Sura ya 22
Misheni ya Alma huko Amoniha
Alma alipata wasiwasi kuhusu uovu wa Wanefi, hivyo alichagua kutumia muda wake wote kuhubiri injili. Alimchagua Nefiha kama mwamuzi mkuu badala yake.
Alma alifundisha injili kote nchini. Alipojaribu kuhubiri huko Amoniha, watu hawakusikiliza. Walimfukuza nje ya mji.
Alma alihuzunika kwamba watu wa Amoniha walikuwa waovu sana. Aliondoka kwenda mji mwingine.
Malaika alimtokea na kumfariji Alma. Malaika alimwambia arudi tena Amoniha na kuhubiri tena. Alma alirudi haraka.
Alma alikuwa na njaa. Wakati akiingia katika mji, alimuomba mtu chakula. Malaika alikuwa amemwambia mtu huyo kwamba Alma angekuja na kwamba Alma alikuwa nabii wa Mungu.
Mtu huyu, Amuleki, alimpeleka Alma katika nyumba yake na kumlisha. Alma alikaa na Amuleki na familia yake kwa siku nyingi. Alimshukuru Mungu kwa sababu ya familia ya Amuleki na akawabariki.
Alma alimwambia Amuleki kuhusu wito wake wa kufundisha watu wa Amoniha. Amuleki alikwenda pamoja na Alma kufundisha watu. Roho Mtakatifu aliwasaidia.
Alma aliwaambia watu watubu au sivyo Mungu angewaangamiza. Alisema Yesu Kristo angekuja na kuokoa wale waliokuwa na imani kwake na kutubu.
Watu wa Amoniha walikasirika. Walijaribu kumtupa Alma gerezani, lakini Bwana alimlinda.
Amuleki alianza kufundisha. Wengi wa watu walimjua Amuleki; hakuwa mtu mgeni kama Alma alivyokuwa. Aliwaambia kuhusu malaika aliyemuona.
Amuleki alisema Alma alikuwa ni nabii wa Mungu na aliongea ukweli. Watu walishangazwa kusikia ushuhuda wa Amuleki.
Baadhi ya watu walipata hasira, hasa mtu mmoja mwovu aliyeitwa Zeezromu. Walijaribu kumtega Amuleki kwa maswali, lakini aliwaambia alijua kuhusu mpango wao.
Zeezromu alitaka kuharibu kila kitu ambacho kilikuwa chema. Angesababisha matatizo, na kisha watu wangemlipa fedha kutatua matatizo aliyoyatengeneza.
Zeezromu hakuweza kumtega Amuleki, hivyo akataka kumpa fedha ili aseme hakuna Mungu. Amuleki alijua Mungu anaishi na alisema Zeezromu alijua pia lakini alipenda fedha kuliko Mungu.
Kisha Amuleki alifundisha kuhusu Yesu Kristo na kuhusu ufufuo na uzima wa milele. Watu walishangazwa. Zeezromu alianza kutetemeka kwa woga.
Zeezromu alijua kwamba Alma na Amuleki walikuwa na nguvu ya Mungu kwa sababu walijua mawazo yake. Zeezromu aliuliza maswali na kusikiliza wakati Alma akimfundisha injili.
Baadhi ya watu waliwaamini Alma na Amuleki na wakaanza kutubu na kujifunza maandiko.
Lakini sehemu kubwa ya watu walitaka kuwaua Alma na Amuleki. Waliwafunga wote wawili na kuwapeleka kwa mwamuzi mkuu.
Zeezromu alijisikia vibaya kwamba alikuwa mwovu na alifundisha uwongo kwa watu. Aliwaomba watu kuwaacha Alma na Amuleki waondoke.
Zeezromu na watu wengine ambao waliyaamini mafundisho ya Alma na Amuleki walitupwa nje ya mji. Watu waovu waliwarushia mawe.
Kisha watu waovu waliwakusanya wanawake na watoto ambao waliamini na kuwatupa, pamoja na maandiko yao, kwenye moto.
Alma na Amuleki walilazimishwa kuwaangalia wanawake na watoto wakifa katika moto. Amuleki alitaka kutumia nguvu za Mungu kuwaokoa.
Lakini Alma alimwambia Amuleki kwamba asizuie mauaji kwa sababu watu waliokuwa wakifa punde wangekuwa na Mungu na watu waovu wangeadhibiwa.
Mwamuzi mkuu aliwapiga Alma na Amuleki mara kadhaa na kuwadhihaki kwa sababu hawakuwasaidia wanawake na watoto waliokuwa wakiungua. Kisha akawatupa gerezani.
Watu wengine waovu walikuja gerezani na kuwatenda mabaya Alma na Amuleki kwa njia nyingi, ikijumuisha kuwashindisha njaa na kuwatemea mate.
Mwamuzi mkuu alisema kama Alma na Amuleki wangetumia nguvu za Mungu kujiokoa, angeamini. Akawapiga vibao tena.
Alma na Amuleki walisimama. Alma akasali na kumuomba Mungu awape nguvu kwa sababu ya imani yao katika Kristo.
Nguvu za Mungu ziliwajaa Alma na Amuleki, na wakazikata kamba ambazo ziliwafunga. Watu waovu waliogopa na kujaribu kukimbia lakini walianguka chini.
Ardhi ilitikisika, na kuta za gereza ziliwaangukia watu waovu. Bwana aliwalinda Alma na Amuleki, na hawakudhurika.
Watu wa Amoniha walikuja kuona nini kilikuwa kimetokea. Wakati walipowaona Alma na Amuleki wakitoka kwenye gereza lililoanguka, walipatwa na woga na wakakimbia.
Bwana alimwambia Alma na Amuleki waende Sidoni. Huko waliwakuta watu wenye haki. Zeezromu pia alikuwa huko na alikuwa mgonjwa sana.
Zeezromu alikuwa na furaha kuwaona Alma na Amuleki. Alikuwa na wasiwasi kwamba walikuwa wameuwawa kwa sababu ya alichokifanya. Aliwaomba wamponye.
Zeezromu aliamini katika Yesu Kristo na alikuwa ametubu dhambi zake. Wakati Alma aliposali kwa ajili yake, Zeezromu aliponywa mara moja.
Zeezromu alibatizwa na alianza kuhubiri injili. Wengine wengi nao pia walibatizwa.
Watu waovu wa Amoniha wote waliuwawa na jeshi la Walamani, kama Alma alivyotoa unabii.