Sura ya 43
Yesu Kristo Anawatokea watu wa Nefi
Wanefi wengi walikusanyika karibu na hekalu kule Neema. Walistaajabishwa na mabadiliko makuu nchini.
Watu walikuwa wakizungumza kuhusu Yesu Kristo na ishara ya kifo chake.
Wakiwa wanazungumza, walisikia sauti tulivu kutoka mbinguni. Ilisababisha mioyo yao kuwaka.
Mara ya kwanza hawakuitambua sauti hiyo, lakini wakati ilipozungumza mara ya tatu, waliielewa.
Sauti ilikuwa ya Baba wa Mbinguni. Ilimtambulisha Yesu Kristo na kuwaambia watu wamsikilize.
Yesu Kristo alishuka chini kutoka mbinguni na kusimama miongoni mwa watu. Walikuwa na uwoga wa kuzungumza kwa maana hawakuelewa kilichokuwa kikitendeka. Walidhania Yesu alikuwa malaika.
Aliwaambia kwamba alikuwa Yesu Kristo, ambaye manabii walisema atakuja.
Yesu aliwaambia watu waje na waguse alama ubavuni mwake na katika mikono na miguu, ambapo alipigiliwa misumari msalabani.
Yesu aliwataka watu wajue kwamba alikuwa Mungu wao na kwamba alikuwa amekufa kwa ajili ya dhambi zao.
Mmoja baada ya mwingine watu waligusa alama ubavuni, mikononi, na miguuni mwa Yesu. Watu walifahamu kwamba alikuwa Mwokozi.
Kisha watu walimsifu Yesu na kuinama miguuni mwake na kumwabudu.
Yesu alimwita Nefi na watu wengine 11 waende kwake. Aliwapa nguvu za ukuhani na kuwafundisha njia sahihi ya kubatiza.
Aliwaambia Wanefi wamwamini, watubu na watii amri. Kama hawangefanya hivyo, hawangeweza kuingia katika ufalme wake.
Aliwafundisha Wanefi jinsi ya kuomba kwa Baba wa Mbinguni. Pia aliwafundisha kuhusu kufunga na akasema wangesamehewa kama wangesameheana.
Baada ya kuwafundisha watu vitu vingi, Yesu aliwaambia waende nyumbani na kufikiria na kusali kuhusu kile alichokuwa amesema.
Wanefi walianza kulia. Hawakutaka Yesu aondoke.
Yesu aliwapenda Wanefi. Aliwaambia wawalete kwake watu waliokuwa wagonjwa au waliokuwa wameumia ili aweze kuwaponya.
Yesu aliwaponya hawa watu. Kila mtu aliinama na kumwabudu.