Mkutano Mkuu
Fokasi kwa Yesu Kristo
Mkutano mkuu wa Aprili 2023


Fokasi kwa Yesu Kristo

Bwana Yesu Kristo ni suluhu ya shida zetu, lakini sisi lazima tuinue macho yetu na tuinue kuona kwetu ili tumwone Yeye.

Baba yangu alikuwa akiniambia, “Usifokasi sana kwenye shida zako ambazo hauwezi kuzitatua.”

Ninashuhudia kwamba Bwana Yesu Kristo ndiye suluhu ya shida zetu ngumu sana. Mahususi, Yeye ameshinda shida nne ambazo kila mmoja wetu anakabiliana nazo na ambazo si kila mmoja wetu tunaweza kusuluhisha wenyewe:

  1. Shida ya kwanza ni kifo cha kimwili. Tunaweza kujaribu kukichelewesha au kukipuuza, lakini hatuwezi kukishinda wenyewe. Yesu Kristo, hata hivyo, alishinda kifo kwa ajili yetu, na kama matokeo, sisi sote tutafufuliwa siku moja.1

  2. Shida ya pili hujumuisha taabu, uzoefu mgumu, huzuni, uchungu na uonevu wa ulimwengu huu. Yesu Kristo alishinda haya yote. Kwa wale wote wanaojitahidi kumfuata Yeye, siku moja “atafuta kila chozi” na kusawazisha mambo tena.2 Wakati huo huo, Yeye anaweza kutuimarisha kupitia majaribu yetu kwa kujiamini, furaha na amani.3

  3. Shida ya tatu ni kifo cha kiroho kutokana na dhambi. Yesu Kristo alishinda shida hii kwa kujichukulia juu Yake “adhabu ya amani yetu.”4 Kwa sababu ya dhabihu Yake ya upatanisho, tunaweza kufanywa huru kutokana na matokeo ya dhambi zetu kama tuna imani katika Mwokozi, tunatubu kwa dhati, tunakubali agano Baba analotoa kwetu kupitia ibada muhimu kama vile ubatizo, na kuvumilia hadi mwisho.5

  4. Shida ya nne ni asili zetu zenye ukomo, na mapungufu. Yesu Kristo ana suluhu ya shida hii pia. Yeye hafuti tu makosa yetu na kutufanya kuwa bila hatia tena. Yeye anafanya “mabadiliko makuu ndani … ya mioyo yetu, kwamba hatuna nia ya kutenda uovu tena, lakini kutenda mema daima.”6 Tunaweza kukamilishwa kwa neema ya Kristo na siku moja kuwa kama Yeye.7

Cha kusikitisha, mara nyingi tunazingatia sana shida zetu wenyewe kwamba tunapoteza fokasi ya suluhu, Mwokozi wetu Yesu Kristo. Ni kwa jinsi gani tunaepuka kosa hilo? Ninaamini jibu lipo katika maagano tunayoalikwa kufanya na Yeye na Baba yetu aliye Mbinguni.

Fokasi kwa Yesu Kristo kupitia Maagano

Maagano yetu yanatusaidia kufokasi umakini wetu, mawazo yetu na matendo yetu kwa Kristo. “Tunapoyashikilia maagano ambayo [sisi] tumeyafanya,” tunaweza kutambua kwa urahisi zaidi “mambo ya ulimwengu huu” ambayo tunapaswa “kuyaweka kando” na “mambo ya [ulimwengu] ulio bora” tunayopaswa kuyatafuta kwa bidii.8

Hicho ndicho watu wa Amoni walifanya katika Kitabu cha Mormoni. Walipojifunza kuhusu Yesu Kristo na kuanza kufokasi maisha yao Kwake, walitambua kwamba walipaswa kuzika silaha zao za vita na kuwa waaminifu kikamilifu na “walitambulika kwa juhudi yao kwa Mungu.”9

Kutii maagano hutuongoza kutafuta chochote kinachokaribisha ushawishi wa Roho na kukataa chochote kinachofukuzia mbali ushawishi huo—“kwani tunajua kwamba kama tunaweza kuwa wenye kustahili uwepo wa Roho Mtakatifu, tunaweza pia kustahili kuishi katika uwepo wa Baba wa Mbinguni na Mwanaye, Yesu Kristo.”10 Hii inaweza kumaanisha kwamba tunabadilisha msamiati wetu, tukitumia zaidi maneno ya ukarimu. Ingeweza kumaanisha kubadilisha tabia zilizo mbaya kiroho kwa tabia mpya ambazo zinaimarisha uhusiano wetu na Bwana, kama vile sala ya kila siku na kujifunza maandiko, binafsi na pamoja na familia zetu.

Rais Russell M. Nelson alisema kwamba “kila mtu anayefanya maagano katika visima vya ubatizo na hekaluni—na kuyashika—ameongeza ufikiaji wa nguvu ya Yesu Kristo. …

“Thawabu ya kutii maagano ni nguvu ya mbinguni—nguvu ambayo inatuimarisha sisi ili kustahimili majaribu, vishawishi na maumivu yetu ya moyo vyema zaidi.”11

Kufanya upya maagano yetu wakati wa sakramenti kila Jumapili ni nafasi nzuri sana ya kujitathmini wenyewe12 na kufokasi tena maisha yetu kwa Yesu Kristo. Kwa kupokea sakramenti, tunatangaza kwamba “daima tunamkumbuka Yeye.”13 Neno daima ni muhimu sana. Linaongeza ushawishi wa Mwokozi katika kila kipengele cha maisha yetu. Hatumkumbuki Yeye kanisani tu au wakati wa sala zetu za asubuhi au wakati tuko kwenye shida na tunahitaji kitu fulani.

Ndiyo, sisi wakati mwingine tunakanganywa. Tunasahau. Tunapoteza fokasi yetu. Lakini kufanya upya maagano yetu humaanisha kwamba sisi tunataka daima kumkumbuka Mwokozi, kwamba tutajaribu kufanya hivyo wiki nzima, na kwamba tutajitoa upya na kufokasi tena Kwake katika meza ya sakramenti wiki ijayo.

Kufokasi kwa Yesu Kristo katika Nyumba Zetu

Ni wazi, kufokasi kwa Yesu Kristo sharti kuwe zaidi ya Jumapili, katika shughuli ya kanisa. Wakati Rais Nelson alipotambulisha Njoo, Unifuate mwaka 2018, alisema, “Ni wakati wa Kanisa lenye kiini nyumbani,”14 Alisema tunapaswa “kuigeuza nyumba [yetu] kuwa mahali patakatifu pa imani” na “kituo cha kujifunza injili.” Na alitoa ahadi nne za kupendeza kwetu kama tutafanya hivyo.15

Ahadi ya kwanza: “Siku zenu za Sabato hakika zitakuwa za furaha.” Itakuwa ni siku tuyayosogea karibu zaidi na Mwokozi wetu. Kama msichana kutoka Peru alivyosema, “Siku ya Bwana ni siku ninayopata majibu mengi kutoka kwa Bwana.”

Ahadi ya pili: “Watoto wenu watafurahia kujifunza na kuishi mafundisho ya Mwokozi.” Hiyo ndiyo sababu ya sisi “kuzungumza kuhusu Kristo, kufurahia katika Kristo, kuhubiri kuhusu Kristo, … ili watoto wetu wajue asili ya kutegemea kwa msamaha wa dhambi zao.”16

Tunafanya hivyo ili kwamba siku moja, wakati mwana wetu anapokwenda kazini au anaposafiri milimani au anapowinda wanyama porini, kama vile Enoshi alivyofanya, aweze kukumbuka kile tulichomfunza kuhusu Kristo na kuhusu shangwe ya kuishi injili. Na nani anayejua? Labda hii itakuwa ile siku yeye atakapohisi njaa ya kiroho ambayo inamgeuza kwa Yesu Kristo ili aweze kusikia sauti ya Bwana ikimwambia, “Umesamehewa dhambi zako, na wewe utabarikiwa.”17

Ahadi ya tatu: “Ushawishi wa adui katika maisha yako na katika nyumba yako utapungua.” Kwa nini? Kwa sababu kadiri tunavyofokasi kwa Yesu Kristo, ndivyo zaidi dhambi zitapoteza mvuto wake.18 Nyumba zetu zinapojazwa na nuru ya Mwokozi, ndivyo kutakuwa na nafasi ndogo zaidi ya giza la adui.

Ahadi ya nne: “Mabadiliko katika familia yako yatakuwa ya ajabu na ya kudumu. Kwa nini? Kwa sababu badiliko ambalo Yesu Kristo huleta ni “badiliko kuu.”19 Yeye hubadilisha asili yetu; tunakuwa “viumbe vipya.”20 Hatua kwa hatua tunakuwa zaidi kama Mwokozi, tuliojazwa mioyo yetu kwa upendo Wake safi kwa watoto wote wa Mungu.

Ni nani asingependa ahadi hizi zitimizwe katika maisha yao na katika familia zao? Ni kipi tunahitaji kufanya ili tuzipate? Jibu ni kuzigeuza nyumba zetu kuwa mahali patakatifu pa imani na kituo cha kujifunza injili. Na ni kwa jinsi gani tunaweza kufanya hivyo? Kwa kufokasi kwa Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo, kuwafanya Wao kiini cha maisha ya familia yetu, ushawishi muhimu sana katika nyumba yetu.

Je, ningeweza kupendekeza kwamba uanze kwa kufanya maneno ya Kristo, yanayopatikana kwenye maandiko, kuwa sehemu ya maisha yako ya kila siku? Hakuna kanuni iliyotolewa kwa ajili ya kujifunza maandiko kikamilifu. Inaweza kuwa dakika 5 au 10 kila siku—au zaidi kama unaweza. Inaweza kuwa sura moja au aya chache kwa siku. Baadhi ya familia wanapendelea kujifunza asubuhi kabla ya kwenda shuleni au kazini. Wengine wanapendelea kusoma usiku kabla ya kulala. Baadhi ya wanandoa vijana wameniambia kwamba wanajifunza binafsi wakiwa njiani kwenda kazini na kisha wanashiriki umaizi na wenza wao kwa ujumbe mfupi ili kwamba maoni yao na majadiliano yarokodiwe

Njoo, Unifuate hutoa mapendekezo mengi ya shughuli na nyenzo ambazo zinaweza kuwasaidia watu binafsi na familia kujifunza kanuni za injili kutoka kwenye maandiko. Video za Biblia na video za Kitabu cha Mormoni zinaweza pia kuwa nyenzo za thamani za kufanya maandiko yapatikane zaidi kwa familia yako. Vijana na watoto mara nyingi wanatiwa msukumo kwa hadithi za kukumbukwa katika maandiko. Hadithi hizi, na kanuni za injili zilizomo, zitabaki kwa watoto, kama marafiki wa kutumainiwa, wanapohitaji mfano mzuri wa huduma, wema, utiifu, subira, ustahimilivu, ufunuo binafsi, hisani, unyenyekevu na imani katika Yesu Kristo. Baada ya muda, uthabiti wako katika kusherehekea neno la Mungu utawasaidia watoto wako wakue karibu na karibu zaidi na Mwokozi. Watakuja kumjua Yeye kushinda awali.

Bwana Yesu Kristo yu hai leo. Yeye anaweza kuwa uwepo hai na wa kila siku katika maisha yetu. Yeye ni suluhu ya shida zetu, lakini sisi lazima tuinue macho yetu na tuinue kuona kwetu ili tumwone Yeye. Yeye alisema “Nitegemeeni katika kila wazo; msitie shaka, msiogope.”21 Tunapofokasi Kwake na Baba yetu aliye Mbinguni, na kufanya na kutii maagano na Wao, na kuwafanya Wao kuwa ushawishi muhimu katika nyumba yetu na familia, tunakuwa aina ya watu Rais Nelson aliowafikiria: “Watu ambao wanaweza, wako tayari, na wanastahili kumpokea Bwana wakati anapokuja tena, watu ambao tayari wamemchagua Yesu Kristo dhidi ya ulimwengu ulioanguka; watu ambao wanashangilia haki yao ya kujiamulia ili kuishi sheria za juu zaidi na takatifu zaidi za Yesu Kristo.”22 Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha