Sura ya 23
Amoni: Mtumishi Mkuu
Wana wanne wa Mosia waliondoka Zarahemla kwenda kufundisha Walamani injili. Kila mmoja alikwenda katika mji tofauti.
Amoni alikwenda katika nchi ya Ishmaeli. Alipokuwa akiingia kwenye mji, Walamani walimfunga kamba na wakamchukua mpaka kwa mfalme, Lamoni.
Amoni alimwambia Mfalme Lamoni kwamba alitaka kuishi kati ya Walamani. Lamoni alifurahi na akawaambia watu wake wamfungue Amoni.
Amoni alisema angekuwa mmoja wa watumishi wa mfalme. Mfalme alimtuma aende kuchunga mifugo.
Siku moja wakati Amoni na baadhi ya watumishi wengine walikuwa wakipeleka mifugo kunywa maji, Walamani wezi waliitawanya mifugo na kujaribu kuiiba.
Watumishi waliokuwa na Amoni waliogopa. Mfalme Lamoni alikuwa amewauwa watumishi wake wengine waliopoteza mifugo.
Amoni alijua hii ilikuwa ni fursa ya kutumia nguvu za Bwana kuvutia mioyo ya Walamani. Kisha wangesikiliza mafundisho yake.
Amoni aliwaambia watumishi kwamba kama wangeikusanya mifugo iliyotawanywa, mfalme asingewaua.
Amoni na watumishi wengine haraka waliipata mifugo na kuirudisha katika sehemu ya kunyweshea.
Walamani wezi walirudi tena. Amoni aliwaambia watumishi wengine kuichunga mifugo wakati akipigana na wezi.
Walamani wezi hawakumwogopa Amoni. Walifikiri wangemuua kiurahisi.
Nguvu za Mungu Zilikuwa pamoja na Amoni. Aliwapiga na kuwauwa baadhi ya wezi kwa mawe, kitu ambacho kiliwafanya wezi waliosalia kupata hasira sana.
Walijaribu kumuua Amoni kwa rungu zao, lakini kila mara mwizi aliponyanyua rungu kumpiga, Amoni alikata mkono wa mwizi. Kwa kuogopa, wezi walikimbia.
Watumishi walipeleka mikono iliyokatwa kwa Mfalme Lamoni na kumwambia ambacho Amoni alikuwa amekifanya.
Mfalme alishangazwa na nguvu kuu ya Amoni. Alitaka kumuona Amoni lakini aliogopa kwa sababu alidhani Amoni alikuwa ni Roho Mkuu.
Wakati Amoni alipokwenda ndani kumuona, Mfalme Lamoni hakujua nini cha kusema. Hakuongea kwa muda wa saa moja.
Roho Mtakatifu alimsaidia Amoni kujua nini mfalme alikuwa akiwaza. Amoni alifafanua kwamba yeye hakuwa Roho Mkuu. Alikuwa ni mtu.
Mfalme alimuahidi Amoni chochote alichotaka kama angemwabia ni nguvu gani alitumia kuwashinda wezi na kujua mawazo ya mfalme.
Amoni alisema kitu pekee alichokitaka ni Mfalme Lamoni kuamini kile ambacho angekisema. Mfalme alisema angeamini chochote ambacho Amoni angemwambia.
Amoni alimuuliza Mfalme Lamoni kama aliamini katika Mungu. Mfalme alisema kwamba aliamini katika Roho Mkuu.
Amoni alisema kwamba Roho Mkuu ni Mungu, ambaye aliumba kila kitu mbinguni na duniani, na kwamba anajua mawazo ya watu.
Amoni alisema watu waliumbwa kwa mfano wa Mungu. Pia alisema Mungu alimwita kufundisha injili kwa Lamoni na watu wake.
Akitumia maandiko, Amoni alimfundisha Mfalme Lamoni kuhusu Uumabji, Adamu, na Yesu Kristo.
Mfalme Lamoni alimwamini Amoni na alisali ili kusamehewa dhambi zake. Kisha alianguka ardhini na kuonekana kama mfu.
Watumishi walimbeba mfalme mpaka kwa mke wake na kumlaza kitandani. Baada ya siku mbili watumishi walidhani alikuwa amekufa na walitaka kumzika.
Malkia hakuamini kwamba mume wake alikuwa amekufa. Akiwa amesikia kuhusu nguvu kuu ya Amoni, alimuomba amsaidie mfalme.
Amoni alijua Lamoni alikuwa chini ya nguvu za Mungu. Alimwambia malkia kwamba Lamoni angeamka siku iliyofuata.
Malkia alikaa pembeni mwa Lamoni usiku mzima. Siku iliyofuata Lamoni aliamka na alisema alimuona Yesu Kristo. Mfalme na malkia walijazwa na Roho Mtakatifu.
Lamoni aliwafundisha watu wake kuhusu Mungu na Yesu Kristo. Wale walioamini walitubu dhambi zao na walibatizwa.