Sura ya 42
Far West, Missouri
Januari–Julai 1838
Joseph Smith aliondoka Kirtland, Ohio, kwa sababu baadhi ya watu huko walikuwa wakijaribu kumuua. Ilikuwa ni majira ya baridi na ilikuwa baridi kali. Maadui wa Joseph walimfuata, wakiwa wamebeba visu na bunduki.
Ilimbidi Joseph ajifiche. Bwana alimlinda ili maadui zake wasiweze kumpata. Usiku mmoja hata alikaa katika nyumba moja na maadui zake, ambao hawakujua kuwa alikuwa hapo.
Wakati mwingine maadui wa Joseph hawakumtambua walipompita mtaani.
Joseph alisafiri karibu maili 1,000 kuelekea Far West, Missouri. Watakatifu katika Missouri walikuwa wakijenga mji huu baada ya kulazimishwa kuhama sehemu nyingine za jimbo. Walikuwa na furaha kumwona Nabii.
Baadhi ya Viongozi wa Kanisa katika Missouri hawakuwa wakitii amri. Baadhi yao walijaribu kujipatia fedha nyingi. Wakati mwingine walikasirikiana na kuzozana juu ya jinsi ya kuwaongoza Watakatifu. Baadhi yao walikuwa hata na hasira na Joseph Smith.
Oliver Cowdery, David Whitmer, na watu wengine walitengwa. Hii ina maana uumini wao Kanisani uliondolewa. Joseph alikuwa na huzuni kwa sababu watu hawa walikuwa marafiki zake.
Watu wengine walichaguliwa ili kuongoza Kanisa katika Far West. Mara Kanisa lilianza kusitawi tena katika eneo hilo.
Mnamo Mei 1838, Nabii na rafiki zake walikuwa wakitafuta maeneo mengine kwa ajili ya Watakatifu kujenga miji. Siku moja walifika mahali maalum, ambapo Yesu alisema palijulikana kama Adam‑ondi-Ahman. Yesu aliwahi kuzungumza na Adamu huko. Adamu alikuwa ameileta familia yake pamoja huko na kuwabariki kabla ya kufa. Siku moja Yesu na Adamu na watu wengine wenye haki watakutana huko tena.