Mkutano Mkuu
Bwana, Tungependa Kumwona Yesu
Mkutano mkuu wa Oktoba 2023


Bwana, Tungependa Kumwona Yesu

Sisi tunataka kumwona Yesu jinsi Yeye alivyo na kuhisi upendo Wake.

Upofu wa Kutambua Uso

Siku moja katika majira ya kuchipua ya 1945, kijana mmoja aliamka katika hospitali ya kijeshi. Alikuwa na bahati ya kuwa hai—alikuwa amepigwa risasi nyuma ya sikio, lakini madaktari walimfanyia upasuaji, na sasa angeweza kutembea na kuzungumza kawaida.

Kwa bahati mbaya, risasi hiyo iliharibu sehemu ya ubongo wake uliotambua nyuso. Sasa anamtazama mkewe bila chembe ya utambuzi; hakuweza kumtambua mama yake mwenyewe. Hata sura kwenye kioo ilikuwa ngeni kwake—hakuweza kujua ikiwa ni ya mwanaume au mwanamke.1

Amekuwa kipofu wa kutambua nyuso—hali inayoathiri mamilioni ya watu.2

Watu ambao wana upofu wa kutambua uso hujaribu kuwatambua wengine kwa kukariri sheria—sheria ya kumtambua binti kwa kovu lake au rafiki kwa mtembeo wa kuburuza miguu.

Kukua

Hapa kuna hadithi ya pili, karibu na nyumbani: Kama mvulana mdogo, mara nyingi nilimwona mama yangu kama mtunga sheria. Aliamua wakati ningeweza kucheza na wakati gani kwenda kulala au, vibaya zaidi, kuondoa magugu kwenye uwanja.

Ni wazi yeye alinipenda. Lakini mara nyingi sana na kwa aibu yangu, nilimwona tu kuwa “Yeye Ambaye Ni Lazima Atiiwe.”

Miaka kadhaa baadaye ndipo nilipomwona kama mtu halisi. Nina aibu kusema kwamba kamwe sikuwahi kutambua dhabihu yake au kujiuliza ni kwa nini kwa miaka mingi aliweza kuvaa sketi zile zile mbili kuu kuu (huku mimi nikipata nguo mpya za shule) au kwa nini, baada ya siku kwisha, alichoka sana na alitaka nilale mapema.

Tunaweza Kuwa Vipofu wa Kutambua Uso

Labda umegundua kwamba hadithi hizi mbili kwa kweli ni hadithi moja—kwa miaka mingi sana, nilikuwa na upofu wa kutambua uso. Nilishindwa kumuona mama yangu kama mtu halisi. Niliona sheria zake lakini sikuziona katika upendo wake.

Ninakuambia hadithi hizi mbili ili kutoa hoja moja: ninashuku kwamba unamfahamu mtu fulani (labda ni wewe ndiyo huyo mtu) ambaye anaugua aina fulani ya upofu wa utambuzi wa uso wa kiroho.

Unaweza kusumbuka kumwona Mungu kama Baba mwenye upendo. Unaweza kutazama mbinguni na kuona sio uso wa upendo na rehema lakini mzigo wa sheria ambazo lazima zipitie njia yako. Labda unaamini kwamba Mungu anatawala katika mbingu Zake, anazungumza kupitia manabii Wake na anampenda dada yako, lakini kwa siri unashangaa kama anakupenda wewe.3 Labda umehisi fimbo ya chuma katika mkono wako lakini bado hujahisi Upendo wa Mwokozi wako unaelekea wapi.4

Nadhani mnawajua watu kama hawa kwa sababu kwa muda mrefu, nilikuwa mtu kama huyu—nilikuwa na upofu wa uso wa kiroho.

Nilidhani maisha yangu yalikuwa kufuata tu sheria na kujilinganisha na viwango vya dhahania. Nilijua Mungu alikupenda wewe kikamilifu lakini binafsi sikuhisi hilo. Nina hofu kwamba niliwaza zaidi kufika mbinguni kuliko kuwa na Baba yangu wa Mbinguni.

Ikiwa wewe, kama mimi, wakati mwingine unachezesha midomo tu lakini “huimbi wimbo wa upendo wa ukombozi,”5 tunaweza kufanya nini?

Jibu, kama Rais Russell M. Nelson anavyotukumbusha, daima ni Yesu.6 Na hiyo ni habari nzuri sana.

Bwana, Tungependa Kumwona Yesu

Kuna mstari mfupi katika Yohana ambao ninaupenda. Mstari unasimulia juu ya kundi la wayunani wanaomwendea mwanafunzi wa Yesu wakiwa na ombi muhimu. “Bwana,” wanasema, “sisi [tungependa] kumwona Yesu.”7

Hilo ndilo sote tunalotaka—tunataka kumwona Yesu jinsi Yeye alivyo na kuhisi upendo Wake. Hii inapaswa kuwa sababu ya karibu kila kitu tunachofanya kanisani—na hasa katika kila mkutano wa sakramenti. Ikiwa unajiuliza ni aina gani ya somo la kufundisha, ni aina gani ya mkutano wa kupanga na kama ukate tamaa juu ya mashemasi na kucheza mpira wa kukwepa, unaweza kuchukua mstari huu kama mwongozo wako: je, hii itasaidia watu kumwona na kumpenda Yesu Kristo? Na kama sio, basi jaribu kitu kingine.

Nilipotambua kwamba nilikuwa na upofu wa uso wa kiroho, kwamba niliona sheria na sio uso wa neema ya Baba, nilijua hili halikuwa tatizo la Kanisa. Wala si la Mungu, na haikumaanisha kila kitu kilipotea; ni jambo ambalo sisi sote tunapaswa kujifunza. Hata mashahidi wa mwanzo wa Ufufuko mara nyingi walikutana uso kwa uso na Bwana aliyefufuka na lakini hawakumtambua; kutoka Kaburi la Bustanini mpaka pwani ya Galilaya, wafuasi Wake wa kwanza “walimwona Yesu amesimama, wala hawakujua ya kuwa ni Yesu.”8 Ilibidi wajifunze kumtambua Yeye, nasi vivyo hivyo.9

Hisani

Nilipotambua nilikuwa mpofu kiroho nilianza kufuata ushauri wa Mormoni wa kuomba “kwa nguvu zote za moyo” ili kujazwa na upendo ulioahidiwa kwa wafuasi Wake—upendo wangu Kwake na upendo Wake kwangu—na “kumwona jinsi alivyo … na kuwa na tumaini hili.”10 Niliomba kwa miaka mingi ili kuweza kufuata amri kuu ya kwanza ya kumpenda Mungu na kuhisi kwamba “ukweli ukweli mkuu wa kwanza … ni kwamba Mungu anatupenda sisi kwa moyo Wake wote, nguvu, akili na uwezo.”11

Injili

Pia nilisoma na kusoma tena na kusoma tena Injili kuu nne—wakati huu haikuwa kwa ajili ya kudondoa sheria Zake bali kuona Yeye ni nani na kipi Yeye hukipenda. Na, punde, nilisombwa na mto wa upendo uliotiririka kutoka Kwake.

Yesu alitangaza mwanzoni, kwamba Yeye alikuja “kuwaponya waliovunjika moyo, kuwatangazia wafungwa uhuru wao, na vipofu kupata kuona tena.”12

Hiyo haikuwa tu orodha ya mambo ya kufanya au mahusiano mazuri ya umma; ndiyo umbo la upendo Wake.

Fungua Injili bila mpangilio; karibu katika kila ukurasa tunamwona Yeye akiwatunza watu wanaoteseka—kijamii, kiroho, na kimwili. Aliwagusa watu waliochukuliwa kuwa najisi na wasio wasafi13 na kuwalisha wenye njaa.14

Ni hadithi gani pendwa kwako kuhusu Yesu Kristo? Nadhania inamuonyesha Mwana wa Mungu akinyoosha mkono kumkumbatia au kutoa tumaini kwa mtu mnyonge—mkoma,15 Msamaria anayechukiwa,16 mwenye dhambi aliyetuhumiwa na mwenye kashfa,17 au adui wa taifa.18 Rehema ya aina hiyo inashangaza.

Jaribu kuandika kila wakati Yeye anaposifia au kuponya au kula na mtu wa nje, na utapungukiwa na wino kabla ya kumaliza kitabu cha Luka.

Nilipoona hili, moyo wangu uliruka katika utambuzi wa upendo, na nikaanza kuhisi kwamba Yeye angeweza kunipenda. Kama vile Rais Nelson alivyofundisha, “Kadri unavyojifunza zaidi juu ya Mwokozi, ndivyo itakavyokuwa rahisi kutumaini rehema Yake, upendo Wake usio na kikomo.”19 Na ndivyo utakavyomwamini na kumpenda zaidi Baba yako wa Mbinguni.

Mzee Holland ametufundisha kwamba Yesu alikuja kutuonyesha “Mungu Baba yetu wa Milele ni nani na yuko vipi, jinsi Yeye alivyojitoa kikamilifu kwa watoto Wake katika kila umri na taifa.”21

Paulo alisema Mungu ni “Baba wa rehema [zote], na Mungu wa faraja yote.”21

Kama unamwona Yeye kwa njia tofauti, tafadhali endelea kujaribu.

Maagano na Kumbatio la Mungu

Manabii hutualika kutafuta uso Wake.22 Ninachukulia hili kama ukumbusho kwamba tunamwabudu Baba yetu, sio kanuni, na kwamba hatufiki tamati mpaka tumwone Yesu kama uso wa upendo wa Baba yetu;23 na tumfuate Yeye, si tu amri Zake.24

Wakati manabii na mitume wanapozungumza kuhusu maagano, wao si kama makocha wanaopiga kelele kutoka benchini, wakituambia “tujaribu zaidi!” Wanatutaka sisi tuone maagano yetu kimsingi ni kuhusu mahusiano25 na yanaweza kuwa tiba ya upofu wa uso wa kiroho.26 Sio sheria za kupata upendo Wake; Yeye tayari anakupenda kikamilifu. Changamoto yetu ni kuelewa na kuyafinyanga maisha yetu kuwa upendo huo.27

Tunajaribu kuona kupitia maagano yetu, kama vile dirishani, kwenye uso nyuma ya rehema ya Baba.

Maagano ndiyo umbo la kumbatio la Mungu.

Mto wa Upendo wa Mungu

Hatimaye, tunaweza kujifunza kwa kumwona Yeye kwa kumtumikia Yeye. “Kwani mtu awezaje kumjua bwana ambaye hajamtumikia?”28

Miaka michache iliyopita, nilipata wito ambao sikuufurahia. Niliamka mapema, nikiwa na wasiwasi—lakini nikiwa na msemo akilini ambao sikuwahi kuusikia hapo awali: kwamba kuhudumu katika Kanisa hili ni kusimama katika mto wa upendo wa Mungu kwa watoto Wake. Kanisa hili ni jamii ya watu wachapakazi wenye sururu na sepeto, wakijaribu kusaidia kusafisha njia ya mto wa upendo wa Mungu kuwafikia watoto Wake mwishoni mwa mstari.

Bila kujali wewe ni nani, jana yako, kuna nafasi yako katika Kanisa hili.29

Chukua sururu na sepeto na ujiunge na timu. Saidia kubeba upendo Wake kwa watoto Wake na baadhi ya upendo huo utarejea kwako.30

Na tutafute uso Wake wa upendo, kumbatio Lake la agano, na kisha kuungana mkono kwa mkono na watoto Wake, na kwa pamoja tutaimba “Mkombozi wa Israeli”:

Nirejeshee, Mwokozi

Nuru yako;

Faraja ya roho nipe;

Na ile shauku

ya kuja kwako

Moyo tumaini iipe.31

Na tutafute uso Wake wa upendo na tuwe vyombo vya rehema Zake kwa watoto Wake.32 Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona Hadyn D. Ellis and Melanie Florence, “Bodamer’s (1947) Paper on Prosopagnosia,” Cognitive Neuropsychology, vol. 7, no. 2 (1990), 84–91; Joshua Davis, “Face Blind,” Wired, Nov. 1, 2006, wired.com.

  2. Ona Dennis Nealon, “How Common Is Face Blindness?,” Harvard Medical School, Feb. 24, 2023, hms.harvard.edu; see also Oliver Sacks, “Face-Blind,” The New Yorker, Aug. 23, 2010, newyorker.com.

  3. “Baadhi ya waumini wa Kanisa wanakubali mafundisho, kanuni na shuhuda zitolewazo mara kwa mara kutoka mimbari hii katika Ukumbi wa Mikutano Mkuu na mikusayiko katika maeneo yote ulimwenguni kuwa ni kweli—na bado wanahangaika kuamini kweli hizi za milele kwamba hutumika katika maisha yao na katika hali zao” (David A. Bednar, “Kaa Ndani Yangu, Nami Ndani Yako,” Liahona, Mei 2023)

  4. Ona 1 Nefi 8:19; 15:23. “Ni vigumu kushika amri za Bwana bila imani na tumaini Kwake” (Henry B. Eyring, “Imani ya Kuuliza na Kisha Kutenda,” Liahona, Nov. 2021).

  5. Alma 5:26.

  6. Russell M. Nelson, “Jibu Daima Ni Yesu Kristo,” Liahona, Mei 2023.

  7. Yohana 12:21.

  8. Yohana 20:14. Waliona lakini hawakumjua akiwa njiani kuelekea Emau (Ona Luka 24:16), katika chumba kilichofungwa (ona Luka 24:37), katika ufukwe wa Galilaya (ona Yohana 21:4), na katika Kaburi la Bustanini (ona Yohana 20:14).

  9. Kama tukimtafuta kwa moyo wetu wote na kuendelea kwa imani, Yeye atapatikana.

    “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, mawazo ya amani na siyo uovu. …

    Na mtanitafuta mimi, na mtanipata, pale mtakaponitafuta” (Yeremia 29:11, 13).

    “Siku itakuja mtakayomjua Mungu, mkiwa mmehuishwa ndani yake na yeye mwenyewe.

    Ndipo mtakapojua ya kuwa mmeniona, ya kuwa mimi ndiye” (Mafundisho na Maagano 88:49–50).

    “Kila mtu atakayeziacha dhambi zake na kuja kwangu, na kulilingana jina langu, na kuitii sauti yangu, na kushika amri zangu, atauona uso wangu na kujua kuwa Mimi Ndimi.” (Mafundisho na Maagano 93:1)

  10. Moroni 7:48. Paulo pia anaunganisha hisani na uwezo wetu wa kuona vizuri. Katika hitimisho la mahubiri yake makuu kuhusu hisani, anaandika kwamba ingawa “wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo,” baadaye tutaona “uso kwa uso: … nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.” (1 Wakorintho 13:12).

  11. Jeffrey R. Holland, “Kesho Bwana Atafanya Miujiza Miongoni Mwenu,” Liahona,, Mei 2016, 127. “Maelezo makuu ya ‘upendo msafi wa Kristo,’… si kama kile ambacho sisi kama Wakristo hujaribu lakini hushindwa kabisa kuonyesha kwa wengine bali ni kile chote ambacho Kristo alifanikiwa kuonyesha kwetu sisi. Hisani ya Kweli imejulikana mara moja tu. Inaonyeshwa kikamilifu na kwa usafi katika upendo wa Kristo usioshindwa, wa mwisho na wa upatanisho kwa ajili yetu” (Jeffrey R. Holland, Christ and the New Covenant: The Messianic Message of the Book of Mormon [1997], 336).

  12. Luka 4:18, Toleo Jipya la King James.

  13. Ona Mathayo 8:3; 9:25.

  14. Ona Mathayo 14:13–21.

  15. Ona Matthayo 8:1–3.

  16. Ona Yohana 4:7–10; Yeye alimsifia Msamaria (ona Luka 10:25–37).

  17. Ona Matthayo 21:31; Luka 7:27–50; 15:1–10; Yohana 8:2–12.

  18. Ona Mathayo 8:5–13.

  19. Russell M. Nelson, “Kristo Amefufuka; Imani Kwake Itahamisha Milima,” Liahona, Mei 2021, 103.

  20. Jeffrey R. Holland, “The Grandeur of God,” Liahona, Nov. 2003, 70. ”Aliyeniona mimi amemwona Baba” (Yohana 14:9).

  21. 2 Wakorintho 1:3.

  22. Ona Zaburi 27:8; Mafundisho na Maagano 88:68.

  23. Ona 2 Wakorintho 4:6; Pope Francis, “Misericordiae Vultus: Bull of Indiction of the Extraordinary Jubilee of Mercy,” Apostolic Letters, vatican.va.

  24. Hii ni dhima muhimu. Siyo tu ile kazi ya wokovu na kutukuka bali kazi Yake ya wokovu na kuinuliwa (ona Kitabu cha Maelezo ya Jumla: Kuhudumu katika Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, 1.2, Maktaba wa Injili). Siendi tu hekaluni lakini kwenye nyumba ya Bwana; si Kanisa la Mormoni bali Kanisa la Yesu Kristo (ona Russell M. Nelson, “Jina Sahihi la Kanisa,” LiahonaLiahona, Nov. 2018, 87–89). Viongozi wetu hutuelekeza Kwake na hata kutukumbusha kwamba “hakuna taasisi maalum inayoitwa ‘Upatanisho’ ambayo kwayo tunaweza kuomba msaada, uponyaji, msamaha au nguvu. Yesu Kristo ndiye chanzo” (Russell M. Nelson, “Kuvuta Nguvu ya Yesu Kristo kwenye Maisha Yetu,” Liahona, Mei 2017).

  25. “Njia ya agano inahusu uhusiano wetu na Mungu”; ni “njia ya upendo— … kujaliana kwa huruma na kufikiana” (Russell M. Nelson, “Agano la Milele,” Liahona, Okt. 2022, 11).

    Ona David A. Bednar, “The Blessed and Happy State” (address given at the seminar for new mission leaders, June 24, 2022); Scott Taylor, “Elder Bednar Shares 7 Lessons on ‘the Blessed and Happy State’ of Obedience,” Church News, June 27, 2022, thechurchnews.com.

    “Kuingia katika maagano matakatifu na kwa kustahili kupokea ibada za ukuhani kunatufunga nira sisi pamoja na kutuunganisha na Bwana Yesu Kristo na Baba wa Mbinguni. Hii kwa urahisi kabisa inamaanisha kwamba tunatumaini katika Mwokozi kama Mwombezi wetu na Mpatanishi na tunategemea wema Wake, rehema na neema wakati wa safari yetu ya maisha. …

    Msimamo wa kuishi na kupenda maagano hujenga uhusiano na Bwana ambao ni wa kina na wa kipekee na ambao unakuwa na nguvu kiroho. Kisha Yesu anakuja kuwa zaidi ya mhusika mkuu katika hadithi za maandiko; mifano Yake na mafundisho Yake yanashawishi kila hamu, wazo na tendo letu,” (David A. Bednar, “Lakini Hatukuwasikiliza,” Liahona, Mei 2022, 15).

    Ona pia D. Todd Christofferson, “Uhusiano Wetu na Mungu,” Liahona, Mei 2022, 78.

  26. “Na pasipo ibada hizo, na mamlaka ya ukuhani, nguvu za uchamungu haziwezi kujidhihirisha kwa mwanadamu katika mwili;

    “Kwani pasipo hizi hakuna mwanadamu anayeweza kuuona uso wa Mungu, hata Baba, na kuishi” (Mafundisho na Maagano 84:21–22).

  27. Patricia Holland, “A Future Filled with Hope” (worldwide devotional for young adults, Jan. 8, 2023), Gospel Library:

    “Hupaswi kuhangaika ukitafuta [tumaini kwamba Yeye atakusaidia]; hupaswi na huwezi kulizalisha tumaini hilo. Kama vile wengi kwenye mzunguko wa rehema, huwezi kuipata kwa kutegemea nguvu yako mwenyewe au ya mwingine. Hakuna kanuni za siri au mbinu za kiinimacho zinazohusika. …

    “Kwa kweli, nafasi tunayofanya ni muhimu lakini ni ndogo sana; Mungu anayo sehemu kubwa ya kazi. Jukumu letu ni kusonga Kwake katika unyenyekevu na urahisi, kisha hatupaswi kutia shaka na kuogopa.”

  28. Mosia 5:13; ona pia Alma 17:3.

  29. Rais Nelson ametuita mara kwa mara “kupanua mzunguko wetu wa upendo ili kukumbatia familia nzima ya binadamu” (“Heri Wapatanishi,” Liahona, Mei 2002, 41). Mnamo Mei 2022 aliwaambia vijana kwamba “utani unaweza kusababisha hukumu na chuki. Iwe Unyanyasaji wowote au ubaguzi juu ya mwingine kwa sababu ya utaifa, rangi, mtazamo wa kijinsia, jinsi, shahada za elimu, utamaduni au utambulisho mwingine ni chukizo kwa Muumba wetu” (“Choices for Eternity” [worldwide devotional for young adults, May 15, 2022], Gospel Library). Na muhimu zaidi, alisema: “Ninahuzunika kwamba kaka na dada zetu weusi ulimwenguni kote wanavumilia machungu ya ubaguzi wa rangi na chuki. Leo ninatoa wito kwa waumini wetu kila mahali kuwa mfano katika kuacha mitazamo na matendo ya chuki. Ninawasihi muhamasishe heshima kwa watoto wote wa Mungu” (“Acha Mungu Ashide,” Liahona, Nov. 2020).

    “Chuki haipatani na neno la Mungu lililofunuliwa. Kupendelewa au kutokupendelewa na Mungu kunategemea msimamo wetu Kwake na kwenye amri zake, siyo kwenye rangi ya ngozi ya mtu au sifa zingine.

    “… Hii inajumuisha chuki ihusianayo na mbari, utaifa, kabila, jinsi, umri, ulemavu, hadhi ya kiuchumi na kijamii, imani za dini au kutoamini na utambulisho wa kijinsia” (Kitabu cha Maelezo ya Jumla, 38.6.14, Maktaba ya Injili).

  30. Ona 1 Nefi 11:25.

  31. Mwokozi wa Israeli,” Nyimbo za Dini, na. 6.

  32. Ona Warumi 9:23.

Chapisha