2010–2019
Wafuasi wa Kweli wa Mwokozi
Mkutano Mkuu wa Oktoba 2019


Wafuasi wa Kweli wa Mwokozi

Tunaweza kuhisi shangwe ya kudumu pale Mwokozi na injili Yake vinapokuwa mfumo ambao tunajenga maisha yetu.

Kwa kiasi fulani kilichojificha ndani ya Agano la Kale kwenye kitabu cha Hagai ni maelezo ya kundi la watu ambao wangeweza kutumia ushauri wa Mzee Holland. Walikuwa wamekosea kwa kutomuweka Kristo kitovu cha maisha yao na huduma yao. Hagai anachora baadhi ya picha zenye maneno ya kuchochea fikra pale anapotoa karipio kwa watu kwa kukaa katika nyumba zao nzuri badala ya kujenga hekalu la Bwana:

“Je! Huu ndio wakati, wa ninyi, kukaa katika nyumba zenye mapambo ya mbao, iwapo nyumba hii inakaa hali ya kuharibika?

“Basi sasa, Bwana wa majeshi asema hivi; Zitafakarini njia zenu.

“Mmepanda mbegu nyingi, mkavuna kidogo; mnakula, lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo, lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka.

“Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu.”1

Je, huvutiwi na maelezo hayo ya upuuzi wa kuyapa kipaumbele mambo yasiyo na matokeo ya milele juu ya mambo ya Mungu?

Katika mkutano wa sakramenti niliohudhuria hivi majuzi, mmisionari aliyerudi alimnukuu baba ambaye alifupisha wazo hili kikamilifu wakati alipowaambia watoto wake, “Tunachohitaji hapa ni Wi-Fi kidogo na Nefi nyingi!”

Nikiwa nimeishi Afrika ya Magharibi kwa miaka mitano, niliona mifano tele ya watu waiipa kipaumbele injili kiuhasilia na pasipo aibu. Mfano mmoja kama huo ni jina la biashara ya kurekebisha matairi na kuweka usawa kwenye usukani huko Ghana. Mmiliki aliipa jina “Mapenzi Yako Yafungamane.”

Tunaweza kuhisi shangwe ya kudumu2 pale Mwokozi na injili Yake vinapokuwa mfumo ambao tunajenga maisha yetu. Hata hivyo, ni rahisi sana kwa mfumo huo kuwa, badala yake, mambo ya ulimwengu, ambapo injili hukaa kama pendeleo la ziada au kama kuhudhuria tu kanisani kwa masaa mawili Jumapili. Wakati hii inapokuwa hivi, inakuwa sawa na kuweka mishahara yetu katika “mfuko uliotoboka toboka.”

Hagai anatuambia kuwa wenye kujitolea—kuwa, kama tunavyosema huko Australia, “kusudi la haki” kwenye kuishi injili. Watu wanakuwa na kusudi la haki wakati wanapokuwa kile wanachojitambulisha kuwa.

Nilijifunza kidogo kuhusu kuwa na kusudi la haki na kujitolea kwa kucheza ragbi. Nilijifunza kuwa wakati nilipocheza kwa nguvu, wakati nilipotoa uwezo wangu wote, furaha yangu ya mchezo ilikuwa kubwa.

Picha
Mzee Vinson akiwa na timu yake ya ragbi

Mwaka wangu pendwa wa ragbi ulikuwa mwaka baada ya shule ya upili. Timu ambayo nilikuwa mshiriki ilikuwa yenye kipaji na yenye kujitolea. Tulikuwa timu bingwa mwaka ule. Hata hivyo, siku moja ilikuwa tucheze na timu yenye kiwango cha chini, na baada ya mchezo sote tulikuwa na miadi ya kuwapeleka wasichana kwenye dansi kubwa, ya mwaka ya chuo. Nilidhani kwamba kwa sababu huu ungekua mchezo rahisi, nilipaswa kujilinda kutokana na majeraha ili niweze kufurahia dansi kikamilifu. Katika mchezo ule, hatukujitolea katika miguso migumu kama ambavyo tulipaswa, na tulipoteza. Kufanya mambo kuwa mabaya zaidi, nilimaliza mchezo kwa mdomo uliovimba, mnene ambao haukuruhusu mwonekano wangu kwa ajili ya miadi kubwa. Pengine nilihitajika kujifunza kitu.

