Sura ya 26
Falme Tatu za Mbinguni
Februari 16, 1832
Siku moja Joseph Smith na Sidney Rigdon walikuwa wakisoma Agano Jipya. Agano Jipya lilisema kuwa watu wema watakwenda mbinguni baada ya kufufuliwa. Joseph alijiuliza ikiwa watu wote watakwenda sehemu moja mbinguni.
Mafundisho na Maagano 76, kichwa cha habari cha sehemu
Wakati Joseph na Sidney wakifikiri kuhusu hili, Baba wa Mbinguni aliwapa ono la kupendeza. Katika ono hili waliona mbingu. Walimwona Baba wa Mbinguni na Yesu wakiwa na nuru iliyowazunguka kote. Kisha waliwaona malaika wakimwabudu Baba wa Mbinguni na Yesu.
Mafundisho na Maagano 76, kichwa cha habari cha sehemu
Wakati Joseph na Sidney walipoandika juu ya ono hili, walishuhudia kwamba Yesu Anaishi. Walikuwa wamemwona Yeye! Na walikuwa wamesikia sauti ikisema kwamba Yeye ni Mwana wa Mungu. Sauti hiyo pia iliwaambia kwamba Yesu alikuwa Amekuja duniani ili kuwezesha watu wote kurudi kuishi tena na Baba wa Mbinguni.
Katika sehemu iliyofuata ya ono, Joseph na Sidney waliona mahali ambapo watu huenda baada ya kufufuka. Kuna sehemu tatu, au falme, za watu kwenda mbinguni. Watakatifu wenye haki wanakwenda kwenye ufalme wa selestia wa mbinguni baada ya kufufuka. Ufalme wa Selestia ndipo Baba wa Mbinguni na Yesu wapo.
Wale walio katika ufalme wa selestia waliamini katika Yesu Kristo wakati wa muda wao duniani. Walibatizwa na kumpokea Roho Mtakatifu.
Wale walio katika ufalme wa selestia walikuwa na majaribu mengi wakati walipokuwa duniani, lakini waliyashinda kwa imani katika Yesu Kristo. Walijaribu kwa bidii kutii amri za Mungu, na walitubu walipokosa kutii.
Watakatifu wenye haki watakuwa kama Baba wa Mbinguni na Yesu. Vitu vyote vitakuwa vyao. Wataishi pamoja na Baba wa Mbinguni na Yesu milele.
Baadaye Joseph na Sidney waliona ufalme wa terestria wa mbinguni.
Watu katika ufalme wa terestria walikuwa watu wema duniani, lakini walidanganywa na watu wabaya. Walitii baadhi ya amri lakini hawakuwa hodari katika ushuhuda wao juu ya Yesu.
Ufalme wa terestria pia unajumuisha watu ambao hawakuamini injili pale walipoisikia duniani na kisha kuiamini walipoisikia baada ya kufa kwao.
Watu katika ufalme wa terestria watamwona Yesu. Lakini hawawezi kuishi na Baba wa Mbinguni na Yesu.
Baadaye Joseph na Sidney waliona ufalme wa telestia wa mbinguni. Watu wanaokwenda kwenye ufalme wa telestia hawakuwa waadilifu duniani.
Watu hawa hawakuamini katika Yesu au injili Yake. Hawakuwaamini manabii na hawakutii amri za Mungu.
Watu katika ufalme wa telestia hawatamwona Yesu au Baba wa Mbinguni na hawawezi kuishi pamoja Nao. Hata hivyo, malaika watawatembelea watu hawa, na Roho Mtakatifu atawafundisha.
Watu ambao wanakwenda katika ufalme wa selestia na terestria watafufuliwa wakati Yesu atakapokuja tena duniani. Watu wanaokwenda katika ufalme wa telestia hawatafufuliwa mpaka miaka 1,000 baada ya Yesu kuja tena.
Katika ono hili, Joseph na Sidney pia waliona mahali ambapo watu waovu zaidi watakwenda. Watakuwa pamoja na Shetani. Hawawezi kuwa na Baba wa Mbinguni, Yesu, au Roho Mtakatifu.
Watu ambao watakuwa na Shetani walijifunza kuhusu Yesu na injili Yake walipokuwa duniani. Roho Mtakatifu aliwashuhudia kuhusu Yesu Kristo. Walijua kuwa Aliishi na kwamba Alikufa kwa ajili yetu.
Lakini hawa watu walifanya mambo mabaya sana. Walikataa ukweli na kukaidi nguvu za Mungu. Walimkataa Roho Mtakatifu. Walisema hawakuamini katika Yesu tena. Hawa watu watateseka milele.
Joseph na Sidney waliona mambo mengine katika ono lao, lakini Yesu aliwaambia wasiandike kila kitu walichokiona. Kupitia nguvu za Roho Mtakatifu, Watakatifu waadilifu wanaweza kuona na kujua mambo haya wao wenyewe. Joseph na Sidney walimshukuru Mungu kwa ono hili la kupendeza.