Mkutano Mkuu
Nguvu ya Kitabu cha Mormoni katika Uongofu
Mkutano mkuu wa Aprili 2020


Nguvu ya Kitabu cha Mormoni katika Uongofu

Kitabu cha Mormoni kinatoa lishe ya kiroho, huelezea mpango wa kutenda, na kutuunganisha na Roho Mtakatifu.

Baada ya kukagua ripoti kutoka kwenye uchunguzi wa afya wa hivi karibuni, nilijifunza kuwa nilihitaji kufanya marekebisho ya mtindo wa maisha. Ili kunisaidia, daktari wangu aliniandikia mpango wa lishe na mazoezi, ambao, ikiwa ningechagua kuufuata, ungenibadilisha kuwa mtu mwenye afya.

Kama kila mmoja wetu angefanya uchunguzi wa kiroho, tungejifunza nini kuhusu sisi wenyewe? Je, ni marekebisho gani ambayo daktari wetu wa kiroho angetuagiza? Kwa sisi kuwa wale tunaohitaji kuwa, ni muhimu kujua nini cha kufanya na kufanya kile tunachojua.

Yesu Kristo ni Daktari Mkuu.1 Kupitia Upatanisho Wake, Yeye hufunga majeraha yetu, huchukua udhaifu wetu, na huponya mioyo yetu iliyovunjika.2 Kupitia neema Yake udhaifu wetu utaimarika.3 Anatualika tumfuate Yeye4 kwa kujifunza kutoka Kwake, kusikiliza maneno Yake, na kutembea katika unyenyekevu wa Roho Yake.5 Ameahidi kutusaidia sisi6 katika mchakato huu wa maisha ya uongofu, ambao hutubadilisha sisi na kuleta furaha ya milele.7

Mwokozi ametupa Kitabu cha Mormoni kama nyenzo yenye nguvu ya kusaidia katika uongofu. Kitabu cha Mormoni kinatoa lishe ya kiroho, huelezea mpango wa kutenda, na kutuunganisha na Roho Mtakatifu. Kikiwa kimeandikwa kwa ajili yetu,8 kimebeba neno la Mungu katika uwazi9 na kinatuambia asili yetu, lengo letu, na takdiri yetu.10 Pamoja na Biblia, Kitabu cha Mormoni kinamshuhudia Yesu Kristo11 na kinatufundisha jinsi tunavyoweza kujua ukweli na kuwa kama Yeye.

Picha
Kaka Saw Polo

Kaka Saw Polo alikuwa na umri wa miaka 58 alipotambulishwa kwenye injili iliyorejeshwa ya Yesu Kristo. Nilipokutana naye, alikuwa akihudumu kama rais wa tawi kwa miaka kadhaa, lakini niligundua kwamba hakuwa amesoma Kitabu cha Mormoni kwa sababu kilikuwa hakipatikani kwa lugha yake ya Kiburma. Wakati nilipomuuliza alijuaje kuwa kitabu hicho kilikuwa cha kweli bila kukisoma, alijibu kwamba alisoma kitabu cha picha Hadithi za Kitabu cha Mormoni kila siku kwa kuangalia vielelezo, kwa kutumia Kamusi ya kutafsiri maneno ya Kiingereza, na kuchukua kwa uangalifu maelezo ya yale aliyojifunza. Alifafanua, “Kila wakati niliposoma, ningesali juu ya yale niliyojifunza, na ningehisi amani na furaha, akili yangu ingekuwa wazi, na moyo wangu ungekuwa laini. Nilihisi Roho Mtakatifu akinishuhudia kwamba kilikuwa cha kweli. Ninajua kwamba Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu.”

Kama vile Kaka Saw Polo, kila mmoja wetu anaweza kusoma Kitabu cha Mormoni kulingana na hali zetu. Tunapotaka kuamini na kutafakari mafundisho yake mioyoni mwetu, tunaweza kumuuliza Mungu kwa imani ikiwa mafundisho ni ya kweli.12 Ikiwa tu waaminifu katika hamu yetu ya kujua na tunayo nia ya kweli ya kuchukua hatua, Yeye atatujibu mioyoni mwetu kupitia Roho Mtakatifu. Ni kwa nguvu za Roho Mtakatifu kwamba tutajua ukweli wa vitu vyote.13 Tunapopata ushuhuda wa kiungu wa Kitabu cha Mormoni, pia tutajua kwa nguvu ile ile kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wa ulimwengu, kwamba Joseph Smith ndiye nabii Wake, na kwamba Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwiso ni Kanisa Lake lililorejeshwa.14

Kama kijana nikiwa naanza huduma yangu ya umisionari, nilipanda ndege kwenda Australia. Nikihisi kuwa mpweke, mwenye wasiwasi, na asiyetosha lakini aliyejitolea kuhudumu, nilihitaji tena hakikisho kuwa kile nilichoamini ni kweli. Nilisali na kusoma maandiko yangu kwa bidii, lakini kadiri safari ilivyoendelea, shaka yangu binafsi ilizidi kuongezeka na hali yangu ya mwili ilizidi kudhoofika. Baada ya kupata taabu kwa masaa kadhaa, mhudumu wa ndege alipita na kusimama karibu na kiti changu. Alikichukua Kitabu cha Mormoni nilichokuwa nasoma kutoka mikononi mwangu. Alitazama kwenye ukurasa wa mbele na akasema, “Hicho ni kitabu kizuri!” kisha akanirudishia kitabu na kuendelea kutembea. Sikuwahi kumuona tena.

