Sura ya 3
Malaika Moroni na Mabamba ya Dhahabu
1823–1827
Miaka mitatu ilipita baada ya ono la kwanza la Joseph. Alipokuwa na umri wa miaka 17, Joseph alijiuliza kile ambacho Mungu alimtaka kufanya. Usiku mmoja Joseph aliomba kuhusu hili. Alikuwa na imani kuwa Mungu Angemwambia cha kufanya.
Joseph aliona mwanga mkali katika chumba chake. Malaika alikuwa amesimama katika mwanga. Uso wa malaika uling’ara sana. Alivaa joho zuri jeupe.
Malaika alisema jina lake lilikuwa Moroni. Mungu alikuwa amemtuma kuzungumza na Joseph. Moroni alisema Mungu alikuwa na kazi kwa ajili ya Joseph kufanya.
Malaika Moroni alimwambia Joseph kuhusu kitabu. Kitabu hicho kilikuwa juu ya watu ambao walikuwa wakiishi Amerika miaka mingi iliyopita. Yesu Kristo alikuwa amekuja kwa watu hawa na kuwafundisha injili Yake.
Moroni alisema kitabu kiliandikwa kwenye kurasa za dhahabu zilizoitwa mabamba. Kiliandikwa kwa lugha ambayo haijulikani kwetu leo. Mungu alitaka Joseph kutafsiri kitabu kile katika lugha ya Kiingereza.
Malaika Moroni alisema mabamba ya dhahabu yalizikwa katika kilima karibu na nyumba ya Joseph. Moroni alisema kuwa mawe mawili, yaliyoitwa Urimu na Thumimu, yalifichwa pamoja na mabamba. Mawe yangemsaidia Joseph kutafsiri kitabu. Wakati Moroni alipokuwa akizungumza, Joseph aliona ono lililomwonyesha mahali ambapo mabamba hayo yalikuwa yamezikwa.
Moroni pia alimwambia Joseph kuhusu Eliya, ambaye alikuwa nabii mkuu aliyeishi miaka mingi iliyopita. Hadithi ya Eliya inapatikana katika Agano la Kale.
Moroni alisema kuwa Eliya angekuja na kurejesha uwezo maalum wa ukuhani duniani. Uwezo huu ungewezesha familia kuunganishwa pamoja katika hekalu ili waweze kuishi pamoja milele.
Malaika Moroni aliondoka, kisha akarudi tena mara mbili zaidi usiku huo. Alimwambia Joseph mambo mengi kila wakati, kisha akaondoka ilipowadia asubuhi. Joseph aliamka na akaenda kufanya kazi na baba yake shambani.
Joseph alikuwa amechoka sana kufanya kazi, hivyo baba yake akamrudisha nyumbani. Alipokuwa akirudi nyumbani, alianguka chini. Moroni kisha akatokea tena na kurudia kile alichosema wakati wa usiku. Wakati Moroni alipoondoka, Joseph alimwambia baba yake mambo ambayo Moroni alimfundisha. Baba yake Joseph alimwamini. Alijua kwamba Mungu alimtuma Moroni, na alimwambia Joseph kumtii.
Joseph alikwenda kwenye kilima ambapo mabamba ya dhahabu yalikuwa yamezikwa. Aliyapata mabamba katika sanduku la jiwe lililokuwa chini ya mwamba mkubwa. Urimu na Thumimu pia vilikuwemo ndani ya sanduku.
Wakati Joseph alipokuwa katika kilima, malaika Moroni alimjia. Moroni hakumruhusu Joseph kuchukua mabamba. Alimwambia Joseph kuja kwenye kilima siku kama hiyo kila mwaka kwa miaka minne.
Joseph alimtii Moroni na akaenda kwenye Kilima Kumora kila mwaka. Pale Moroni alimfundisha Joseph kuhusu ufalme wa Bwana duniani.
Familia ya Joseph Smith ilikuwa masikini na walihitaji pesa. Joseph alitaka kuisaidia familia yake, hivyo alikwenda kwenye jimbo la Pennsylvania kufanya kazi. Aliishi na mtu mmoja aliyeitwa Bw. Hale.
Bwana Hale alikuwa na binti aliyeitwa Emma. Joseph na Emma walipendana, na baada ya muda walioana. Kisha walirudi kuishi na familia ya Joseph huko New York, ambako Joseph alimsaidia baba yake shambani.
Miezi kadhaa baada ya Joseph na Emma kuoana, Joseph alirudi tena kwenye Kilima Kumora. Miaka minne ilikuwa imepita tangu Joseph alipoona mabamba ya dhahabu kwa mara ya kwanza, na wakati huu Moroni alimruhusu kuyatwaa. Moroni alimwambia Joseph ayatunze vyema mabamba.
Watu wengi walisikia kuhusu Joseph kupokea mabamba ya dhahabu. Walijaribu kuiba mabamba kutoka kwake, lakini aliyaficha mahali ambapo yasingeweza kupatikana. Mungu alimsaidia Joseph kuyatunza vyema mabamba ya dhahabu.
Watu wa eneo hilo walisababisha matatizo mengi kwa Joseph. Walisema uongo kuhusu yeye na familia yake.
Matatizo yalikuwa makubwa sana kiasi kwamba Joseph na Emma waliamua kurudi Pennsylvania, ambako Joseph alitarajia angeanza kutafsiri mabamba kwa amani. Mtu aliyeitwa Martin Harris aliishi karibu na Joseph. Alikuwa mkarimu kwa Joseph na Emma na akawapa fedha ili kuwasaidia kuhama.