2010–2019
Kuheshimu Jina Lake
Mkutano Mkuu wa Oktoba 2019


Kuheshimu Jina Lake

Kwa utambulisho wa agano na kuwa wake, tunaitwa kwa jina la Yesu Kristo.

Kama wazazi wanavyongojea kwa hamu kuzaliwa kwa mtoto, wana jukumu la kuchagua jina kwa ajili ya mtoto wao mpya. Pengine wakati ulipozaliwa, ulipokea jina ambalo lilipitishwa katika familia yako kwa vizazi vingi. Au labda jina ulilopewa lilikuwa maarufu katika mwaka au eneo ulilozaliwa.

Nabii Helamani na mkewe waliwapa majina ya kifamilia yenye maana watoto wao wachanga Nefi na Lehi. Helamani baadaye aliwaambia wanawe:

“Nimewapatia majina ya wazazi wetu wa kwanza … ili mnapokumbuka majina yenu mtaweza kuwakumbuka; na mnapowakumbuka mngekumbuka kazi zao … vile zimesemwa, na pia kuandikwa, kwamba walikuwa wazuri.

“Kwa hivyo, wana wangu, ninataka kwamba mfanye yale ambayo ni mazuri,”1

Majina ya Nefi na Lehi yaliwasaidia kukumbuka kazi nzuri za mababu zao na kuwatia moyo kufanya vizuri pia.

Akina Dada, haijalishi tunaishi wapi, tunazungumza lugha gani, au tuna umri wa miaka 8 au 108, sote tunashiriki jina maalumu ambalo lina malengo sawa na hayo.

“Maana [sisi] sote tuliobatizwa katika Kristo, tumemvaa Kristo … maana [sisi] sote tumekuwa mmoja katika Kristo Yesu.”2

Kama waumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, “kwanza tuliahidi utayari wetu wa kujichukulia juu yetu jina la Kristo … kupitia ibada ya Ubatizo.”3 Kupitia agano hili, tuliahidi daima kumkumbuka, kushika amri zake, na kuwatumikia wengine. Utayari wetu wa kutunza agano hili hufanywa upya kila siku ya Sabato tunapopokea sakramenti na kufurahia tena katika baraka za “[kuenenda] katika upya wa uzima.”4

Jina tulilopewa wakati wa kuzaliwa linatoa taswira ya utambulisho wetu binafsi na kutufanya kuwa sehemu ya familia zetu za kidunia. Hata hivyo, wakati “tulipozaliwa mara ya pili” kwenye ubatizo, ufahamu wetu juu ya sisi ni kina nani ulikuzwa. “Kwa sababu ya agano lile ambalo mmefanya mtaitwa watoto wa Kristo,… kwani tazama, … amewazaa kiroho; kwani mnasema kwamba mioyo yenu inabadilishwa kwa imani katika jina lake; kwa hivyo, amewazaa.”5

Kwa hivyo, kwa utambulisho wa agano na kuwa wake, tunaitwa kwa jina la Yesu Kristo. Na “hakuna jina lingine litakalotolewa wala njia nyingine wala mbinu yoyote ambayo wokovu utawashukia watoto wa watu, ila tu katika na kupitia jina la Kristo Bwana Mwenyezi.”6

Jina la Yesu lilijulikana muda mrefu kabla ya kuzaliwa Kwake. Kwa mfalme Benyamini, malaika alitabiri, “Na ataitwa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, … na mama yake ataitwa Mariamu.7 Kazi yake ya “upendo ukomboao”8 pia ilijulishwa kwa watoto wa Mungu wakati wowote ambapo injili imekuwapo duniani, tangu siku za Adamu na Hawa hadi siku yetu, ili waweze kujua “asili ya kutegemea msamaha wa dhambi zao.”9

Mwaka jana, Rais Russell M. Nelson alitoa “ombi la kinabii” kwa akina dada ili “kuumba wakati ujao kwa kusaidia kukusanya Israeli iliyotawanyika.” Alitualika kusoma Kitabu cha Mormoni na “kuwekea alama kila aya ambayo inamzungumzia au inamtaja Mwokozi.” Alituomba kwamba “tuwe na shauku ya kuzungumza kuhusu Kristo, kufurahia katika Kristo, na kuhubiri kuhusu Kristo pamoja na [familia zetu] na rafiki zetu.” Pengine umeanza kutambua matunda ya ahadi yake kwamba “wewe na wao mtasogea karibu na Mwokozi … Na mabadiliko, hata miujiza, itaanza kutokea.”10

Ahadi yetu ya daima kumkumbuka Mwokozi hutupatia nguvu ya kusimamia ukweli na haki—iwe tupo katika umati mkubwa au katika sehemu zetu binafsi, ambapo hakuna yeyote anayejua matendo yetu isipokuwa Mungu. Tunapomkumbuka yeye na jina Lake tunalobeba, hatuna nafasi kwenye kujilinganisha kwa kujidhalilisha au hukumu za kupita kiasi. Macho yetu yakiwa kwa Mwokozi, tunajiona vile tulivyo hasa—mtoto mwenye thamani wa Mungu.

Kukumbuka agano letu kunafifisha wasiwasi wa kidunia, kunageuza shaka binafsi kuwa ujasiri, na kutoa tumaini wakati wa majaribu.

Na wakati tunapojikwaa na kuanguka katika maendeleo yetu kwenye njia ya agano, tunapaswa tu kukumbuka jina Lake na fadhili Zake za upendo kwetu. “Kwani ana uwezo wote, hekima yote, na akili yote; anaelewa vitu vyote, na ni Kiumbe cha huruma … kwa wale ambao watatubu na kuamini katika jina lake.”11 Hakika, hakuna sauti tamu kuliko jina la Yesu kwa wale wote ambao, kwa moyo uliovunjika na roho iliyopondeka, wanatafuta “kufanya vizuri zaidi na kuwa wazuri zaidi.”12

Rais Nelson alifundisha: “Siku imepita ambapo unaweza kuwa Mkristo mtulivu na aliyeridhika. Dini yako siyo tu kuhusu kujitokeza kanisani Jumapili. Ni kuhusu kujitokeza kama mfuasi wa kweli kuanzia Jumapili asubuhi hadi Jumamosi usiku. … Hakuna kitu kama ‘mfuasi wa muda’ wa Bwana Yesu Kristo.”13

Utayari wetu wa kujichukulia juu yetu jina la Kristo ni zaidi ya mabadilishano rasmi ya maneno. Siyo ahadi ya kupita tu au mshikamano wa kitamaduni. Siyo kanuni ya kifungu au beji ya jina tunayovaa. Siyo msemo ambao kwa urahisi tunauweka kwenye rafu au kuutundika juu ya ukuta. Lake ni jina ambalo “huwekwa,”14 huandikwa mioyoni mwetu, na “kuchorwa katika nyuso [zetu].”15

Dhabihu ya upatanisho ya Mwokozi inapaswa kukumbukwa, kila wakati, kupitia mawazo yetu, matendo, na mwingiliano wetu na wengine. Si tu kwamba Yeye hukumbuka majina yetu, bali anatukumbuka sisi kila wakati. Mwokozi alitangaza:

“Kwani mwanamke anaweza kusahau mtoto wake ambaye anamnyonyesha, kwamba asiwe na huruma kwa mwana wa tumbo lake? Ndio, wanaweza kusahau, lakini sitakusahau, Ee nyumba ya Israeli.

“Tazama, Nimewachora kwenye viganja vya mikono yangu.”16

Rais George Albert Smith alifundisha, “Heshimu majina uliyo nayo, kwa sababu siku moja utakuwa na fursa na jukumu la kutoa ripoti … kwa Baba yako aliye mbinguni … kile ulichofanya kwa [majina hayo].”17

Kama majina yaliyochaguliwa kwa uangalifu ya Nefi na Lehi, je! inaweza kusemwa na kuandikwa kwetu kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Bwana Yesu Kristo? Je! tunaheshimu jina la Yesu Kristo ambalo tumejichukulia wenyewe kwa hiari? Je! sisi ni “watumishi na mashahidi”18 wa fadhili zake za upendo na nguvu Zake za ukombozi?”

Siyo muda mrefu uliopita, nilikuwa nikisikiliza Kitabu cha Mormoni. Katika sura ya mwisho ya 2 Nefi, nilimsikia Nefi akisema kitu ambacho sikuwahi kukisoma kabla kama kilivyosomwa. Kote katika historia yake, anafundisha na kushuhudia juu ya “Mkombozi,” “Mtakatifu wa Israeli,” “Mwanakondoo wa Mungu,” na “Masiya.” Lakini wakati akihitimisha maelezo yake, nilimsikia akisema maneno haya: “Nafurahia kwa uwazi; nafurahia ukweli; namfurahia Yesu wangu, kwani ameikomboa nafsi yangu.”19 Niliposikia maneno haya, moyo wangu ulifurahia na ilibidi nisikilize tena na tena. Nilitambua na kuitikia aya hiyo kama vile ninavyotambua na kuitikia jina langu mwenyewe.

Bwana amesema, “Ndio, heri watu hawa ambao wako tayari kulichukua jina langu; kwani wataitwa kwa jina langu; na watakuwa wangu.”20

Kama waumini wa Kanisa La Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, acha “[tujichukulie] kwa furaha jina la Kristo”21 kwa kuheshimu jina lake kwa upendo, kujitolea, na kazi nzuri. Ninashuhudia kwamba yeye ni “Mwanakondoo wa Mungu, ndio, hata Mwana wa Baba wa Milele.”22 Katika jina la mwana Wake mtakatifu, Yesu Kristo, amina.

Chapisha