Mkutano Mkuu
Ukweli wa Milele
Mkutano mkuu wa Oktoba 2023


Ukweli wa Milele

Hitaji la kutambua ukweli sasa ni la msingi sana!

Akina kaka na akina dada, tunawashukuru kwa kujitolea kwenu kwa Mungu Baba na kwa Mwanawe, Yesu Kristo, na tunashukuru kwa upendo wenu na huduma kwa kila mmoja. Ninyi ni watu bora sana!

Utangulizi

Baada ya mimi na mke wangu, Anne kupokea wito wa kutumikia kama viongozi wa misheni, familia yetu iliazimia kujua jina la kila mmisionari kabla ya kwenda eneo la misheni. Tulipata picha, tukatengeneza kadi zenye maelezo machache kuwahusu wao na kuanza kuchunguza nyuso na kukariri majina.

Tulipowasili, tuliitisha mikutano ya utambulisho pamoja na wamisionari. Tulipokuwa tukichangamana, nilimsikia mvulana wetu wa miaka tisa akisema:

“Nafurahi kukutana nawe, Sam!”

“Rachel, unatokea wapi?”

“Wow, David, wewe ni mrefu!”

Baada ya kujua hilo, nilimwendea mtoto wetu na kumnong’oneza, “Hujambo, kumbuka kuwaita wamisionari Mzee au Dada.”

Aliniangalia kwa mshangao na kusema, “Baba, nilidhani tulipaswa kukariri majina yao.” Mwana wetu alifanya kile alichodhani kilikuwa sahihi kulingana na uelewa wake.

Hivyo, ni upi uelewa wetu wa ukweli katika ulimwengu wa leo? Mara kwa mara tunalipuliwa na mitazamo mikali, ripoti za upendeleo na data zisizo kamili. Wakati huo huo, ukubwa na vyanzo vya taarifa hii vinakuwa kwa kasi. Hitaji la kutambua ukweli sasa ni la msingi sana!

Ukweli ni muhimu kwetu ili kujenga na kuimarisha uhusiano na Mungu, kupata amani na shangwe na kufikia hatma yetu ya kiungu. Leo, ngoja tuzingatie maswali yafuatayo:

  • Ukweli ni nini na kwa nini ni wa muhimu?

  • Je tunaupataje ukweli?

  • Tuupatapo ukweli, je, tunaushiriki vipi?

Ukweli ni wa Milele

Bwana alitufundisha katika maandiko kwamba, “ukweli ni maarifa ya mambo kama yalivyo, na kama yalivyokuwa, na kama yatakavyokuwa” (Mafundisho na Maagano 93:24). “Haukuumbwa au kutengenezwa” (Mafundisho na Maagano 93:29) na “hauna mwisho” (Mafundisho na Maagano 88:66).1 Ukweli ni kamili, usiobadilika na usiofichika. Kwa maneno mengine, ukweli ni wa milele.2

Ukweli hutusaidia kuepuka uongo,3 kutambua jema kutokana na baya,4 kupokea ulinzi,5 na kupata faraja na uponyaji.6 Ukweli pia unaweza kuongoza matendo yetu,7 kutuweka huru,8 kututakasa,9 na kutuongoza kwenye uzima wa milele.10

Mungu Hufunua Ukweli wa Milele

Mungu hufunua ukweli wa milele kwetu kupitia mtandao wa uhusiano wa kimafunuo ukimuhusisha Yeye mwenyewe, Yesu Kristo, Roho Mtakatifu, manabii na sisi. Acha tujadili majukumu tofauti lakini yanayoingiliana ambayo kila mshiriki huyafanya katika mchakato huu.

Kwanza, Mungu ni chanzo cha ukweli wote wa milele.11 Yeye na Mwanawe, Yesu Kristo,12 wana uelewa mkamilifu wa ukweli na daima hutenda kulingana na kanuni na sheria za kweli.13 Nguvu hizi huwaruhusu Wao kutengeneza na kutawala ulimwengu14 pamoja na kutupenda, na kutuongoza, kutulea kikamilifu.15 Wanatutaka sisi tuelewe na tutumie ukweli ili sisi tuweze kufurahia baraka ambazo Wao wanazo.16 Wao wanaweza kuutoa ukweli huo binafsi au kwa kawaida, kupitia wajumbe kama vile Roho Mtakatifu, malaika au manabii wanaoishi.

Pili, Roho Mtakatifu hushuhudia ukweli wote.17 Yeye hufunua kweli kwetu moja kwa moja na hushuhudia juu ya ukweli uliofundishwa na wengine. Misukumo kutoka kwa Roho kwa kawaida huja kama mawazo akilini mwetu na hisia mioyoni mwetu.18

Tatu, manabii hupokea ukweli kutoka kwa Mungu na kushiriki ukweli huo pamoja nasi.19 Tunajifunza ukweli kutoka kwa manabii waliopita katika maandiko20 na kutoka kwa manabii walio hai kwenye mkutano mkuu na kupitia njia zingine rasmi za mawasiliano.

Mwishowe, wewe na mimi tuna jukumu muhimu katika mchakato huu. Mungu anategemea tutafute, tutambue na tutende juu ya ukweli. Uwezo wetu wa kupokea na kuutumia ukweli hutegemea uimara wa uhusiano wetu na Baba na Mwana, uitikiaji wetu kwenye ushawishi wa Roho Mtakatifu, na unyoofu wetu kwa manabii wa siku za mwisho.

Tunahitaji kukumbuka kwamba Shetani anafanya kazi kutuweka sisi mbali na ukweli. Anajua kwamba bila ukweli, hatuwezi kupata uzima wa milele. Anasuka nyuzi za ukweli kwa filosofia za ulimwengu ili kutukanganya na kutuvuruga sisi kutoka kwenye kile kinachowasilishwa na Mungu.21

Kutafuta, Kutambua na Kutumia Ukweli wa Milele

Tunapotafuta ukweli wa milele,22 maswali mawili yafuatayo yanaweza kutusaidia tutambue kama wazo hutoka kwa Mungu au kutoka chanzo kingine:

  • Je, jambo linafundishwa mara kwa mara katika maandiko na manabii walio hai?

  • Je, jambo hilo limethibitishwa kwa ushahidi wa Roho Mtakatifu?

Mungu hufunua kweli za kimaandiko kupitia manabii na Roho Mtakatifu huthibitisha kweli hizo na hutusaidia kuzitumia.23 Sisi lazima tutafute na tujiandae kupokea misukumo hii ya kiroho pale inapokuja.24 Tunapokea vyema ushuhuda wa Roho pale tuwapo wanyenyekevu,25 kuomba kwa dhati na kujifunza maneno ya Mungu,26 na kushika amri Zake.27

Pale Roho Mtakatifu anapothibitisha kuhusu ukweli mahususi kwetu, uelewa wetu huongezeka kwa kadiri tunapoiweka kanuni hiyo kwenye matendo. Baada ya muda, tunapoendelea kuishi kanuni hiyo, tunapata maarifa ya uhakika ya ukweli huo.28

Kwa mfano, nimefanya makosa na kuhisi hatia kwa chaguzi mbaya. Lakini kupitia sala, kujifunza na imani katika Yesu Kristo, nilipokea ushahidi wa kanuni ya toba.29 Nilipoendelea kutubu, uelewa wangu kuhusu toba ulikuwa imara. Nilihisi kuwa karibu na Mungu na Mwana Wake. Sasa najua kwamba dhambi inaweza kusamehewa kupitia kwa Yesu Kristo, kwa sababu nimepata baraka za toba kila siku.30

Mtumaini Mungu Wakati Ukweli Bado Haujafunuliwa

Je, tunapaswa kufanya nini tunapotafuta kwa dhati ukweli ambao bado haujafuniliwa? Ninawahurumia sana wale miongoni mwetu wanaotamani majibu ambayo hayaonekani kuja.

Kwa Joseph Smith, Bwana alishauri, “Nyamaza mpaka nitakapoona inafaa kuyafanya mambo yote yajulikane … kuhusu jambo hili” (Mafundisho na Maagano10:37).

Na kwa Emma Smith, Bwana alielezea “Usinungʼunike kwa sababu ya vitu ambavyo wewe hujaviona, kwani vimezuiliwa kwako na kwa ulimwengu, ambayo ni hekima kwangu katika wakati ujao” (Mafundisho na Maagano 25:4).

Mimi pia nimetafuta majibu kwa maswali ya nafsi. Majibu mengi yamekuja, na baadhi hayajaja.31 Tunapoendelea kusubiri—tukiamini hekima na upendo wa Bwana, tukishika amri zake na kutegemea kile ambacho tunajua—Yeye anatusaidia kupata amani mpaka afunue ukweli wa vitu vyote.32

Kuelewa Mafundisho na Sera

Tutafutapo ukweli, ukweli huo hutusaidia kuelewa tofauti kati ya mafundisho na sera. Mafundisho hurejelea kweli za milele, kama vile asili ya Uungu, mpango wa wokovu, na dhabihu ya upatanisho ya Yesu Kristo. Sera ni matumizi ya mafundisho kulingana na hali ya sasa. Sera hutusaidia tulisimamie Kanisa kwa mpangilio.

Wakati mafundisho kamwe hayabadiliki, sera hubadilika mara kwa mara. Bwana hutenda kazi kupitia manabii Wake ili kuimarisha mafundisho Yake na kuboresha sera za Kanisa kulingana na mahitaji ya watoto Wake.

Kwa bahati mbaya, wakati mwingine tunachanganya sera na mafundisho. Kama hatuelewi tofauti, tunajihatarisha kukata tamaa pale sera zinapobadilika na kusababisha kuhoji hekima ya Mungu au jukumu la ufunuo la manabii.33

Kufundisha Ukweli wa Milele

Tunapopokea ukweli kutoka kwa Mungu, anatuhimiza kushiriki maarifa hayo na wengine.34 Tunafanya hili tunapofundisha darasa, kumwongoza mtoto au kujadili kweli za injili pamoja na rafiki.

Lengo letu ni kufundisha ukweli katika njia ambayo hualika nguvu ya uongofu ya Roho Mtakatifu..35 Acha nishiriki baadhi ya mialiko rahisi kutoka kwa Bwana na manabii Wake ambayo inaweza kusaidia.36

  1. Fokasi kwa Baba wa Mbinguni, Yesu Kristo na mafundisho Yao ya msingi.37

  2. Bakia imara kwenye maandiko na katika mafundisho ya manabii wa siku za mwisho.38

  3. Tegemea mafundisho yaliyodhibitishwa kupitia mashahidi kadhaa wenye mamlaka.39

  4. Epuka kubahatisha, maoni binafsi au mawazo ya kilimwengu.40

  5. Fundisha kipengele cha mafundisho ndani ya mazingira yahusianayo na kweli za injili.41

  6. Tumia mbinu za kufundisha ambazo hualika ushawishi wa Roho.42

  7. Wasiliana wazi wazi ili kuepuka kutoelewana.43

Ongea Ukweli kwa Upendo

Jinsi tunavyofundisha ukweli ni jambo la msingi sana. Paulo anatuhimiza kuzungumza “ukweli katika upendo” (ona Waefeso 4:14–15). Ukweli huwa na nafasi nzuri ya kumbariki mtu mwingine wakati unapofikishwa kwa upendo kama wa Kristo.44

Ukweli ufundishwao bila upendo unaweza kusababisha hisia za hukumu, kukata tamaa na upweke. Daima hupelekea kwenye kinyongo na mgawanyiko—hata ugomvi. Kwa upande mwingine, upendo bila ukweli ni bure na hukosa ahadi ya ukuaji.

Vyote ukweli na upendo ni vya msingi katika ukuaji wetu wa kiroho.45 Ukweli hutoa mafundisho, kanuni na sheria zilizo muhimu kupata uzima wa milele, wakati upendo hukuza ari inayohitajika kukumbatia na kutenda juu ya kile kilicho kweli.

Daima nina shukrani kwa wengine ambao kwa subira walinifundisha kanuni za milele kwa upendo.

Hitimisho

Katika kuhitimisha, acha nishiriki kweli za milele ambazo zimekuwa nanga kwa nafsi yangu. Nimepata kujua kweli hizi kwa kufuata kanuni zilizojadiliwa leo.

Najua kwamba Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni.46 Yeye anajua yote,47 ana nguvu zote,48 na anapenda kwa ukamilifu.49 Alitengeneza mpango kwa ajili yetu ili tupate uzima wa milele na kuwa kama Yeye.50

Kama sehemu ya mpango huo, Yeye alimtuma Mwana Wake, Yesu kristo, atusaidie.51 Yesu alitufundisha tufanye mapenzi ya Baba52 na tupendane.53 Alilipia dhambi zetu54 na kuyatoa maisha Yake msalabani.55 Alifufuka kutoka wafu baada ya siku tatu.56 Kupitia Kristo na neema Yake, tutafufuka,57 tunaweza kusamehewa,58 na tunaweza kupata nguvu katika mateso.59

Wakati wa huduma Yake duniani, Yesu alianzisha Kanisa Lake.60 Baada ya muda, Kanisa hilo lilibadilishwa na kweli zikapotea.61 Yesu Kristo alirejesha Kanisa Lake na kweli za injili kupitia Nabii Joseph Smith.62 Na leo, Kristo anaendelea kuongoza Kanisa Lake kupitia manabii na mitume walio hai.63

Ninajua kwamba tunaposonga kwa Kristo, hatimaye “tutakamilishwa ndani yake” (Moroni 10:32), kupata “shangwe kamili” (Mafundisho na Maagano 93:33), na kupokea “vyote ambayo Baba anavyo” (Mafundisho na Maagano 84:38). Juu ya kweli hizi za milele ninashuhudia katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona pia Zaburi 117:2; Mafundisho na Maagano 1:39.

  2. “Kinyume na mashaka ya baadhi yenu kuna kitu kama hicho cha ukweli na uongo. Hakika kuna ukweli halisi—ukweli wa milele. Mojawapo wa majanga ya siku yetu ni kwamba watu wachache wanajua wapi pa kugeukia kwa ajili ya ukweli” (Russell M. Nelson, “Ukweli Halisi, Mafundisho Halisi na Ufunuo Halisi,” Liahona, Nov. 2021, 6).

  3. Ona Joseph Smith—Mathayo 1:37.

  4. Ona Moroni 7:19.

  5. Ona 2 Nefi 1:9; Mafundisho na Maagano 17:8.

  6. Ona Yakobo 2:8

  7. Ona Zaburi 119:105; 2 Nefi 32:3.

  8. Ona Yohana 8:32; Mafundisho na Maagano 98:8.

  9. Ona Yohana 17:17.

  10. Ona 2 Nefi 31:20.

  11. Ona Mafundisho na Maagano 88:11–13; 93:36.

  12. Ona Yohana 5:19–20; 7:16; 8:26; 18:37; Musa 1:6.

  13. Ona Waebrania 42:12–26; Mafundisho na Maagano 88:41.

  14. Ona Musa 1:30–39.

  15. Ona 2 Nefi 26:24.

  16. Ona Mafundisho na Maagano 82:8–9.

  17. Ona Yohana 16:13; Yakobo 4:13; Moroni 10:5; Mafundisho na Maagano 50:14; 75:10; 76:12; 91:4; 124:97.

  18. Ona Mafundisho na Maagano 6:22–23; 8:2–3.

  19. Ona Yeremia 1:5, 7; Amosi 3:7; Mathayo 28:16–20; Moroni 7:31; Mafundisho na Maagano 1:38; 21:1–6; 43:1–7. Nabii ni “mtu ambaye ameitwa na huongea kwa niaba ya Mungu. Kama mjumbe wa Mungu, nabii hupokea mamlaka ya ukuhani, amri, unabii na ufunuo kutoka kwa Mungu. Jukumu lake ni kujulisha mapenzi na hulka ya kweli ya Mungu kwa wanadamu na kuonyesha maana ya uhusiano wa Mungu na wanadamu. Nabii hupinga dhambi na kutabiri matokeo yake. Yeye ni mhubiri wa haki. Wakati mwingine, nabii anaweza kuongozwa ili kutabiri yajayo kwa manufaa ya wanadamu. Jukumu lake la msingi, hata hivyo, ni kutoa ushuhuda wa Kristo. Rais wa Kanisa La Yesu Kristo La Watakatifu wa Siku za Mwisho ni nabii wa Mungu duniani leo. Washiriki wa Urais wa Kwanza na Mitume Kumi na Wawili wanakubalika kama manabii, waonaji na wafunuzi” (Mwongozo wa Maandiko, “Nabii,” Maktaba ya Injili). Mifano ya kanuni hizi inapatikana katika maisha ya Adamu (ona Musa 6:51–62), Henoko (ona Musa 6:26–36), Nuhu (ona Musa 8:19, 23–24), Ibrahimu (ona Mwanzo 12:1–3; Ibrahimu 2:8–9), Musa (ona Kutoka 3:1–15; Musa 1:1–6, 25–26), Petro (ona Mathayo 16:13–19), na Joseph Smith (ona Mafundisho na Maagano 5:6–10; 20:2; 21:4–6).

  20. Ona 2 Timotheo 3:16.

  21. Ona Yohana 8:44; 2 Nephi 2:18; Mafundisho na Maagano 93:39; Musa 4:4.

  22. Ona 1 Nefi 10:19. Rais Dallin H. Oaks alielekeza: “Tunahitaji kuwa waangalifu wakati tunapotafuta ukweli wa [Mungu] na kuchagua vyanzo kwa ajili ya uchunguzi huo. Hatupaswi kuzingatia umaarufu au mamlaka ya kidunia kama vyanzo vya ukweli vya kuaminika. … Wakati tunapotafuta ukweli kuhusu dini, tunapaswa kutumia mbinu za kiroho zinazofaa kwa ajili ya uchunguzi huo: sala, ushahidi wa Roho Mtakatifu na kujifunza maandiko na maneno ya manabii wa sasa” (“Ukweli na Mpango,” Liahona, Nov. 2018, 25).

  23. Mzee D. Todd Christofferson alifundisha: “Mitume na manabii … hutangaza neno la Mungu, lakini kama nyongeza, tunaamini wanaume na wanawake kwa ujumla na hata watoto wanaweza kujifunza na kuongozwa na ushawishi mtakatifu katika kujibu sala na kujifunza maandiko. … Waumini wa Kanisa la Yesu Kristo hupewa kipawa cha Roho Mtakatifu, ambacho huwezesha mawasiliano endelevu na Baba yao wa Mbinguni. … Hii si kusema kwamba kila muumini huzungumza kwa ajili ya Kanisa au anaweza kufafanua maandiko ya Kanisa bali kwamba kila mmoja aweze kupokea mwongozo mtakatifu katika kukabiliana na changamoto na fursa za maisha yake” (“The Doctrine of Christ,” Liahona, Mei 2012, 89–90, note 2).

  24. Ona 2 Nefi 33:1–2.

  25. Ona Mafundisho na Maagano 1:28.

  26. Ona Moroni 10:3–5; Mafundisho na Maagano 9:7–9; 84:85.

  27. Ona Mafundisho na Maagano 5:35; 63:23; 93:27–28. Licha ya juhudi zetu za dhati, baadhi yetu bado wanaweza kupata ugumu kumhisi Roho kutokana na changamoto za afya ya akili. Msongo wa mawazo, wasiwasi na hali zingine za ubongo zinaweza kuongeza ugumu kwenye kumtambua Roho Mtakatifu. Katika hali kama hizo, Bwana anatualika tuendelee kuishi injili, na Yeye atatubariki (ona Mosia 2:41). Tunaweza kutafuta shughuli za ziada—kama vile kusikiliza muziki mtakatifu, kujikita kwenye shughuli, au kutumia muda kwenye asili—ambapo kutatusaidia tuhisi matunda ya Roho (ona Wagalatia 5:22–23) na kuimarisha muunganiko wetu kwa Mungu.

    Mzee Jeffrey R. Holland alieleza: “Hivyo basi, unajibu vipi wakati changamoto za kiakili na kihisia zinakukabili wewe ama wale unaowapenda? Zaidi ya yote, usipoteze imani katika Baba yako wa Mbinguni, ambaye anakupenda zaidi ya unavyoweza kufikiria. … Kwa uaminifu tafuteni njia tukufu ambazo zimethibitishwa ambazo huleta Roho ya Bwana katika maisha yenu. Tafuteni ushauri wa wale wanaoshikilia funguo kwa ajili ya ustawi wako wa kiroho. Omba na uitunze nguvu ya baraka ya ukuhani. Pokea sakramenti kila wiki, na ushikilie kwa nguvu ahadi za ukamilifu za Upatanisho wa Yesu Kristo. Kuwa na imani katika miujiza. Nimewaona wengi wao wakija wakati kila ishara nyingine waliyonayo inaonyesha kwamba tumaini limepotea. Tumaini kamwe halipotei” (“Like a Broken Vessel,” Liahona, Nov. 2013, 40–41).

  28. Ona Yohana 7:17; Alma 32:26–34. Hatimaye, Mungu hutamani sisi tupate ukweli “mstari juu ya mstari, amri juu ya amri,” mpaka tuelewe vitu vyote (ona Mithali 28:5; 2 Nefi 28:30; Mafundisho na Maagano 88:67; 93:28).

  29. Ona 1 Yohana 1:9–10; 2:1–2.

  30. Rais Nelson alieleza: “Hakuna kinacholeta uhuru zaidi, cha kiungwana zaidi, au cha muhimu zaidi kwa ukuaji wetu binafsi kuliko ilivyo fokasi yetu ya kila siku, kwenye toba. Toba siyo tukio; ni mchakato. Ni ufunguo kwa furaha na amani ya akili. Inapoambatana na imani, toba hufungua kufikia kwetu kwenye nguvu ya Upatanisho ya Yesu Kristo” (“Tunaweza Kufanya Vizuri Zaidi na Kuwa Bora Zaidi,” Liahona, Mei 2019, 67).

  31. Sijui sababu zote za kwa nini Mungu hutuzuia sisi kwenye kweli zote za milele, lakini Mzee Orson F Whitney alitoa mawazo ya kuvutia: “Ni baraka kuamini kuliko kuona, kwani kwa kuonyesha imani huja maendeleo ya kiroho, chanzo kimojawapo kikuu sana cha uwepo wa mwanadamu, wakati maarifa, kama ikiimeza imani, huizuia isifanye kazi, hivyo kuzuia maendeleo hayo. ‘Maarifa ni nguvu;’ na vitu vyote vitajulikana kwa wakati sahihi. Lakini maarifa yasiyokomaa—kujua ndani ya muda usio sahihi—ni hatari kwa vyote maendeleo na furaha” (“The Divinity of Jesus Christ,” Improvement Era, Jan. 1926, 222; ona pia Liahona, Dec. 2003, 14–15).

  32. Ona Mafundisho na Maagano 76:5–10. Bwana pia alimshauri Hyrum Smith, “Usitafute kulitangaza neno langu, bali kwanza tafuta kulipata neno langu. … Kaa kimya [na] jifunze neno langu ” (Mafundisho na Maagano 11:21–22). Nabii Alma anatoa mfano wa kushughulikia maswali ambayo hayajajibiwa: “Siri hizi hazijafahamishwa kwangu kabisa; kwa hivyo sitaongea tena” (Alma 37:11). Pia alielezea kwa mwana wake Koriantoni kwamba “kuna siri nyingi ambazo zimefichwa, ambazo hakuna azijuaye isipokuwa Mungu mwenyewe” (Alma 40:3). Nimepata pia nguvu kutokana na jibu la Nefi wakati yeye alipopata swali ambalo hakuweza kulijibu: “Najua kwamba [Mungu] anawapenda watoto wake; walakini sijui maana ya vitu vyote” (1 Nefi 11:17).

  33. Vivyo hivyo, desturi za kimila sio mafundisho wala sera. Zinaweza kutumiwa kama hutusaidia kufuata mafundisho na sera, lakini pia huweza kuzuia ukuaji wetu wa kiroho kama hazijalenga kanuni za kweli. Tunapaswa kuepuka desturi ambazo hazijengi imani zetu au kutusaidia kusonga kuelekea maisha ya milele.

  34. Ona Mafundisho na Maagano 15:5; 88:77–78.

  35. Ona Mafundisho na Maagano 50:21–23.

  36. Imetoholewa kutoka “Principles for Ensuring Doctrinal Purity,” iliyokubalika na Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili mnamo Februari, 2023).

  37. Ona 1 Nefi 15:14. Bwana aliwaelekeza watumishi wake kuepuka kufokasi kwenye imani au dhana ambazo si kitovu cha injili Yake “Na juu ya imani wewe usizungumzie, bali wewe utatangaza toba na imani juu ya Mwokozi, na ondoleo la dhambi kwa ubatizo, na kwa moto, ndivyo, hata Roho Mtakatifu” (Mafundisho na Maagano 19:31).

    Mzee Neil L. Andersen alielezea: “Acha tufokasi kwa Mwokozi Yesu Kristo na zawadi ya dhabihu Yake ya upatanisho. Hii haimaanishi kwamba hatuwezi kusimulia uzoefu kutoka kwenye maisha yetu wenyewe au kushiriki mawazo kutoka kwa wengine. Wakati mada yetu inaweza kuhusu familia au huduma au mahekalu au misheni ya hivi karibuni, kila kitu … kinapaswa kuelekezwa kwa Bwana Yesu Kristo” (“Tunazungumza Kuhusu Kristo,” Liahona, Nov. 2020, 89–90).

  38. Ona Mafundisho na Maagano 28:2–3, 8. Nabii Alma aliwaasa wale waliochaguliwa kufundisha injili “wasifundishe chochote ila tu vitu vile ambavyo alikuwa amewafundisha, na ambavyo vilikuwa vimezungumzwa na manabii watakatifu” (Mosia 18:19).

    Rais Henry B. Eyring alitangaza, “Tunapaswa kufundisha mafundisho ya msingi ya Kanisa kama yalivyo katika maandiko ya msingi na mafundisho ya manabii, ambao jukumu lao ni kutoa mafundisho” (“The Lord Will Multiply the Harvest” [evening with a General Authority, Feb. 6, 1998], in Teaching Seminary: Preservice Readings [2004], 96).

    Mzee D. Todd Christofferson alishuhudia kwamba “katika Kanisa leo, kama ilivyokuwa zamani, kuanzisha mafundisho ya Kristo ama kusahihisha makosa ya mafundisho ni jambo lenye ufunuo wa kiungu kwa wale ambao Bwana amewatunukia mamlaka ya kitume” (“The Doctrine of Christ,” 86).

  39. Ona 2 Wakorintho 13:1; 2 Nefi 11:3; Etheri 5:4; Mafundisho na Maagano 6:28. Mzee Neil L. Andersen alisema: “Wachache walihoji imani yao walipopata kaulli iliyotolewa na kiongozi wa Kanisa miongo kadhaa iliyopita ambayo haikuwa sawa na mafundisho yetu. Kuna kanuni muhimu inayosimamia mafundisho ya Kanisa. Fundisho hufundishwa na washiriki wote15 wa Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili. Haifichwi katika aya isiyoonekana ya hotuba moja. Kanuni za kweli hufundishwa na wengi na mara kwa mara. Mafundisho yetu sio magumu kuyapata” (“Trial of Your Faith,” Liahona, Nov. 2012, 41).

    Mzee D. Todd Christofferson vivyo hivyo alifundisha: “Inapaswa ikumbukwe kwamba si lazima kila maelezo yanayotolewa na kiongozi wa Kanisa, aliyepita au aliyeko sasa, lazima yajumuishe mafundisho. Inaeleweka kawaida katika Kanisa kwamba maelezo yanayotolewa na kiongozi mmoja kwenye tukio moja daima yanawakilisha oni binafsi, ingawaje huwa ni oni lililozingatiwa vyema, ambalo halikukusudiwa kuwa rasmi au la kufuatwa na Kanisa lote.” (“The Doctrine of Christ,” 88).

  40. Ona 3 Nefi 11:32, 40. Rais Gordon B. Hinckley alisema: “Nimewahi kuongea kuhusu umuhimu wa kuyatunza mafundisho ya Kanisa kuwa safi. … Nina wasiwasi kwenye hili. Upotoshaji mdogo katika ufundishaji wa mafundisho huweza kupelekea uongo mkubwa na wa kishetani ” (in Teachings of Gordon B. Hinckley [1997], 620).

    Rais Dallin H. Oaks alionya kwamba kuna baadhi “ambao huchagua sentensi chache kutoka kwenye mafundisho ya nabii na kuyatumia kusaidia ajenda zao za kisiasa au malengo mengine binafsi. … Kutumia maneno ya nabii kusaidia ajenda binafsi, ya kisiasa au kiuchumi au vinginevyo, ni kujaribu kucheza na nabii, na siyo kumfuata nabii” (“Our Strengths Can Become Our Downfall” [Brigham Young University devotional, June 7, 1992], 7, speeches.byu.edu).

    Rais Henry B. Eyring alionya: “Mafundisho hupata nguvu yake wakati Roho Mtakatifu anapothibisha kwamba ni kweli. … Kwa sababu tunahitaji Roho Mtakatifu, ni lazima tuwe waangalifu na makini ili tusifundishe zaidi ya mafundisho ya kweli. Roho Mtakatifu ndiye Roho wa Kweli. Uthibitisho Wake unaalikwa kwa kuepukana na dhana au fasiri binafsi. Hiyo inaweza ngumu kufanya. … Inavutia kujaribu kitu kipya au cha kuvutia. Bali tunaalika Roho Mtakatifu kama mwenzi wetu wakati tunapokuwa makini kufunza mafundisho ya kweli. Njia moja ya hakika zaidi ya kuzuia hata kukaribia mafundisho ya kupotosha ni kuchagua kurahisisha kufundisha kwetu. Usalama unapatikana kwa urahisi huo, na kidogo sana hupotea” (“The Power of Teaching Doctrine,” Liahona, July 1999, 86).

    Mzee Dale G. Renlund alifundisha: “Kutafuta uelewa zaidi ni sehemu muhimu ya ukuaji wetu kiroho, lakini tafadhali kuwa makini. Kutafuta uelewa hakuwezi kuondoa ufunuo. Uchunguzi hakutapelekea uelewa mkubwa wa kiroho, lakini utatupeleka kwenye udanganyifu au kugeuza mwelekeo wetu kutoka kwenye kile kilichofunuliwa” (“Asili Yako ya Kiungu na Hatma Yako ya Milele,” Liahona, Mei 2022, 70).

  41. Ona Mathayo 23:23. Rais Joseph F. Smith alionya: “Si busara sana kuchukua kipande cha ukweli na kukifanya kuwa ukweli kamili. … Kanuni zote zilizofunuliwa za injili ya Kristo ni za muhimu na msingi katika mpango wa wokovu.” Alielezea zaidi: “Si sera nzuri au mafundisho ya kuvutia kuchukua sehemu ya hizi, kuzitenganisha kutoka kwenye mpango mzima wa ukweli wa injili, kuzifanya mchezo maalumu na kuzitegemea kwa ajili ya wokovu wetu au maendeleo. … Zote ni za muhimu” (Gospel Doctrine, 5th edition [1939], 122).

