Liahona
Jinsi ya Kuwa Mwanafunzi wa Yesu Kristo
Julai 2024


Makala

Jinsi ya Kuwa Mwanafunzi wa Yesu Kristo

Mwaka huu, mpango wa misioni wa Eneo la Kati la Afrika ni “Mimi ni Mwanafunzi wa Yesu Kristo”.

Unaweza kujiuliza ni aina gani ya mwanafunzi unapaswa kuwa. Jibu ni: Yule anayejitahidi kufanya na kushika maagano matakatifu, anayejitegemea, anayependa, anayeshiriki na kualika. Kwa mtazamo wangu, tabia hizi ni viashiria vya kupiga hatua vya mwanafunzi wa Yesu Kristo.

Tunapodhamiria kumfuata Yesu Kristo, tunakuwa wafuasi wake. Lengo letu kisha linakuwa kujiandaa sisi wenyewe kuwa warithi wa Ufalme wa Mungu. Ili kufanya hili, tunapaswa kufuata mfano Wake. Kuna nyenzo nyingi zilizopo zinazotusaidia tujifunze zaidi kuhusu maisha Yake. Hizi hujumuisha maandiko, maneno ya manabii na hata mafunuo ya hivi leo.

Kitu kimoja nilichojifunza kutoka kwa Mwokozi ninapojifunza kuhusu maisha Yake ni kwamba aliwaalika wote wamfuate Yeye. Katika Mathayo 4:19, Kristo alitoa mwaliko huu kwa wavuvi aliokutana nao ukingoni mwa bahari: “Nifuateni, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa watu”, na tunaona jinsi kukubali mwaliko huu kulivyobadili maisha ya wavuvi hawa. Hivyo, ninaamini kwamba, kama wafuasi Wake, tunaitwa kuwaalika wengine wamfuate Yeye.

Maandiko yanatufundisha kwamba kuna shangwe katika kuzileta nafsi kwa Kristo na tunaahidiwa shangwe kuu pamoja nao katika ufalme wa Mungu. Wengi wamejitoa na kuwaalika wengine.

Mfalme Dario, katika Agano la Kale, wakati aliposhuhudia nguvu ya Mungu wa Danieli, alituma tangazo kwa watu wote wa nchi katika lugha zao, akiwaamuru wamche Mungu wa Danieli.

Kitabu cha Mormoni pia kinasimulia hadithi ya jinsi Mlamani aitwaye Abishi ambaye alikuwa ameongoka kwa Bwana miaka mingi iliyopita, alivyowaalika wengine waende kwenye nyumba ya Mfalme Lamoni kushuhudia nguvu ya Mungu. Alifanya hivyo kwa ujasiri, licha ya uhasama ambao watu wake, Walamani, walikuwa nao dhidi ya Wanefi. Maandiko yanaeleza kwamba alikimbia kutoka nyumba hadi nyumba (Alma 19:16-17).

Lehi, pia, aliyatoa maisha yake yote akiialika familia yake kuishi Injili. Ninajua kwamba kila mmoja wetu, ambaye amechagua kumfuata Kristo, ameitwa kuitangaza injili Yake ulimwenguni kote ili kuzileta kweli hizi kwa wengine na kisha kuwaalika wamfuate Yesu Kristo ambaye ndiye Njia Pekee ya uzima wa milele.

Mimi pamoja na mume wangu tunapambana kuifanya nyumba yetu iwe mahali pa sisi na watoto wetu kujifunza injili. Tunawasaidia wao wapate ushuhuda wao kwenye kanuni hizi. Kupitia sala, tunapokea mwongozo wa jinsi ya kuwafundisha kwa kuwa bado ni wadogo na bado hawana uelewa kamili wa mambo yote.

Kuwaalika wengine daima siyo kazi rahisi, lakini tunapata nguvu na faraja katika Kristo. Katika mahubiri yake ya Mkutano Mkuu wa Aprili 2023, Mzee Soares wa Akidi ya Kumi na Wawili alisema: “Kama wafuasi Wake, sisi ni watu Wake wa kipekee, tulioitwa kutangaza wema Wake, wakuzaji wa amani ambayo kwa ukarimu ilitolewa kupitia Yeye pamoja na dhabihu Yake ya kulipia dhambi. Amani hii ni zawadi iliyoahidiwa kwa wote wanaogeuza mioyo yao kuelekea kwa mwokozi na kuishi kwa haki; amani hiyo hutupatia nguvu ya kupata shangwe kwenye maisha haya na kutusaidia tuvumilie majaribu machungu ya safari yetu.”

Pia tunaweza kujialika sisi wenyewe kumfuata Kristo. Acha tufikirie kuhusu kanuni zote za injili ambazo hatuziishi na kisha tudhamirie kuanzia sasa kufanya kila linalowezekana ili kubadilika. Katika familia yangu, tumetengeneza orodha ya vitu tutakavyovifanyia kazi mwaka huu ili kuwa bora na kusonga karibu na Mwokozi.

Nashuhudia kwamba mwokozi ni mfano wa kufuata, katika jina la Yesu kristo, amina!

Chapisha