Uzoefu tofauti sana ulitokea katika mchezo wa baadaye ambapo nilijitolea kikamilifu. Kuna wakati nilikimbia kwa kusudi la dhati kwenye mguso; mara moja nilihisi maumivu usoni kwangu. Nikiwa nimefunzwa na baba yangu kwamba kamwe sipaswi kuruhusu upinzani ujue ikiwa nimeumia, niliendelea kucheza mchezo. Usiku ule, wakati nikijaribu kula, niligundua kwamba sikuweza kung’ata. Asubuhi iliyofuata, nilikwenda hospitali, ambapo mionzi ilithibitisha kwamba taya langu lilikuwa limevunjika. Mdomo wangu ulifungwa waya kwa wiki sita zilizofuatia.

Mafunzo yalipatikana kutokana na mfano huu wa mdomo mnene na taya lililovunjika. Licha ya kumbukumbu zangu za matamanio yasiyoisha ya chakula kigumu kipindi cha wiki sita wakati ambapo ningeweza kutumia maji maji tu, sihisi majuto kuhusu taya langu lililovunjika kwa sababu ilitokana na kujitoa kwangu kote. Lakini nina majuto kuhusu mdomo mnene kwa sababu uliashiria kujitoa kiasi.

Kutoa vyote haimaanishi kwamba daima tutakuwa tumefungwa katika baraka au daima kufanikiwa. Lakini inamaanisha kwamba tutakuwa na shangwe. Shangwe si starehe ya mara moja au hata furaha ya muda. Shangwe hudumu na imejengwa juu ya juhudi zetu za kukubalika na Bwana.3

Mfano wa kukubalika huko ni hadithi ya Oliver Granger. Kama Rais Boyd K. Packer alivyosema: “Wakati watakatifu walipofukuzwa kutoka Kirtland, … Oliver alibaki nyuma kuuza mali zao kwa kiasi kidogo ambacho angeweza. Hakukua na uwezekano mkubwa kwamba angeweza kufanikiwa. Na, hakika, hakufanikiwa!”4 Alikuwa amepewa jukumu na Urais wa Kwanza kutimiza jukumu ambalo lilikuwa gumu, kama si lisilowezekana. Lakini Bwana alimsifu kwa juhudi zake dhahiri zisizo na mafanikio katika maneno haya:

“Ninamkumbuka mtumishi wangu Oliver Granger; tazama, amini ninamwambia yeye kwamba jina lake litakumbukwa kuwa takatifu kutoka kizazi hadi kizazi, milele na milele, asema Bwana.

“Kwa hiyo, na apambane kwa dhati kwa ajili ya ukombozi wa Urais wa Kwanza wa Kanisa langu, … na ikiwa ataanguka atainuka tena, kwani dhabihu yake itakuwa takatifu zaidi kwangu Mimi kuliko mafanikio yake, asema Bwana.”5

Hilo linaweza kuwa kweli juu yetu sote—si mafanikio yetu bali dhabihu na juhudi zetu ambazo zina umuhimu kwa Bwana.

Mfano mwingine wa mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo ni rafiki yetu mpendwa huko Côte d’Ivoire Afrika Magharibi. Dada huyu mzuri, mwaminifu aliteseka hisia mbaya, na hata baadhi ya unyanyasaji wa kimwili, kutoka kwa mume wake kwa muda mrefu kiasi, na hatimaye walitalikiana. Hakuwahi kamwe kuyumba katika imani na wema wake, lakini kwa sababu ya ukatili wa mumewe, dada huyu alikuwa ameumia sana kwa muda mrefu. Kwa maneno yake mwenyewe, anaelezea kile kilichotokea:

“Japo nilisema nimemsamehe, daima nililala na jeraha; niliishi siku zangu kwa jeraha hilo. lilikuwa ni kama moto katika moyo wangu. Mara nyingi niliomba kwa Bwana aliondoe kwangu, lakini liliuma kiasi kwamba niliamini ningeishi maisha yangu yote nikiwa nalo. Liliuma kuliko wakati nilipompoteza mama yangu nikiwa na umri mdogo; liliuma kuliko wakati nilipompoteza baba yangu na hata mwanangu. Lilionekana kusambaa na kufunika moyo wangu, likinipa msukumo kwamba ningekufa muda wowote.

“Wakati mwingine nilijiuliza mwenyewe kile ambacho Mwokozi angefanya katika hali yangu, na hakika ningesema, ‘Hii inachosha, Bwana.’

“Kisha asubuhi moja nilitazama maumivu yaliyotokana na haya yote katika moyo wangu na kwenda mbali zaidi, nikiyatazama katika nafsi yangu. Hayakuonekana. Akili yangu kwa haraka ilipitia kurejea sababu zote [nilizokuwa nazo] za kuhisi maumivu, lakini sikuhisi maumivu. Nilisubiri siku nzima ili kuona ikiwa ningehisi maumivu katika moyo wangu; sikuyahisi. Kisha nilipiga magoti na kumshukuru Mungu kwa kufanya dhabihu ya upatanisho wa Bwana itende kazi kwangu.”6

Dada huyu sasa kwa furaha ameunganishwa kwa mwanaume mzuri, mwaminifu anayempenda kwa dhati.

Hivyo mtazamo wetu unapaswa kuwa vipi ikiwa sisi ni wafuasi wa kweli wa Kristo? Na injili ina thamani gani kwetu pale “tunapozitafakari njia [zetu],” kama Hagai alivyopendekeza?

Ninapenda mfano wa mtazamo sahihi uliooneshwa na baba wa Mfalme Lamoni. Mtakumbuka hasira yake ya mwanzo kwa kumkuta mwanawe akiwa ameambatana na Amoni, Mnefi—watu ambao Walamani waliwachukia. Alivuta upanga wake kushindana na Amoni na punde alikuta upanga wa Amoni kwenye koo lake mwenyewe. “Sasa mfalme, akiogopa kwamba atapoteza uhai wake, alisema: Ukiniokoa nitakupa chochote utakachoniomba, hata kama ni nusu ya ufalme.”7

Kumbuka ahadi yake—nusu ya ufalme wake kwa ajili ya maisha yake.

Lakini baadaye, baada ya kuelewa injili, alitoa ahadi nyingine. “Mfalme alisema: Nitafanya nini ili nipate uzima wa milele ambao umeuzungumzia? Ndio, nitafanya nini ili nizaliwe kwa Mungu, ili hii roho mbovu ing’olewe nje ya mwili wangu, na nipokee Roho yake, ili niweze kujazwa na shangwe, ili nisitupiliwe nje siku ya mwisho? Tazama, alisema, nitatoa umiliki wangu wote, ndio, nitaacha ufalme wangu, ili nipokee hii shangwe kuu.”8

Wakati huu, alikuwa amejiandaa kutoa ufalme wake wote, kwa sababu injili ilikuwa na thamani kuliko vyote alivyokuwa navyo! Alikuwa na kusudi la haki kwenye injili.

Hivyo, swali kwa kila mmoja wetu ni, je, sisi pia tuna kusudi la haki kwenye injili? Kwa sababu kutofanya kwa moyo wote si kuwa na kusudi la haki! Na Mungu hajulikani kwa kumwaga sifa kwa vuguvugu.9

Hakuna hazina, wala jambo lolote la kuburudisha, wala cheo chochote, wala mtandao wowote wa kijamii, wala mchezo wowote wa video, wala mchezo wowote, wala muunganiko wowote na mtu maarufu, wala chochote duniani ambacho kina thamani zaidi kuliko maisha ya milele. Hivyo ushauri wa Bwana kwa kila mtu ni “zitafakarini njia zenu.”

Hisia zangu zinaelezewa vyema katika maneno ya Nefi: “Nafurahia kwa uwazi; nafurahia ukweli; namfurahia Yesu wangu, kwani ameikomboa nafsi yangu kutoka jahanamu.”10

Je, sisi ni wafuasi wa kweli wa Yeye aliyetoa Vyake vyote kwa ajili yetu? Yeye ambaye ni Mkombozi wetu na Mwombezi wetu kwa Baba? Yeye ambaye alijitoa hasa katika dhabihu ya upatanisho Wake na vivyo hivyo sasa katika upendo Wake, rehema Yake, na hamu Yake kwetu kupata shangwe ya milele? Nawasihi wale wote wanaosikiliza na kusoma maneno haya: Tafadhali, tafadhali msiondoe kujitolea kwenu kote mpaka mtakapokamilisha katika baadhi ya wakati ujao, usioonekana. Pata kusudi la haki sasa na uhisi shangwe! Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha