda aletwe kwenye kuimba upendo ukomboao. Katika juhudi zetu zote, acha tukumbuke kujaribu uwezo wa neno la Mungu, ulio ndani yetu.

Tatu, kwenye Kitabu cha Helamani tunasoma, “Ndiyo, tunaona kwamba yeyote atakaye angelishikilia neno la Mungu, ambalo ni jepesi na lenye nguvu, ambalo litaangamiza ujanja wote na mitego na hila za ibilisi, na kumwongoza mwanamume [na mwanamke] wa Kristo katika njia iliyosonga na nyembamba mpaka ngʼambo ya shimo la dhiki lisilo na mwisho …na kuangusha roho zao … katika mkono wa kuume wa Mungu katika ufalme wa mbinguni.”14 Je, unatafuta kuangamiza ujanja wote na mitego na hila za ibilisi ambazo zimeenea katika falsafa za siku yetu? Je, unatamani kutawanya mawingu ya mkanganyiko yaliyosababishwa na wingi wa taarifa ili ufokasi zaidi kwa upekee kwenye njia ya agano? Tafadhali jaribu uwezo wa neno la Mungu.

Kama mtu ambaye nimebadilishwa kwa nguvu ya neno, binafsi ninashuhudia juu ya ukweli huu wa kupendeza uliofundishwa na nabii wetu mpendwa, Rais Russell M. Nelson: “Kwangu mimi, nguvu ya Kitabu cha Mormoni ni dhahiri kabisa kwenye badiliko kuu ambalo huja kwenye maisha ya wale wote wanaokisoma ‘kwa moyo wa kweli na kusudi halisi, wakiwa na imani katika Kristo.’ Waongofu wengi huacha vingi ambavyo mwanzo walivipenda sana ili kuishi kwa maneno ya kitabu hicho. … Kitakuwa chombo chako cha kufaa katika kuleta nafsi kwa Yesu Kristo.”15

Chanzo cha Uwezo

Kwenye vielelezo hivi na vinginevyo, tunashuhudia uwezo wa neno la Mungu katika maisha ya watoto Wake. Tunaweza kuuliza, ni nini chanzo cha uwezo au nguvu hiyo?

Tunapozingatia swali hili, ni muhimu kukumbuka kwamba kirai “neno,” kama kilivyotumika kwenye maandiko, kina angalau maana mbili. Mzee David A. Bednar hivi karibuni alifundisha kwamba “moja ya majina ya Yesu Kristo ni Neno’” na kwamba “mafundisho ya Mwokozi, kama yalivyorekodiwa kwenye maandiko matakatifu, nayo pia ni ‘neno.’”16

Nabii Nefi alielezea uhusiano kati ya maana hizi mbili wakati alipoandika: “Sikilizeni maneno haya na mwamini katika Kristo; na kama hamwamini katika maneno haya aminini katika Kristo. Na kama mtamwamini Kristo mtaamini katika maneno haya, kwani ni maneno ya Kristo, na ameyatoa kwangu.”17 Hivyo tunajifunza kwamba kuna uwezo katika maneno ya manabii wa kale na wa leo kwa usahihi kwa sababu maneno yao ni maneno ya Bwana.18 Rafiki zangu wapendwa, kuukubali ukweli huu wa milele ni muhimu kwenye kunusurika kwetu kiroho katika siku za mwisho19 ambapo, kama ilivyotabiriwa, kuna “njaa katika nchi, si njaa ya kukosa chakula, wala kiu ya kukosa maji, bali ya kusikia maneno ya Bwana.”20

Hatimaye, uwezo wa neno la Mungu ni Bwana Yesu Kristo.21 Tunapotafakari hili kwa ukamilifu, tunaweza kufanya muunganiko muhimu wa milele kati ya jukumu la manabii Wake na Mkombozi Mwenyewe. Upendo wetu Kwake, hamu yetu ya kusogea karibu Naye na kukaa katika pendo Lake,22 utatusukuma kujaribu uwezo wa neno katika maisha yetu—uwezo unaotiririka kutoka Kwake kama Mwokozi wetu binafsi na Mkombozi23 na uwezo unaotiririka kutoka Kwake kupitia maneno ya “vyombo viteule vya Bwana.”24 Tutakuja kufahamu kwamba, kama vile vyanzo vingine vilivyo na msaada katika kujifunza kwetu juu ya Mwokozi na maneno ya manabii Wake, havipaswi kamwe kuwa mbadala wa vyombo viteule. Lazima tunywe kwa wingi na mara nyingi,25 moja kwa moja kutoka kwenye chanzo.26

Ninatoa upendo wangu kwa kila mmoja wenu, kaka na dada zangu. Katika upendo huo, ninawasihi mpate uzoefu wa uwezo wa neno la Mungu, hasa kupitia Kitabu cha Mormoni, kila siku ya maisha yenu. Unapofanya hivyo, utapata uzoefu wa ahadi hii ya kinabii kutoka kwa Rais Russell M. Nelson: “Ninaahidi kwamba unapojifunza kwa sala Kitabu cha Mormoni kila siku, utafanya maamuzi mazuri—kila siku. Ninaahidi kwamba unapotafakari kile unachojifunza, madirisha ya mbinguni yatafunguka, na utapata majibu ya maswali yako na mwongozo wa maisha yako mwenyewe. Ninaahidi kwamba unapozama kila siku kwenye Kitabu cha Mormoni, unaweza kukingwa dhidi ya maovu ya siku.”27

Ninashuhudia kwamba Baba yetu wa Mbinguni ametupatia neno kwa sababu anatupenda kwa ukamilifu na anataka kila mmoja wetu arejee nyumbani kuishi Naye milele. Ninashuhudia juu ya “neno … kufanyika mwili,”28 hata Yesu Kristo na juu ya nguvu Yake ya kutuokoa na kutukomboa. Ninajua kwamba uwezo Wake unatiririka kupitia maneno ya manabii Wake, wote waliopita na wa leo.

Ni sala ya moyo wangu kwamba tupate hekima na unyenyekevu wa kung’ang’ania29 neno la Mungu na kubaki kwenye njia ya agano iongozayo kwenye kuinuliwa na uzima wa milele.30 Na daima tupate uzoefu wa badiliko kuu linalopatikana kwa kila mmoja wetu kupitia uwezo wa Neno.31 Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha