Sura ya 5
Safari ya Nyikani
Bwana aliwataka wana wa Lehi wawe na wake ambao wangewafundisha watoto wao injili. Alimwamuru Lehi kuwatuma wanawe kurudi Yerusalemu kuileta familia ya Ishmaeli.
Nefi na kaka zake walirudi Yerusalemu. Walimwambia Ishmaeli kile Bwana alichomtaka afanye. Ishmaeli aliwaamini, na yeye pamoja na familia yake waliondoka pamoja na wana wa Lehi.
Wakiwa wanasafiri nyikani, Lamani, Lemueli, na wengine wa familia ya Ishmaeli walikasirika. Walitaka kurudi Yerusalemu.
Nefi aliwakumbusha Lamani na Lemueli kuhusu yale yote ambayo Bwana alikuwa amewatendea. Aliwaambia wawe na imani kubwa zaidi. Walimkasirikia Nefi lakini hawakurudi Yerusalemu.
Nefi, kaka zake, na Zoramu baadaye waliwaoa mabinti wa Ishmaeli.
Bwana alimwambia Lehi aendelee na safari yake. Asubuhi iliyofuata Lehi aligundua mpira wa shaba ulioitwa Liahona nje ya hema lake. Uliashiria wapi pa kuelekea nyikani.
Familia ya Lehi walikusanya chakula na nafaka na kuyapakia mahema yao. Walisafiri nyikani kwa muda wa siku nyingi, wakifuata maelekezo ya Liahona.
Nefi na kaka zake walitumia pinde na mishale kuwindia chakula wakiwa safirini.
Upinde wa Nefi uliokuwa umetengenezwa kwa chuma ulivunjika, na pinde za kaka zake zilikuwa zimelegea. Kaka zake hawakuweza kuwinda wanyama wowote, kwa hivyo kila mtu alihisi njaa. Lamani na Lemueli walikuwa na hasira.
Nefi alitengeneza upinde kutokana na mbao na kumuuliza baba yake mahali ambapo angelikwenda kuwinda. Lehi alipokea maelezo katika Liahona. Nefi alifuata maelezo na akapata wanyama kadhaa.
Liahona ilifanya kazi tu wakati familia ya Lehi ilikuwa aminifu, yenye bidii, na tiifu.
Nefi alirudi na wale wanyama aliokuwa amepata. Wote walifurahia kupata chakula. Walihuzunika kwamba walikuwa na hasira, na walimshukuru Mungu kwa kuwabariki.
Safari haikuwa rahisi Mara nyingi familia ya Lehi walikuwa wenye uchovu, wenye njaa, na kiu. Ishameli alifariki na mabinti zake walihuzunika. Walinung’unika dhidi ya Lehi.
Lamani na Lemueli pia walinung’unika. Hawakuamini kwamba Bwana alikuwa amezungumza na Nefi. Walitaka kuwaua Lehi na Nefi ili warudi Yerusalemu.
Sauti ya Bwana iliwazungumzia Lamani na Lemueli. Iliwaambia wasiwakasirikie Lehi na Nefi. Lamani na Lemueli walitubu.
Familia ya Lehi iliendelea na safari yao ngumu. Mungu aliwasaidia na kuwaimarisha. Watoto walizaliwa. Lehi na Saria walipata wana wawili zaidi, walioitwa Yakobo na Yusufu.
Baada ya kusafiri nyikani kwa miaka minane, familia ya Lehi iliwasili katika eneo la pwani. Hapo walipata matunda na asali. Waliliita eneo lile Neema.