Sura ya 22
Watakatifu Wanaanza Kuishi Missouri
Julai–Agosti 1831
Nabii Joseph Smith, Sidney Rigdon, Edward Partridge, na wengine walikwenda Missouri. Walikuwa na furaha sana kwenda kwa sababu walitaka kujifunza mengi juu ya kujenga mji wa Sayuni.
Walisafiri sehemu ya safari kwa kutumia mashua. Walipofika Missouri, Joseph alitaka kutembea. Alijua ardhi ya Missouri ilikuwa takatifu, na alitaka kuiona.
Joseph na rafiki zake walitembea karibu maili 300 kupitia Missouri kuelekea Jackson County.
Siku chache baada ya Joseph Smith na rafiki zake kuwasili Jackson County, Watakatifu kutoka New York waliwasili pale.
Wamisionari kutoka Kirtland pia waliwasili Jackson County.
Joseph Smith na Askofu Edward Partridge waliwaambia watu cha kufanya. Baadhi walitakiwa kununua ardhi katika Missouri. Oliver Cowdery na William W. Phelps walipaswa kuanzisha shule. Walipaswa pia kuchagua na kuandika vitabu kwa ajili ya watoto kusoma shuleni.
Joseph alitaka kujua mahali ambapo mji wa Sayuni ulipaswa kujengwa. Aliomba kwa Baba wa Mbinguni, na maombi yake yalijibiwa.
Mafundisho na Maagano 57, kichwa cha habari cha sehemu
Bwana alifunua kwamba mji wa Sayuni ungejengwa katika Jackson County, Missouri. Pia Alifunua kwamba hekalu lingejengwa huko Independence, mji katika Jackson County (ona ramani kwenye ukurasa wa 89). Bwana pia aliahidi kwamba wale ambao watashika amri zake na kuvumilia majaribu kwa uaminifu watavikwa taji la utukufu.
Bwana aliwaambia Watakatifu katika Missouri kwamba walipaswa kutii sheria za nchi. Walipaswa kufanya mambo mengi mema bila kuambiwa. Bwana pia aliahidi kwamba wakati watu wanapotubu, Hatazikumbuka tena dhambi zao.
Bwana alisema kwamba Sidney Rigdon alipaswa kuweka wakfu ardhi. Sidney Rigdon aliwauliza Watakatifu ikiwa walipokea ardhi kwa mioyo ya shukrani na ikiwa waliahidi kushika amri. “Tumefanya hivyo,” walijibu. Kisha Sidney Rigdon aliomba na kuiweka wakfu ardhi.
Siku iliyofuata, Joseph Smith, Oliver Cowdery, Sidney Rigdon, na viongozi wengine walifanya mkutano katika mahali maalum huko Independence. Walisoma maandiko na kuomba. Kisha Joseph Smith aliweka wakfu mahali pale kwa ajili ya ujenzi wa hekalu.
Siku iliyofuata Watakatifu wote katika Missouri walikwenda kwenye mkutano. Walijazwa na Roho Mtakatifu, na wakashangilia. Joseph aliwaambia kwamba Mungu angewabariki ikiwa watakuwa waaminifu.
Siku chache baadaye, Yesu alimpa Joseph ufunuo kuhusu siku ya Sabato, au Jumapili. Yesu alisema Jumapili ni siku Yake takatifu. Jumapili tunapaswa kufanya mambo ya kutusaidia kumkumbuka Yeye. Tunapaswa kupumzika kufanya kazi yetu. Tunapaswa kwenda kanisani na kushiriki sakramenti. Tunapaswa kutubu dhambi zetu. Tunapaswa kufunga na kuomba. Tunapaswa kushukuru kwa baraka zetu zote.
Watakatifu wanaofanya mambo haya watakuwa na vitu vyote vizuri wanavyohitaji. Watakuwa na furaha, watakuwa na amani, na watapokea uzima wa milele.