Sura ya 14
Abinadi na Mfalme Nuhu
Zenifu alikuwa mfalme mwenye haki wa kundi la Wanefi. Alipozeeka, mtoto wake Nuhu alikuwa mfalme.
Nuhu hakuwa mfalme mzuri kama baba yake. Alikuwa mwovu na hangetii amri za Mungu.
Aliwalazimisha watu wake kumpa sehemu ya kipato chao, mifugo, dhahabu na fedha.
Mfalme Nuhu alifanya hivi kwa kuwa alikuwa mvivu. Aliwafanya Wanefi kumpa kila kitu alichohitaji ili kuishi.
Aliwaweka makuhani waovu badala ya wale wema ambao baba yake aliwaweka. Makuhani hawa waovu waliwafundisha watu kutenda dhambi.
Mfalme Nuhu alikuwa na majengo mengi mazuri, ikijumuisha kasri kubwa lenye kiti cha enzi. Majengo yalikuwa yamepambwa kwa dhahabu, fedha na mbao za thamani sana.
Nuhu aliupenda utajiri aliochukua kutoka kwa watu wake. Yeye pamoja na makuhani wake walitumia muda wao kunywa mvinyo na kuwa waovu.
Mungu alimtuma nabii aliyeitwa Abinadi kwa watu wa Nuhu. Abinadi aliwaonya kwamba kama hawangetubu, wangekuwa watumwa wa walamani.
Wakati mfalme Nuhu aliposikia kile Abinadi alichosema, alikasirika. Aliwatuma watu kumpleka Abinadi kwenye kasri ili kwamba amuue.
Abinadi alipelekwa kwa mfalme. Mfalme Nuhu na makuhani wake walimuuliza maswali mengi. Walijaribu kumtega katika kusema kitu kisicho sahihi.
Abinadi hakuogopa kujibu maswali yao. alijua kwamba Mungu angemsaidia. Makuhani walishangazwa na majibu ya Abinadi.
Mfalme Nuhu alikasirika na kuamuru makuhani wake kumuua Abinadi. Abinadi aliwaambia kama wangemgusa, Mungu angewaua.
Roho Mtakatifu alimlinda Abinadi ili kwamba angemaliza kusema Bwana alichomtaka kusema. Uso wa Abinadi uling’aa. Makuhani waliogopa kumgusa.
Akinena kwa nguvu kutoka kwa Mungu, Abinadi aliwaambia watu kuhusu uovu wao. Aliwasomea amri za Mungu.
Aliwaambia Yesu Kristo angezaliwa duniani. Yesu angefanya iwezekane kwa watu kutubu, kufufuka, na kuishi na Mungu.
Abinadi aliwaambia watu watubu na kuamini katika Yesu Kristo au sivyo wasingeokolewa.
Mfalme Nuhu na wengine wote isipokuwa mmoja wa makuhani wake walikataa kumwamini Abinadi. Nuhu aliwaambia makuhani kumuua Abinadi. Walimfunga na kumtupa gerezani.
Kuhani mmoja aliyemwamini Abinadi aliitwa Alma. Alimuomba mfalme Nuhu kumruhusu Abinadi aende.
Mfalme alimkasirikia Alma na akamfukuza. Kisha akatuma watumishi wake kumuua. Alma alikimbia na kujificha, na watumishi wa mfalme hawakumpata.
Baada ya kukaa kwa siku tatu gerezani, Abinadi aliletwa tena mbele ya Mfalme Nuhu. Mfalme alimwambia Abinadi kukanusha alichokisema dhidi yake na watu wake.
Mfalme Nuhu alimwambia Abinadi kwamba kama hatakanusha yote aliyoyasema, atauwawa.
Abinadi alijua alikuwa amezungumza ukweli. Alikuwa tayari kufa kuliko kukanusha kile Mungu alichomtuma kusema.
Mfalme Nuhu aliamrisha makuhani wake kumuua Abinadi. Walimfunga, wakamchapa kwa mjeledi, na kumchoma moto mpaka kufa. Kabla hajafa, Abinadi alisema Mfalme Nuhu pia angekufa kwa kuchomwa moto.
Baadhi ya Wanefi walimpinga Mfalme Nuhu na kujaribu kumuua. Jeshi la Walamani pia lilikuja kupigana na mfalme na watu wake.
Mfalme na wale waliomfuata walikimbia kutoka kwa Walamani, lakini Walamani waliwashika na kuanza kuwaua. Mfalme aliwaambia wanaume waache famila zao na waendelee kukimbia.
Wengi wa wanaume hawakufanya hivyo. Walitekwa na Walamani.
Wengi wa wanaume ambao walikimbia pamoja na Mfalme Nuhu walihuzunika. Walitaka kurudi na kuwasaidia wake zao na watoto na watu wao.
Mfalme Nuhu hakutaka wanaume warudi kwa familia zao. Aliwaamrisha kubaki pamoja naye.
Wanaume walimkasirikia Mfalme Nuhu. Walimchoma mpaka kufa, kama Abinadi alivyotoa unabii. Kisha wakarudi kwa familia zao.