Sura ya 20
Vipawa vya Roho
Machi 8, 1831
Joseph Smith alipokea mafunuo mengi ambayo yalifundisha juu ya Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu ni Roho anayemsaidia Baba wa Mbinguni na Yesu. Roho Mtakatifu hana mwili wa nyama na mifupa.
Kupitia nguvu ya Roho Mtakatifu, Mungu hutoa vipawa maalum kwa waumini wa Kanisa. Hivi huitwa vipawa vya Roho, au vipawa vya kiroho. Kila Mtakatifu ana angalau kipawa kimoja cha roho. Waumini wa kanisa wanapaswa kujifunza kuhusu vipawa vyao na kuvitumia ili kusaidiana. Yesu alimwambia Joseph Smith baadhi ya vipawa hivi.
Baadhi ya Watakatifu wamepewa kipawa cha kujua kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu. Wanajua Yeye alikufa kwa ajili yetu. Watakatifu wengine wanapewa kipawa cha kutambua na kuamini shuhuda za kweli za watu wengine kuhusu Yesu.
Baadhi ya Watakatifu wanapewa kipawa cha kuwa viongozi.
Baadhi ya Watakatifu wanapewa kipawa cha kujua tofauti kati ya roho wa haki na wa uovu. Roho za haki zinatumwa na Mungu na hutufanya tujisikie vizuri. Roho za uovu zinatumwa na Shetani na huleta hisia mbaya.
Baadhi ya Watakatifu hupewa kipawa cha hekima. Kipawa hiki kinawasaidia kufanya maamuzi mazuri na kutumia vizuri maarifa ambayo Baba wa Mbinguni huwapa. Baadhi ya Watakatifu hupewa kipawa cha maarifa. Wale walio na kipawa hiki wanapaswa kuwafundisha wengine na kuwasaidia kufanya maamuzi yenye hekima.
Baadhi ya Watakatifu wanapewa kipawa cha imani ya kuponywa. Wengine hupewa kipawa cha kuponya watu wagonjwa. Roho Mtakatifu huwapa baadhi ya Watakatifu kipawa cha kufanya miujiza. Miujiza huonyesha uwezo wa Mungu.
Baadhi ya Watakatifu wanapewa kipawa cha kuzungumza kwa lugha wasizozijua.
Baadhi ya Watakatifu wanapewa kipawa cha unabii. Kipawa hiki kinawasaidia kujua na kuelewa mambo yaliyotokea katika siku za nyuma, mambo yanayotokea sasa, na mambo ambayo yatatokea katika siku zijazo.
Baadhi ya Watakatifu wamepewa vipawa vingi. Watakatifu wote wanapaswa kutumia vipawa vyao kuwatumikia na kuwabariki wengine.
Askofu anaweza kujua ni vipawa gani kila Mtakatifu anacho. Anajua ni nani watakuwa walimu wazuri. Anajua ni Watakatifu gani wanampenda Mungu na kutii amri.
Watakatifu wenye haki wanapaswa kufanya kazi na kuomba ili kupewa vipawa wanavyohitaji. Vipawa hivi vyote vinatoka kwa Mungu.