Mkutano Mkuu
Je, Unataka Kuwa na Furaha?
Mkutano mkuu wa Oktoba 2023


Je, Unataka Kuwa na Furaha?

Baki katika njia ya agano. Maisha yako yatakuwa rahisi, yenye furaha, na yaliyojaa shangwe.

Je, unataka kuwa na furaha? Ni nini hukufanya usiwe na furaha? Rais Russell M. Nelson alisema: “Kama unataka kuwa na huzuni, vunja amri—na usitubu kamwe. Kama unataka kuwa na furaha, baki katika njia ya agano.”1 Je, siyo rahisi kuwa na furaha? Fanya maagano tu na kuyashika katika maisha yako. Hebu tupitie baadhi ya mambo ambayo yanaweza kutusaidia tubaki kwenye njia ya agano na kutufanya tuwe na furaha.

1. Njia ya Agano ni Nini?

Kulingana na Mzee Dale G. Renlund: “Neno njia ya agano humaanisha mtiririko wa maagano ambayo kupitia kwayo tunakuja kwa Kristo na kuunganika Naye. Kupitia muunganiko huu wa agano, tunaweza kufikia nguvu Zake za milele. Njia huanza na imani katika Yesu Kristo na toba, ikifuatiwa na ubatizo na kumpokea Roho Mtakatifu.”2 Tunaweka upya maagano haya kila wakati tunapopokea sakramenti.

Kuanzia na agano la ubatizo, tunafanya maagano zaidi katika maisha yetu yote. Tena, Mzee Renlund alisema: “Njia ya agano huongoza kwenye ibada za hekaluni, kama vile endaumenti ya hekaluni. Endaumenti ni zawadi ya Mungu ya maagano matakatifu ambayo hutuunganisha kikamilifu Kwake.”3

2. Je, Uko kwenye Njia ya Agano?

Wakati mwingine tunapofanya maagano, tunashindwa kuyashika. Wakati hii inapotokea, unawezaje kurudi kwenye njia ya agano? Acha nishiriki baadhi ya mifano ya kurudi kwenye njia ya agano.

Zaidi ya mwezi mmoja uliopita, nilipokea ujumbe kutoka kwa mmisionari aliyerejea ambaye alihudumu pamoja nasi. Alisema: “Muda wa mwisho umekuwa mgumu. Kupambana na wasiwasi na msongo wa mawazo kila siku kumekuwa kukinilemea na ni ngumu sana. Ninahisi mpweke na mwenye huzuni tu. Nimekuwa nikiomba mwongozo wa Baba yetu wa Mbinguni kwa ajili ya amani na faraja katika kile ninachoweza kufanya ili kupambana na magumu. … Nilipokuwa nikiomba na kutafuta mwongozo, nilihisi msukumo wa Roho ukiniambia kwamba nilihitaji kulipa zaka yangu kikamilifu. … Nilimhisi roho kwa nguvu sana na mara moja nilihisi hamu ya kufanya hivyo. Kwa nia ya kufanya hivyo nilihisi msukumo kwamba ‘ukilipa zaka yako kila kitu kitakuwa sawa.’ Bado ninajitahidi kupata amani, lakini nina ushuhuda katika Mwokozi wetu na kwamba kupitia utiifu wangu ninaweza kuhisi na kupata amani ninayoitafuta katika moyo na akili yangu. Hivi majuzi nimeamua kurudi kanisani na kupata mwongozo wa roho katika yote ninayofanya.”

Na sasa anaendelea vizuri. Unaweza pia kumwomba Baba wa Mbinguni amani, lakini jibu linaweza kuwa tofauti na vile unavyotarajia litakuwa. Mradi tu unatafuta kumjua Mwokozi na kuomba kwa Baba wa Mbinguni, Atakupa jibu lililoboreshwa kwa ajili yako.

Rais Thomas S. Monson alifundisha:

“Somo kuu tunaloweza kujifunza duniani ni kwamba wakati Mungu anapozungumza na sisi tunatii, daima tutakuwa sahihi.”4

“Tunaposhika amri, maisha yetu yatakuwa na furaha tele, yenye kuridhisha zaidi, na sio ya kutatanisha sana. Changamoto na shida zetu zitakuwa rahisi kuvumilia, na tutapokea baraka za [Mungu] alizoahidi.”5

Nilipoitwa kuwa askofu, ilikuwa ni wakati mgumu sana wa maisha yangu. Nilikuwa baba kijana katika miaka yangu ya mwanzo ya 30, lakini nilikuwa na matatizo ya kifedha kwa sababu ya changamoto za familia. Sikuweza kupata suluhisho lolote, na nilifikiri changamoto hazingeisha. Nilikuwa nimechoka kifedha na kihisia. Nilianza kutilia shaka nguvu zangu za kiroho pia. Ilikuwa ni wakati huo mgumu ambapo rais wangu wa kigingi alinipa wito. Nilikubali wito hata hivyo, japokuwa ulikuwa ni mgumu.

Mke wangu pia alikuwa na mahojiano na rais wa kigingi, lakini hakusema ndio, na hakusema hapana pia lakini alitiririkwa na machozi tu. Alilia kwa wiki nzima, akimwuliza Baba wa Mbinguni, “Kwa nini sasa?” na “Je, kweli unamjua kila mtu?” Hakupata jibu, lakini niliungwa mkono kama askofu Jumapili iliyofuata. Hakumuuliza Baba wa Mbinguni maswali hayo tena lakini aliniunga mkono katika wito wangu kwa miaka sita.

Siku ya Jumapili nilipopumzishwa, mke wangu alisikia sauti alipokuwa akipokea sakramenti. Sauti hiyo ilimnong’oneza, “Kwa sababu ilikuwa vigumu sana kwako kutembea, nilimwita kama askofu ili kukushika na kukutembeza.” Akikumbuka miaka sita iliyopita, aligundua kwamba changamoto zote nyingi ambazo zilionekana kutokuwa na mwisho sasa zilikuwa zimetatuliwa njiani.

Tulijifunza kwamba tunapofikiri kuwa si wakati mzuri kwetu kupokea wito, inaweza kuwa wakati tunaohitaji wito huo zaidi. Wakati wowote Bwana anapotuomba tutumikie katika wito wowote, iwe ni wito mwepesi au mzito, yeye huona mahitaji yetu. Yeye hutupatia nguvu tunazohitaji na ana baraka zilizo tayari kumwagwa juu yetu tunapotumikia kwa uaminifu.

Kuna mambo mengine tofauti yanayotuondoa kwenye njia ya agano. Bila kujali ni yapi, hatujachelewa kuelekeza mioyo yetu kwa Baba wa Mbinguni kwa ajili ya usaidizi. Mzee Paul V. Johnson alitufundisha: “Tunapomfuata Shetani, tunampa nguvu. Tunapomfuata Mungu, Yeye anatupatia nguvu.”6

Mfalme Benjamini katika Kitabu cha Mormoni anashuhudia: “Ningetamani mtafakari juu ya hali ya baraka na yenye furaha ya wale wanaotii amri za Mungu. Kwani tazama, wanabarikiwa katika vitu vyote, vya muda na vya kiroho; na kama watavumilia kwa uaminifu hadi mwisho watapokewa mbinguni, kwamba hapo waishi na Mungu katika hali ya furaha isiyo na mwisho.”7

3. Jinsi gani Kushika Maagano yako na Mungu kunaweza Kukufanya Uwe na Furaha?

Mke wangu anasema kwamba ndoa yetu inatuunganisha, na kwa sababu hiyo anaweza kufanya mambo ambayo hangeweza kufanya hapo awali. Kwa mfano, tangu alipokuwa mdogo, alikuwa na wakati mgumu kutoka nje gizani, lakini si vigumu tena kwa sababu ninaenda naye. Yeye ni mfupi na hawezi kufikia rafu ndefu isipokuwa atumie kiti au ngazi, lakini ninaweza kumfikishia vitu kutoka kwenye rafu ndefu kwa sababu mimi ni mrefu kuliko yeye. Kujifunga nira ya Mwokozi wetu ni kama hivyo. Tunapojifunga nira Kwake, tunaweza kufanya mambo ambayo hatungeweza kufanya sisi wenyewe kwa sababu Yeye anaweza kufanya mambo ambayo hatuwezi kujifanyia wenyewe.

Mzee David A. Bednar alisema, “Kufanya na kushika maagano matakatifu hutuunganisha na Bwana Yesu Kristo” Kimsingi, Mwokozi anatualika kumtegemea na kuvuta kwa pamoja Naye, ingawa juhudi zetu bora si sawa na zake na haziwezi kulinganishwa na Zake. Tunapomwamini na kuvuta mzigo wetu pamoja Naye wakati wa safari ya maisha ya duniani, kwa hakika nira Yake ni laini, na mzigo Wake ni mwepesi.”8

Rais Nelson pia amefundisha:

“Kujifunga nira na Mwokozi humaanisha kwamba unaweza kutumia nguvu Zake na uwezo Wake wa kukomboa.”9

“Thawabu ya kushika maagano na Mungu ni uweza wa kimbingu—nguvu ambayo inatuimarisha sisi ili kuhimili majaribu, vishawishi, na maumivu ya moyo vyema zaidi. Nguvu hii inarahisisha njia yetu. Wale wanaoishi sheria ya juu zaidi ya Yesu Kristo wanao uweza wa kufikia nguvu zake za hali ya juu zaidi.”10

“Kushika maagano kwa kweli hurahisisha maisha! Kila mtu anayefanya maagano katika visima vya ubatizo na hekaluni—na kuyashika—ameongeza upatikanaji wa uweza wa Yesu Kristo.”11

Wapendwa kaka zangu na dada zangu, je, mnataka kuwa na furaha? Baki katika njia ya agano. Maisha yako yatakuwa rahisi, yenye furaha, na kujawa na shangwe. Mwokozi wetu anatualika, “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.”12 Yeye ni Kristo aliye hai. Yeye hubeba mizigo yetu na hurahisisha maisha yetu. Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha