Mkutano Mkuu
Imani ya kutenda na Kuwa
Mkutano Mkuu wa Oktoba 2021


Imani ya kutenda na Kuwa

Kupitia sala, na kujifunza maandiko, na kutenda, tunaweza kufungua baraka za mbinguni na kuwa wafuasi bora wa Mwokozi Yesu Kristo.

Muda mfupi baada ya kuitwa kutumikia kwenye akidi ya Sabini, nilipata nafasi ya kumtembelea Rais Russell M. Nelson kwa dakika chache. lilikuwa si tukio la kupangwa katika mgahawani, na alikuwa mwema sana kumualika Mzee S. Mark Palmer pamoja na mimi kukaa na kufurahia chakula cha mchana pamoja naye.

“Tunazungumza nini wakati wa chakula cha mchana na nabii?” lilikuwa wazo lililokuja akilini mwangu. Kwa hivyo niliamua kumuuliza Rais Nelson ikiwa alikuwa na ushauri au mwongozo wowote kwangu kwani nilikuwa naanza wito wangu. Jibu lake lilikuwa rahisi sana na la moja kwa moja; aliniangalia na kusema, “Mzee Schmeil, umeitwa kwa kile unachoweza kuwa.” Kutoka kwenye uzoefu huo nilitafakari kwa kina juu ya kile Bwana anataka niwe. Wakati nikifikiria juu ya hili, niligundua kuwa Ananitaka niwe mume bora, baba bora, na mwana na mtumishi bora. Ndipo nikagundua kuwa haya yote yanaweza kutimizwa wakati nikifanyia kazi kuwa mwanafunzi bora wa Mwokozi Yesu Kristo.

Mkutano mkuu uliopita, Rais Nelson alisema: “Kufanya jambo lolote vizuri kunahitaji juhudi. Kuwa mfuasi wa kweli wa Yesu Kristo huitaji hilo.”1 Rais Nelson anatualika tufanye bidii kuwa wafuasi bora wa Yesu Kristo. Alituambia kuwa ili zaidi kuwa kama Mwokozi, tunahitaji kuimarisha imani yetu kwa kuuliza, kutenda, na kujifunza, ikiwa ni sehemu ya mambo kadhaa.

1. Uliza

Alisema, “Muombe Baba yako wa Mbinguni, katika jina la Yesu Kristo, kwa ajili ya msaada.”2 Kuuliza kupitia sala ni moja ya funguo za kujua jinsi ya kuwa mfuasi bora wa Yesu Kristo.

Kuelekea mwisho wa huduma Yake kwa Wanefi katika Amerika, Yesu Kristo Alipaa kwenda mbinguni. Baadaye, wanafunzi Wake walikusanyika pamoja, “wakiwa wameungana katika sala yenye nguvu na kufunga. Na Yesu tena alijidhihirisha kwao, kwani walikuwa wanaomba kwa Baba katika jina lake.”3 Kwa nini Yesu Kristo aliamua kujionyesha tena kwa wafuasi wake? Kwa sababu walikuwa wanasali; walikuwa wanaomba

Kisha aliendelea:

“Sasa naenda kwa Baba. Na amin, nawaambia, vitu vyovyote mtakavyomuuliza Baba katika jina langu, vitatolewa kwenu.

“Kwa hivyo, ombeni na mtapokea; bisheni na mtafunguliwa; kwani yule ambaye huuliza hupokea; na kwa yule ambaye hubisha, itafunguliwa.”4

Tunahitaji kuomba kwa imani ili kujua mapenzi ya Bwana, na tukubali kwamba Bwana anajua kilicho bora kwetu.

2. Tenda

Kutenda ni ufunguo mwingine muhimu wa kuwa mwanafunzi bora wa Yesu Kristo. Tunapotenda, Yeye atatuongoza na kutuonyesha njia. Nina hakika kwamba Nefi alikuwa akitafuta mwongozo kutoka kwa Bwana kujua jinsi ya kupata mabamba ya shaba kutoka kwa Labani, hata hivyo yeye na kaka zake walijaribu mara mbili bila mafanikio. Lakini walikuwa wakifanya kazi, na Bwana alikuwa akiwaongoza njiani. Hatimaye, mara ya tatu, Nefi alifanikiwa mara ya tatu. Alikumbuka, “Niliongozwa na Roho, bila kujua mapema mambo ambayo nilipaswa kufanya.”5

Hivi ndivyo Bwana anavyofanya kazi tunapojitahidi na kutenda, hata wakati hatuna uelewa kamili wa nini kinapaswa kufanywa. Bwana alimwambia Nefi kipi cha kufanya: nenda na chukua bamba. Lakini hakumuambia Nefi ni kwa namna ipi angefanya. Alimwachia Nefi kujua na kutafuta msaada wa Bwana—na hivi ndivyo mara nyingi Bwana hufanya kazi katika maisha yetu. Tunapotenda kwa imani, Bwana anatuongoza na kutuelekeza.

3. Jifunze

Katika Nefi 3, wanafunzi walimwambia Mwokozi kwamba kulikuwa na mabishano kati ya watu kuhusu jina la Kanisa. Kwa kujibu, Mwokozi alifundisha kanuni muhimu alipouliza, “Je! Hawajasoma maandiko?”6 Kusoma basi ni ufunguo mwingine muhimu wa kuwa mwanafunzi bora wa Yesu Kristo. Sala na kujifunza maandiko huenda sambamba. Hufanya kazi pamoja kwa faida yetu. Huu ndio mchakato ambao Bwana ameanzisha. “Shiriki maneno ya Kristo; kwani tazama, maneno ya Kristo yatawaelezea vitu vyote mnavyostahili kutenda.”7

Mwokozi pia alifundisha kwamba hatupaswi tu kujifunza maandiko lakini pia kufundisha kutoka kwayo, kama alivyoonyesha kwa Wanefi: “Na ikawa kwamba wakati Yesu alikuwa ameelezea maandiko yote, ambayo walikuwa wameandika, aliamuru wao kwamba wanapaswa kufundisha mambo ambayo alikuwa amewaelezea.”8

Hii ni moja ya sababu kwa nini ilikuwa muhimu sana kwa Nefi kurudi kuchukua bamba za shaba: familia yake ilihitaji maandiko sio tu kuwasaidia kusafiri kwenda nchi ya ahadi lakini pia kuwasaidia kufundisha watoto wao. Sisi pia lazima tutafute mwongozo kutoka kwenye maandiko kwa ajili ya safari yetu, na lazima tufundishe kutoka kwayo katika nyumba zetu na kwenye miito ya Kanisa.

4. Tenda ili Kuwa

Mara nyingi majibu ya maombi hayatakuja mara moja. Lakini lazima tuwe na imani ya kuendelea, kutenda kwa haki, na kuwa wa kudumu kama Nefi wakati alipokuwa akijaribu kupata mabamba ya shaba. Bwana atatuonyesha kwa ufupi wakati fulani; wakati tunapojifunza maandiko, Bwana atatupa majibu au nguvu zinazohitajika katika siku moja zaidi, wiki moja zaidi, na za kujaribu mara moja zaidi. Mzee Richard G. Scott alisema: “Shukuru kwamba wakati mwingine Mungu hukuruhusu upambane kwa muda mrefu kabla ya jibu hilo kuja. Hiyo inasababisha imani yako kuongezeka na tabia yako kukua.”9

Kupitia sala na kujifunza maandiko, Bwana daima amenipa nguvu ya kutenda na kuvumilia siku moja zaidi, wiki moja zaidi, na kujaribu tena. Mara nyingi, majibu hayakuja papo hapo. Nina maswali ambayo hayajajibiwa bado, lakini ninaendelea kuuliza na kusoma, na ninafurahi kwamba Bwana anaendelea kunipa nguvu ya kutenda wakati ninasubiri majibu.

Mzee Scott pia alisema, “Unapotembea mpaka kwenye ukingo wa ufahamu wako katika machweo ya kutokuwa na uhakika, ukitumia imani, utaongozwa kupata suluhisho ambalo vinginevyo usingelipata.”10

Kuwa mfuasi bora wa Mwokozi Yesu Kristo ni safari ya maisha yote, na sisi sote tuko katika hatua tofauti, tukitembea kwa mwendo tofauti. Lazima tukumbuke kuwa haya si mashindano, na tuko hapa kupendana na kusaidiana. Tunahitaji kuwa wenye kutenda ili kumruhusu Mwokozi afanye kazi nasi katika maisha yetu.

Akiongea na Sidney Rigdon, Bwana alisema yafuatayo: “Nimekuangalia na kazi zako. Nimezisikia sala zako, na nimekutayarisha kwa kazi iliyo kuu.”11 Nashuhudia kwamba Bwana husikia na kujibu sala; Anatujua; na Ana kazi kubwa kwa ajili ya kila mmoja wetu. Kupitia sala, na kujifunza maandiko, na kutenda, tunaweza kufungua baraka za mbinguni na kuwa wafuasi bora wa Mwokozi Yesu Kristo.

Raisi Dallin H. Oaks alifundisha kwamba: “hukumu ya Mwisho si tu tathmini ya majumuisho ya matendo mema na mabaya—yale tuliyofanya. Ni utambuzi wa athari ya mwisho ya matendo na mawazo—kile ambacho tumekuwa.”12

Ninashukuru kwa manabii, waonaji, na wafunuzi; wao ndio walinzi kwenye mnara. Wanaona vitu ambavyo hatuvioni. Nashuhudia kwamba kupitia maneno yao, tunaweza kuwa wafuasi bora wa Mwokozi Yesu Kristo na kufikia takdiri yetu. Nashuhudia kwamba Kristo anaishi na anamjua kila mmoja wetu kibinafsi. Hili ni kanisa Lake. Katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.

Chapisha