Wakati maneno yake yalipokuwa yakisikika masikioni mwangu, nilisikia wazi na nilihisi moyoni mwangu, “Niko hapa, na ninajua wewe ulipo. Fanya tu kadiri ya uwezo wako, kwa maana nitayafanya mengine.” Kwenye ndege ile juu ya Bahari ya Pacific, nilipata ushahidi binafsi kupitia kusoma kwangu Kitabu cha Mormoni na mwongozo wa Roho Mtakatifu kwamba Mwokozi wangu alijua mimi ni nani na kwamba injili ni ya kweli.

Mzee David A. Bednar alifundisha: “Kujua kuwa injili ni ya kweli ndiyo msingi wa ushuhuda. Kuwa mkweli kila wakati katika injili ndio msingi wa uongofu.”15 Uongofu unatutaka sisi kuwa “watendaji wa neno, na siyo wasikilizaji tu.”16 Utekelezaji wa mpango wa Bwana kwetu—mafundisho ya Kristo—unafundishwa kwa uwazi zaidi kwenye Kitabu cha Mormoni.17 Unajumuisha:

  • Kwanza, kuonesha imani katika Yesu Kristo kwa kumwamini Yeye, kutii amri Zake, na kujua kuwa Atatusaidia.18

  • Pili, kutubu kila siku makosa yetu na kupata furaha na amani pale Anapotusamehe.19 Toba inahitaji sisi kuwasamehe wengine20 na inatusaidia sisi kusonga mbele. Mwokozi ameahidi kutusamehe kila wakati tunapotubu.21

  • Tatu, kufanya na kutunza maagano na Mungu kupitia ibada kama vile ubatizo. Hii itatufanya sisi tubaki kwenye njia ya agano ambayo inatuongoza Kwake.22

  • Nne, kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kipawa hiki kinatuwezesha kuwa na wenza wa kudumu wa yule anayetakasa, kufariji, na kutuongoza sisi.23

  • Tano, kuvumilia hadi mwisho kwa kusonga mbele kwa bidii huku tukisherehekea neno la Kristo kila siku.24 Kwa kula na kusherehekea kutoka Kitabu cha Mormoni na kushikilia mafundisho yake, tunaweza kushinda majaribu na kupokea mwongozo na ulinzi katika maisha yetu yote.25

Kwa kutumia mara kwa mara mafundisho ya Kristo katika maisha yetu, tutashinda hali ambayo inazuia mabadiliko na woga ambao unazuia kutenda. Tutapokea ufunuo binafsi, kwani Roho Mtakatifu “ atakuonyesha wewe vitu vyote unavyotakiwa kufanya,”26 na “maneno ya Kristo yatakuambia wewe vitu vyote unavyotakiwa kufanya.”27

Kwa miaka 20, Kaka Huang Juncong alisumbuka na pombe, sigara, na kamari ya mara kwa mara. Wakati alipotambulishwa kwa Yesu Kristo na injili Yake iliyorejeshwa, Kaka Huang alitamani kubadilika kwa ajili ya familia yake changa. Changamoto yake kubwa ilikuwa uvutaji wa sigara. Mvutaji mkubwa wa sigara, alijaribu kuacha mara nyingi bila ya mafanikio. Siku moja, maneno haya kutoka katika Kitabu cha Mormoni yalimwingia akilini mwake: “na moyo wa kweli, kwa kusudi halisi.”28 Ingawa majaribio ya awali yalishindwa, alihisi labda angebadilika kwa msaada kutoka kwa Baba wa Mbingu na Yesu Kristo.

Wamisionari waliunganisha imani yao na yake na walitoa mpango wa utekelezaji wa vitendo, pamoja na dozi nyingi za sala na kusoma neno la Mungu. Kwa moyo wa kweli na kusudi halisi, Kaka Huang alitenda kwa uaminifu na akagundua kuwa kadiri alivyofokasi zaidi kwenye tabia mpya alizotamani kuzikuza, kama vile kusoma Kitabu cha Mormoni, alifokasi kidogo kwenye tabia ambazo alitaka kuziacha.

Akikumbuka uzoefu wake kutoka miaka 15 iliyopita, alisema, “Sikumbuki ni lini hasa niliacha kuvuta sigara, lakini wakati nikijaribu sana kila siku kufanya vitu ambavyo nilijua nilihitaji kufanya kumkaribisha Roho wa Bwana katika maisha yangu na kuendelea kuvifanya, sikuwa nikivutiwa tena na sigara na sijawahi tangu hapo.” Kwa kuyatumia mafundisho ya Kitabu cha Mormoni, maisha ya Kaka Huang yamebadilishwa, na amekuwa mume na baba bora.

Picha
Huang Juncong na familia

Rais Russell M. Nelson ameahidi: “Unaposoma kwa maombi Kitabu cha Mormoni kila siku, utafanya maamuzi mazuri—kila siku. Ninaahidi kwamba unapotafakari kile unachojifunza, madirisha ya mbinguni yatafunguka, na utapata majibu ya maswali yako na mwongozo wa maisha yako mwenyewe. Ninaahidi kwamba unapozama kila siku kwenye Kitabu cha Mormoni, unaweza kukingwa dhidi ya maovu ya siku, hata tauni mbaya ya ponografia na uraibu mwingine wa kutia ganzi akili.”29

Marafiki wapendwa, Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu, na tutamkaribia Yeye kama tutakisoma.30 Tunapojaribu maneno yake, tutapata ushahidi wa ukweli wake.31 Tunapoishi siku zote kulingana na mafundisho yake, hatutakuwa “tena na hamu ya kutenda uovu.”32 Moyo wetu, mwonekano na asili yetu vitabadilika kuwa zaidi kama Mwokozi.33 Ninatoa ushahidi wangu wa hakika kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwokozi wetu, Mkombozi, na Rafiki. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha