Sura ya 63
Waanzilishi Wanaenda Bonde la Salt Lake
Aprili–Julai 1847
Kundi la kwanza la waanzilishi liliondoka winter quarters mnamo Aprili 1847 ili kuanza safari ya magharibi. Wakiongozwa na Brigham Young, kundi lilikuwa na wanaume 143, wanawake 3 na watoto 2.
Wakati wa safari ya kwanza, ardhi ambayo waanzilishi walivuka ilikuwa kwa sehemu kubwa ni tambarare na ilifunikwa na majani marefu. Aina hii ya ardhi inaitwa uwanda. Wahindi waliishi katika uwanda. Hapakuwa na miji au mashamba.
Kila mtu alikuwa na kazi ya kufanya njiani. Wanawake walihudumia watoto na kupika chakula. Wanaume walitengeneza njia, kujenga madaraja, kurekebisha magari ya kukokotwa na maksai, na kutafuta chakula.
Waanzilishi walisafiri siku nzima. Wakati wa usiku waliweka magari yao ya kukokotwa na maksai katika mzunguko na kupiga kambi. Watu na wanyama walikaa ndani ya duara. Waliwasha moto na kupika chakula chao.
Mara nyingi waanzilishi walicheza dansi na kuimba. Moja ya nyimbo walizozipenda ulikuwa “Come, Come, Ye Saints.” Kuuimba kuliwasaidia kuwa na ujasiri wa kukabiliana na changamoto zao. Brigham Young aliwaambia Watakatifu kupumzika na kumwabudu Mungu siku za Jumapili. Watakatifu waliomba, walisoma maandiko, na kufanya mkutano wa sakramenti.
Kila asubuhi saa kumi na moja, mwanamume angepiga tarumbeta ndogo ya kuwaambia waanzilishi ilikuwa ni wakati wa kuamka. Walitakiwa kuomba, kula kifungua kinywa, kulisha wanyama, na kuwa tayari kuanza mwendo ifikapo saa moja kamili.
Waanzilishi walisafiri kwa muda wa miezi minne kuvuka uwanda ule. Walikutana na watu wengine wachache njiani. Baadhi yao walikuwa watega wanyama ambao walimwambia Brigham Young asiende kwenye Milima ya Mawe kwa sababu ingekuwa vigumu kupanda mazao huko.
Watu wengine walimwambia Brigham Young awapeleke Watakatifu California kwa sababu udongo ulikuwa na rutuba na hali ya hewa ilikuwa rafiki. Lakini Brigham Young alisema Bwana alikuwa amemwonyesha mahali ambapo Watakatifu walipaswa kwenda.
Hatimaye waanzilishi walifika Milima ya Mawe, ambapo ilikuwa vigumu sana kusafiri.
Brigham Young aliugua na hakuweza kusafiri haraka sana. Alichagua baadhi ya wanaume kutangulia mbele kwenye Bonde Kuu la Salt Lake na kuanza kupanda mazao.
Wanaume walichukua magari yao ya kukokotwa na maksai juu ya milima. Wakashuka chini katika bonde na kupiga kambi karibu na kijito.
Waliweka wakfu ardhi na kumwomba Bwana kubariki mbegu walizokuwa wanakwenda kuzipanda. Kisha walipanda mbegu.
Siku tatu baadaye, Brigham Young na wengine waliosalia wa kundi lake wakatokeza juu ya milima na kutazama chini bondeni. Wakati Brigham Young alipoliona, alijua hapo ndipo mahali ambapo Bwana alitaka Watakatifu waishi. Alisema, “Hapa ni mahali sahihi. Songa mbele.” Watakatifu waliendesha magari yao ya kukokotwa na maksai kushuka bondeni. Ilikuwa tarehe 24 Julai 1847. Baada ya kusafiri maili 1,000 kuvuka tambarare na milima, Watakatifu hatimaye walikuwa wamepata mahali ambapo wangeweza kuishi. Walishukuru kwamba Mungu alikuwa amewaongoza mahali penye amani na usalama, ingawaje walijua kungekuwa na changamoto nyingi zaidi za kuzishinda.