Sura ya 2
Ono la Kwanza la Joseph Smith
1820
Joseph Smith na familia yake walimwamini Mungu. Walisoma Biblia pamoja. Wazazi wa Joseph waliwafundisha watoto wao kuwa wema.
Kulikuwa na makanisa mengi sehemu aliyoishi Joseph. Watu wote walitofautiana juu ya kanisa gani lilikuwa sahihi. Joseph hakujua ni kanisa gani la kujiunga nalo. Alitaka kujua ni Kanisa gani lilikuwa la kweli la Yesu Kristo.
Siku moja wakati Joseph alipokuwa na umri wa miaka 14, alisoma katika Biblia kwamba tunapaswa kumwomba Mungu wakati tunapotaka kujua kitu. Joseph aliamua kuomba na kumwuliza Mungu ni kanisa gani angejiunga nalo.
Katika siku nzuri ya majira ya kuchipua, Joseph alikwenda msituni karibu na nyumba yake. Alipiga magoti na kuomba kwa sauti. Alikuwa na imani ya kwamba Baba wa Mbinguni angejibu maombi yake.
Shetani hakutaka Joseph aombe. Alijaribu kumzuia Joseph na kufanya giza kumzunguka. Joseph alikuwa na hofu na hakuweza kuzungumza.
Lakini Joseph hakukoma kuomba. Shetani asingeweza kumzuia.
Kisha Joseph alipata ono. Aliona mwanga wenye mng’aro mzuri, uliomzunguka kote. Aliwaona Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wakisimama juu yake angani. Baba wa Mbinguni alimwonyesha Yesu na akasema, “Huyu ni Mwanangu Mpendwa. Msikilize Yeye!”
Joseph alimwuliza Yesu ni kanisa gani angejiunga nalo. Yesu alimwambia Joseph asijiunge na kanisa lolote kwani yote yalikuwa si sahihi. Hakuna hata moja lililokuwa kanisa Lake. Alimwambia Joseph mambo mengine mengi. Kisha ono likamalizika.
Wakati Joseph aliporudi nyumbani, mama yake alimuuliza kama alikuwa sawa. Joseph alisema alikuwa sawa. Kisha akamwambia mama yake kuwa alikuwa ameona ono. Alimwambia kile alichojifunza katika ono lake.
Joseph pia aliwaambia baadhi ya watu katika mji kuhusu ono lake. Watu hawakumwamini. Walisema alikuwa anasema uongo, na wakawa na hasira na wakawa wakatili kwake.
Joseph daima alisema ukweli kuhusu ono lake. Alijua alikuwa amewaona Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Alijua kwamba hakuna kanisa lolote duniani lililokuwa la kweli.