Sura ya 57
Nabii Anauawa
Juni 1844
Maadui wa Kanisa walimlaumu Joseph Smith kwa matatizo katika Nauvoo, na walitaka yeye na viongozi wengine wakamatwe. Lakini baada ya Joseph kukamatwa, jaji alisema hakuwa amefanya kosa lolote na alimwacha aende zake.
Magenge ya watu wenye fujo yalikuwa na hasira kwamba Joseph Smith alikuwa ameachiliwa. Walitishia kushambulia Nauvoo. Walitishia hata kumpaka lami na kummwagia manyoya mmoja wa majaji. Joseph alimwomba gavana wa Illinois kuyazuia magenge hayo, lakini gavana aliamini uongo wa magenge na hakuyazuia.
Joseph Smith alijua angeweza kuwekwa jela tena, na alikuwa na hofu nduguye Hyrum pia angewekwa jela. Joseph alimwambia Hyrum aichukue familia yake na kwenda mji mwingine, lakini Hyrum asingemwacha ndugu yake.
Joseph Smith alihisi kwamba kama yeye na Hyrum wakiondoka Nauvoo, magenge ya watu wenye fujo yasingewaumiza Watakatifu. Waliamua kwenda upande mwingine wa mto na kujificha. Kisha wangeweza kwenda magharibi ili kupata sehemu nyingine kwa ajili ya waumini wa Kanisa kuishi.
Baadhi ya watu walidhani Joseph Smith alikuwa akikimbia kwa sababu alikuwa anaogopa. Emma Smith, mkewe Joseph, aliwatuma baadhi ya marafiki kumtafuta na kumwomba arudi. Joseph alidhani angeuawa ikiwa angerudi Nauvoo, lakini alifanya kile marafiki zake walichomtaka afanye.
Siku baada ya Joseph na Hyrum kurudi Nauvoo, wao na viongozi wengine wa mji walienda Carthage, mji uliokuwa umbali wa takribani maili 20. Huko Carthage walikamatwa kwa madai ya uongo, na Joseph, Hyrum, na baadhi ya marafiki zao waliwekwa jela hadi pale ambapo kesi itakapoweza kusikilizwa.
Joseph, Hyrum, na marafiki zao walikuwa jela kwa siku tatu. Wakati huu, magenge ya watu wenye fujo yaliwatishia na kusema mambo mabaya juu yao. Wakiwa jela, Joseph na marafiki zake waliomba na kusoma Kitabu cha Mormoni. John Taylor aliimba moja ya nyimbo pendwa za Joseph juu ya Yesu.
Kufikia mchana wa tarehe 27 Juni 1844, ni Joseph, Hyrum, John Taylor, na Willard Richards pekee ndio waliokuwa bado katika jela ya Carthage. Kama yapata saa kumi na moja, genge la watu wenye fujo la zaidi ya watu 100 lilivamia jela. Baadhi ya washiriki wa genge hilo walipiga risasi kwenye madirisha, na wengine walikimbia mbele na kuwapita walinzi na kupanda juu kwa ngazi mpaka kwenye chumba ambapo Joseph na marafiki zake walikuwemo.
Ndugu hawa walijaribu kufunga mlango, lakini kulikuwa na watu wengi mno kwa wao kuweza kujilinda. Genge lilisukuma mlango na kumpiga risasi Hyrum Smith. Wakati Joseph alipoona kwamba Hyrum amekufa, alipiga kelele, “Ee, mpendwa kaka Hyrum!” Genge pia lilimpiga risasi John Taylor, ambaye alijeruhiwa vibaya lakini hakuuawa. Hawakumpiga risasi Willard Richards.
Baada ya Hyrum na John Taylor kupigwa risasi, Joseph Smith alikimbilia dirishani. Alipigwa na risasi mbili zilizorushwa kutoka kwenye mlango wa chumba na risasi ya tatu ilipigwa kutokea nje ya jela. Alilia, “Ee Bwana Mungu wangu!” na kuanguka nje ya dirisha. Nabii alikuwa amekufa. Alikuwa ametoa maisha yake kwa ajili ya injili ya Yesu Kristo.
Miili ya Joseph na Hyrum Smith ilipelekwa Nauvoo, ambapo walizikwa. Familia zao na waumini wengine wa Kanisa walihuzunika sana.
Nabii Joseph Smith alifanya kazi nyingi muhimu. Alitafsiri Kitabu cha Mormoni. Yesu alirejesha Kanisa Lake kupitia yeye. Joseph Smith alituma wamisionari kufundisha injili katika nchi zingine. Aliongoza Watakatifu katika kujenga mji mzuri. Mungu alimpenda Joseph Smith. Watakatifu pia walimpenda. Joseph Smith alifanya mengi kwa ajili ya wokovu wetu wa milele kuliko mtu yeyote isipokuwa Yesu Kristo.