    Mzee Neal A. Maxwell alielezea: “Kanuni za injili … huhitaji kufungamanishwa. Zinapoachanishwa au kutenganishwa, tafsiri za watu na utekelezaji wa mafundisho haya huweza kuwa sumu. Upendo, kama hautafunganishwa na amri ya saba, unaweza kuwa wa kidunia. Amri ya tano husisitiza kuwaheshimu wazazi, kama haitafunganishwa na amri ya kwanza, inaweza kupelekea heshima kamili kwa wazazi wasio waaminifu na sio kwa Mungu. … Hata saburi huwekwa sawa kwa ‘kukemea kwa ukali kwa wakati wake, utakapokuwa umeongozwa na Roho Mtakatifu’ [Mafundisho na Maagano 121:43]” (“Behold, the Enemy Is Combined,” Ensign, Mei 1993, 78–79).

    Rais Marion G. Romney alielekeza, “Kupekua [maandiko] kwa lengo la kugundua kile yanachofundisha kama ilivyoamriwa na Yesu ni tofauti na kupekua ndani yake kwa lengo la kupata vipengele ambavyo vinaweza kutumika kwenye huduma ili kusaidia hitaji lililopangwa” (“Records of Great Worth,” Ensign, Sept. 1980, 3).

  42. Ona 1 Wakorintho 2:4; Moroni 6:9. Mzee Jeffrey R. Holland alisisitiza hitaji la kuwasiliana injili ya Yesu Kristo katika njia inayopelekea kuinuliwa kiroho kupitia nguvu ya Roho Mtakatifu: “Bwana kamwe hajatoa ushauri wa kusisitiza kwa Kanisa kama ule wa kufundisha injili ‘kwa Rohom hata mfariji aliyetumwa kufundisha ukweli.’ Je, tunafundisha injili ‘kwa Roho wa ukweli?’ Yeye ameuliza. Au tunaifundisha ‘katika njia zinginezo? Na kama itakuwa kwa njia nyingine,’ anaonya ‘hatokani na Mungu’ [Mafundisho na Maagano 50:14, 17–18]. … Hakuna mafunzo ya milele yanayoweza kutokea pasipo kuhuishwa huko kwa Roho kutoka mbinguni. … Hicho ndicho waumini wetu hasa huhitaji. … Wanataka imani yao iimarishwe na tumaini lao lifanywe upya. Wanataka, kwa ufupi, kulishwa na neno zuri la Mungu, kuimarishwa na nguvu za mbinguni” (“Mwalimu Anatoka kwa Mungu,” Ensign, Mei 1998, 26).

  43. Ona Alma 13:23. Akiongea kuhusu Baba yetu wa Mbinguni, Rais Russell M. Nelson alishuhudia, “Anawasiliana kwa urahisi, kimya kimya na kwa uwazi wa hali ya juu kiasi kwamba hatuwezi kutomuelewa” (“Msikilize Yeye,” Liahona, Mei 2020, 89).

  44. Ona Zaburi 26:3; Warumi 13:10; 1 Wakorintho 13:1–8; 1 Yohana 3:18.

  45. Ona Zaburi 40:11.

  46. Ona Warumi 8:16.

  47. Ona 1 Samweli 2:3; Mathayo 6:8; 2 Nefi 2:24; 9:20.

  48. Ona Mwanzo 17:1; Yeremia 32:17; 1 Nefi 7:12; Alma 26:35.

  49. Ona Yeremia 31:3; 1 Yohana 4:7–10; Alma 26:37.

  50. Ona 2 Nefi 9; Mafundisho na Maagano 20:17–31; Musa 6:52–62.

  51. Ona Yohana 3:16; 1 Yohana 4:9–10.

  52. Ona Yohana 8:29; 3 Nefi 27:13.

  53. Ona Yohana 15:12; 1 Yohana 3:11.

  54. Ona Luka 22:39–46.

  55. Ona Yohana 19:16–30.

  56. Ona Yohana 20:1–18.

  57. See 1 Wakorintho 15:20–22; Mosia 15:20–24; 16:7–9; Mafundisho na Maagano 76:16–17.

  58. Ona Matendo ya Mitume 11:17–18; 1 Timotheo 1:14–16; Alma 34:8–10; Moroni 6:2–3, 8; Mafundisho na Maagano 19:13–19.

  59. See Mathayo 11:28–30; 2 Wakorintho 12:7–10; Wafilipi 4:13; Alma 26:11–13.

  60. Ona Mathayo 16:18–19; Waefeso 2:20.

  61. Ona Mathayo 24:24; Matendo ya Mitume 20:28–30.

  62. Ona Mafundisho na Maagano 20:1–4; 21:1–7; 27:12; 110; 135:3; Joseph Smith—Historia ya 1:1–20.

  63. Ona Mafundisho na Maagano 27:38; 43:1–7; 107:91–92.

Chapisha