Mkutano Mkuu
Mnyenyekevu Kukubali na Kufuata
Mkutano mkuu wa Oktoba 2023


Mnyenyekevu Kukubali na Kufuata

Unyenyekevu ni hitaji la lazima kwetu ili kuwa tayari kurudi katika uwepo wa Mungu.

Katika mlango wa tano wa Alma, swali la kujichunguza limeulizwa: “Mngeweza kusema, kama mngeitwa kufariki wakati huu, ndani yenu, kwamba mlikuwa wanyenyekevu wa kutosha?”1 Swahi hilo linamaanisha kwamba unyenyekevu ni hitaji la lazima kwetu kuwa tayari kurudi katika uwepo wa Mungu.

Sote tunapenda kufikiria kuwa tu wanyenyekevu vya kutosha, lakini baadhi ya uzoefu katika maisha unatufanya tutambue kuwa mtu yule wa asili mwenye kiburi mara kwa mara yuko hai ndani yetu.

Miaka kadhaa iliyopita, wakati mabinti zetu wawili walipokuwa bado wanaishi nyumbani, niliamua kuwaonyesha wao na mke wangu biashara ambayo mimi nilikuwa nikiisimamia katika kampuni ambayo nilikuwa nikifanyia kazi.

Dhumuni langu hasa lilikuwa kuwaonyesha mahali ambapo, tofauti na nyumbani kwetu, kila mtu atafanya kile nitakachowaambia wafanye bila kuniuliza maswali. Tulipofika tu lango la mbele, ambalo kwa kawaida linafunguka lenyewe gari langu linapokuwa likikaribia, nilishangaa kwamba halikufunguka wakati huu. Badala yake, mlinzi ambaye kamwe sijapata kumwona hapo kabla alikuja kwenye gari na akaniomba kitambulisho cha kampuni yangu.

Nilimwambia mimi sihitaji kitambulisho kuingia ndani ya jengo hilo na gari langu na kisha nikamuuliza swali moja la kiburi cha hali ya juu: “Unajua unaongea na nani?”

Ambapo alijibu, “Vyema, kwa vile hauna kitambulisho cha kampuni siwezi kujua wewe ni nani, na wakati ninapokuwa hapa langoni hautaruhusiwa kuingia humu ndani pasipo kuwa na kitambulisho sahihi.”

Nilitafakari huku nikiangalia kioo cha kutazama nyuma ya gari ili kuona mabinti zangu wanafanya nini juu ya hilo, lakini nilijua mabinti zangu walikuwa wakifurahia kila sekunde ya wakati ule! Mke wangu akiwa pembeni yangu alitikisa kichwa chake katika kutoridhika na tabia yangu. Hoja yangu ya mwisho basi ilikuwa kuomba radhi kwa mlinzi na kusema nisamehe kwa kumjibu vibaya sana. “Umesamehewa,” yeye alisema, “lakini bila kitambulisho cha kampuni, huwezi kuingia ndani leo!”

Kisha nikaendesha gari pole pole kuelekea nyumbani kuchukua kitambulisho, nikiwa nimejifunza somo hili la thamani: tunapochagua kutokuwa wanyenyekevu, tunaishia kudharaulika.

Katika methali tunaona, “Kiburi cha mtu kitamshusha: bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa.”2 Ili kukuza unyenyekevu, lazima tuelewe ina maana gani hasa katika muktadha wa injili.

Baadhi ya watu wanachanganya kuwa mnyenyekevu na vitu vingine kama vile, kwa mfano, kuwa maskini. Lakini kwa kweli kuna wengi walio maskini na ni wenye kiburi na pia wengi walio matajiri na ni wanyenyekevu. Baadhi walio na haya sana au wasiojiamini yawezekana kwa muonekano wa nje ni wanyenyekevu lakini ndani wamejaa kiburi.

Basi unyenyekevu ni nini? Kulingana na Hubiri Injili Yangu, ni “utayari wa kujiweka chini ya mapenzi ya Bwana. … Ni kuwa mwenye kuweza kufundishika. … [Ni] kichocheo muhimu cha ukuaji wa kiroho.”3

Kuna fursa nyingi za uhakika kwa ajili yetu sote za kuboreka katika sifa hii kama ya Kristo. Ningependa kufafanua kwanza jinsi gani tulivyo wanyenyekevu, au tunapaswa kuwa, katika kufuata ushauri wa nabii wetu. Chemsha bongo kwa kila mmoja ingeweza kuwa:

  • Je, tunalitaja jina kamili la Kanisa katika kuchangamana kwetu kote? Rais Russell M. Nelson alisema, “Kuliondoa jina la Bwana kutoka katika Kanisa la Bwana ni ushindi mkubwa kwa Shetani.”4

  • Je, tunamruhusu Mungu ashinde katika maisha yetu kwa kukubali mwaliko maalumu wa nabiii wetu? “Leo ninawaomba waumini wetu kila mahali kuongoza katika kuachana na mitazamo na matendo ya kibaguzi.”5

  • Je, sisi tunaushinda ulimwengu, tukitumainia mafundisho ya Kristo kuliko falsafa za wanadamu, kama manabii wetu walivyofundisha?6

  • Je, sisi tumekuwa wapatanishi, tukisema mambo chanya kwa watu na kuhusu watu? Rais Nelson katika mkutano mkuu uliopita alitufundisha yafuatayo: “Kama kuna kitu chochote kilicho chema, chenye kupendeza, au chenye taarifa njema au chenye kustahili sifa ambacho tunaweza kusema kuhusu mtu mwingine—mbele yake au bila uwepo wake—kinapaswa kiwe msingi wa mawasiliano yetu7

Haya maelekezo ni rahisi lakini ni yenye nguvu zaidi. Kumbuka, watu wote wa Musa walichopaswa kufanya ili waponywe ilikuwa kumtazama nyoka wa shaba ambaye Musa alimwinua juu.8 Lakini “kwa sababu ya urahisi wa njia, au wepesi wake, kulikuwa na wengi walio angamia.”9

Wakati wa mkutano huu tumesikia na bado tutasikia ushauri usioshindwa wa manabii na mitume wetu. Ni tukio sahihi la kukuza unyenyekevu na kuacha maoni yetu imara yamezwe na sadikisho imara zaidi kwamba Bwana ananena kupitia viongozi hawa wateule.

Juu ya yote, katika kukuza unyenyekevu ni lazima pia tuelewe na kukubali kwamba hatuwezi kushinda changamoto zetu au kupata uwezekano wetu mkamilifu kupitia jitihada zetu wenyewe pekee. Wazungumzaji wahamasishaji, waandishi, makocha na wavutiaji ulimwenguni kote, hususani katika jukwaa la kidigitali, watasema kwamba kila kitu kinatutegemea sisi pekee na matendo yetu. Ulimwengu unaamini katika mkono wa mwanadamu;

Lakini kupitia injili ya urejesho, tumejifunza kwamba kwa sehemu kubwa tunategemea ukarimu wa Baba wa Mbinguni na Upatanisho wa Mwokozi wetu Yesu Kristo “kwani tunajua kwamba ni kwa neema kwamba tunaokolewa, baada ya kufanya yote tunayoweza kufanya.”10 Hiyo ndiyo sababu ni muhimu kufanya na kushika maagano na Mungu, kwa vile kufanya hivyo kutatupa sisi ufikiaji kamili kwenye uponyaji, uwezeshaji na nguvu ya ukamilishaji ya Yesu Kristo kupitia Upatanisho Wake.

Kuhudhuria mkutano wa sakramenti kila wiki na kuabudu hekaluni mara kwa mara ili kushiriki katika ibada na kupokea na kufanya upya maagano ni ishara kwamba tunatambua utegemezi wetu kwa Baba wa Mbinguni na Mwokozi wetu Yesu Kristo. Hiyo itaalika nguvu zao katika maisha yetu ili itusaidie kuvuka matatizo yetu yote na mwishowe kutimiza kipimo cha kuumbwa kwetu.

Siyo zamani sana kiwango cha unyenyekevu na uelewa wangu juu ya utegemezi wangu kwa Bwana kwa mara nyingine unajaribiwa tena. Nilikuwa ndani ya teksi nikienda uwanja wa ndege kwenda safari fupi kwa ndege mahali ambako kulikuwa na hali ngumu ya kutatua. Dereva wa teksi, ambaye hakuwa muumini wa Kanisa, aliniangalia kupitia kioo cha kutazama nyuma cha gari na kusema, “naweza kuona hauko sawa leo!”

“Umejuaje?” Niliuliza.

“Ndiyo,” alisema. Kisha akasema kitu fulani kama, “Kwa kweli una mawazo hasi yamekuzunguka!”

Nilimwelezea nilikuwa na hali ngumu ya kuishughulikia, na kisha akaniuliza, “Je, umefanya kila kitu kilicho ndani ya uwezo wako katika kutatua hili?”

Nilijibu kwamba nimefanya kila kitu ambacho ningeweza.

Kisha akasema jambo ambalo kamwe sijalisahau, “Basi liache hili katika mikono ya Mungu, na kila kitu kitakuwa sawa.”

Naungama kwamba nilishawishika kumwuliza, “Je, unajua unaongea na nani?” “Lakini sikufanya hivyo! Nilichokifanya ni kuwa mnyenyekevu mimi mwenyewe mbele za Bwana wakati wote wa safari ile ya ndege ya saa moja, nikiomba msaada wa kiungu. Nilipoondoka kwenye ile ndege, nilijua kwamba ile hali ngumu ya kutatuliwa tayari ilikuwa imekaa sawa na kwamba uwepo wangu hata haungekuwa muhimu tena.

Akina kaka na akina dada, amri, mwaliko na ahadi kutoka kwa Bwana ni wazi na ni wa kufariji: “Jinyenyekeze; na Bwana Mungu wako atakuongoza kwa mkono, na kukupa jibu la sala zako.”11

Na tuwe wanyenyekevu ili kufuata ushauri wa manabii na kukubali kwamba ni Mungu pekee na Yesu Kristo ndio wanaoweza kutubadilisha sisi—kupitia ibada na maagano yanayopokelewa katika Kanisa Lake—katika toleo letu wenyewe bora katika maisha haya na, siku moja, yatufanye kuwa wakamilifu katika Kristo. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Chapisha