Sura ya 25
Haruni Anamfundisha Baba wa Mfalme Lamoni
Roho aliwaongoza Haruni na wenzake hadi nchi ya Nefi kumfundisha baba wa Lamoni, mfalme wa Walamani wote.
Haruni alimwambia mfalme kuwa alikuwa kaka yake Amoni. Mfalme alikuwa akifikiria kuhusu ukarimu wa Amoni na kuhusu kile ambacho Amoni alikuwa amemwambia.
Haruni alimuuliza mfalme kama aliamini katika Mungu. Mfalme alisema hakuwa na uhakika lakini angeamini kama Haruni angesema kuna Mungu. Haruni alimhakikishia mfalme kwamba Mungu yu hai.
Haruni alimsomea mfalme maandiko. Alimfundisha kuhusu Uumbaji wa dunia, Anguko la Adamu, na misheni ya Yesu Kristo.
Mfalme aliuliza kile ambacho alihitaji kufanya ili apate Roho Mtakatifu na awe tayari kuishi na Mungu. Mfalme alikuwa tayari kufanya chochote, hata kuacha ufalme wake.
Haruni alimwambia mfalme kwamba alihitaji kutubu dhambi zake kikamilifu. Alihitaji kusali na kuwa na imani kwa Mungu.
Mfalme alisali aweze kujua ikiwa kweli Mungu yupo. Alisema angetubu dhambi zake zote.
Mfalme alianguka sakafuni na akaonekana kama amefariki. Wakati malkia alipomwona, alidhani ya kwamba Haruni na wenzake walikuwa wamemuua.
Malkia aliwashurutisha watumishi wake wawaue Haruni na wenzake, lakini watumishi waliogopa. Aliwatuma wakawatafute watu wengine ambao wangefanya hivyo.
Kabla ya umati mkubwa kukusanyika na kusababisha usumbufu, Haruni aliuchukua mkono wa mfalme na kumuambia asimame. Mfalme alisimama.
Mfalme alimtuliza mkewe na watumishi waliokuwa wamejawa hofu na kisha akawafundisha injili. Wote waliamini katika Yesu Kristo.