Sura ya 35
Kapteni Moroni na Pahorani
Kapteni Moroni alifurahi kusikia kwamba Helamani na jeshi lake waliweza kutwaa tena sehemu kubwa ya ardhi ya Wanefi kutoka kwa Walamani.
Lakini Helamani na jeshi lake walihitaji msaada. Hawakuwa na wanajeshi wa kutosha kulinda miji mingi.
Kapteni Moroni aliandika barua kwa Pahorani mwamuzi mkuu na gavana. Alimuomba Pahorani atume wanajeshi zaidi kulisaidia jeshi la Helamani.
Walamani waliuvamia mji wa Wanefi ambao Helamani alikuwa ameuchukua. Waliwauwa wengi wa Wanefi na kuwafukuza waliobaki kutoka kwenye mji.
Akiwa ameukasirikia uongozi wa serikali kwa sababu hawakutuma msaada, Moroni aliandika barua nyingine kwa Pahorani.
Kapteni Moroni aliandika kwamba watu wengi walikuwa wameuwawa kwa sababu Pahorani hakutuma wanajeshi zaidi.
Kwa vile Pahorani hakutuma haraka watu zaidi na chakula, Moroni angechukua jeshi lake mpaka Zarahemla na kuchukua kile jeshi lake lilichokihitaji.
Punde Moroni alipokea barua kutoka kwa Pahorani. Alikuwa na huzuni kwamba Moroni na jeshi lake walikuwa wakiteseka.
Pahorani alimwambia Moroni kwamba kundi la Wanefi waovu walioitwa watu wa mfalme hawakumtaka yeye kuwa mwamuzi mkuu. Walikuwa wamemlazimisha yeye na wale waliomuunga mkono kutoka nje ya Zarahemla.
Pahorani aliongeza kwamba alikuwa akikusanya jeshi kujaribu kuuchukua tena mji wa Zarahemla.
Watu wa mfalme walikuwa wamemchagua mfalme kuwa kiongozi wao na walikuwa wameungana na Walamani.
Pahorani hakuwa na hasira juu ya kile Moroni alichokuwa amekiandika. Alitaka Wanefi kuwa huru pia.
Alimuomba Moroni kuleta watu wachache kumsaidia na akasema kama Moroni angekusanya watu zaidi njiani, jeshi lililoungana lingeweza kuuchukua tena mji wa Zarahemla.
Kapteni Moroni alikuwa na furaha kwamba Pahorani bado alikuwa mwaminifu kwa nchi yake na bado alitaka uhuru kwa ajili ya watu.
Akiwa na watu wachache, Moroni alikwenda kukutana na Pahorani. Alibeba bendera ndogo ya uhuru, na maelfu ya wanaume waliungana nao njiani.
Jeshi la muungano la Moroni na Pahorani lilisonga kuelekea Zarahemla. Walimuua mfalme wa Wanefi waovu na kuwateka watu wake.
Kisha Moroni alituma chakula na wanajeshi 12,000 kusaidia majeshi ya Wanefi. Majeshi haya yaliwafukuza Walamani, na kulikuwa na amani tena katika nchi.