Sura ya 8
Kuwa Tayari kwa ajili ya Kanisa la Yesu Kristo
Apili 1830
Ilikuwa karibu na wakati wa Kanisa la Yesu Kristo kurudi tena duniani. Yesu alimpa Joseph Smith ufunuo ili watu waweze kuwa tayari kwa ajili ya Kanisa Lake. Yesu alifunua mengi kuhusu injili Yake na kuhusu mambo mengine ambayo watu walipaswa kujua kabla ya Kanisa Lake kuanzishwa.
Yesu alisema Kitabu cha Mormoni kinafundisha injili Yake na kinashuhudia juu ya Mungu na kazi Yake. Yesu aliahidi baraka kwa wale wanaopokea kitabu katika imani—na adhabu kwa wale wanaokikataa.
Yesu alielezea kuhusu maisha Yake hapa duniani. Baba wa Mbinguni alimtuma hapa kuwa Mwokozi wetu. Shetani alimjaribu, lakini Yesu hakuweza kumsikiliza.
Yesu alihisi huzuni kubwa kwa mambo mabaya ambayo watu hufanya. Kuelekea mwisho wa maisha yake, Aliteseka na kumwaga damu kwa ajili ya watu wote. Watu hawatateseka kama Yeye alivyoteseka ikiwa watatubu.
Watu waovu walimweka Yesu juu ya msalaba na kumuua.
Marafiki wa Yesu waliweka mwili Wake katika kaburi.
Baada ya siku tatu, Yesu alifufuka. Alikuwa hai tena!
Kwa sababu Yesu alifufuka, watu wote watafufuliwa. Kwa sababu aliteseka na kufa kwa ajili ya dhambi za watu wote, tunaweza kusamehewa ikiwa tutatubu. Tutarudi kuishi na Baba wa Mbinguni ikiwa tutakuwa na imani, tutatubu, kubatizwa, na kufanya kadiri tuwezavyo ili kutii amri.
Yesu pia aliwafundisha watu kuhusu ubatizo. Alisema ni lazima wabatizwe ili kuwa waumini wa Kanisa Lake. Wale wanaotaka kubatizwa lazima watubu. Lazima wampende na kumtii Yesu. Lazima pia wawe angalau na umri wa miaka minane.
Yesu alifundisha njia sahihi ya kubatiza. Alisema kuhani katika Ukuhani wa Haruni au mtu ambaye ana Ukuhani wa Melkizedeki wanaweza kumbatiza mtu. Mwanamume anamchukua mtu ndani ya maji na anasema ombi maalum.
Mwanamume ambaye anabatiza anamzamisha mtu ndani ya maji. Kisha anamtoa mtu nje ya maji.
Wakati watu wanapobatizwa, wanaahidi kumtii Yesu. Wao pia wanaahidi kusema na kufanya mambo mema.
Yesu alisema kuhusu kubariki watoto. Wanaume ambao wana Ukuhani wa Melkizedeki wanaweza kubariki watoto. Wanaume wanamshikilia mtoto katika mikono yao, na mwanamume mmoja anampa mtoto jina na baraka.
Yesu alisema kuhusu sakramenti. Alisema tunapaswa kupokea sakramenti mara kwa mara. Lakini ikiwa tutafanya jambo baya, hatupaswi kupokea sakramenti mpaka tuwe tumetubu.
Tunapokea sakramenti kumkumbuka Yesu. Mkate unatusaidia kufikiria juu ya mwili Wake. Tunakumbuka kwamba Alikufa msalabani kwa ajili yetu.
Maji yanatusaidia kufikiria juu ya damu ya Yesu. Tunakumbuka kwamba aliteseka na kumwaga damu kwa ajili yetu katika Bustani ya Gethsemane.
Tunafanya maagano wakati tunapopokea sakramenti. Agano ni ahadi. Tunaahidi kwamba tutajaribu kuwa kama Yesu. Tunaahidi kwamba daima tutamkumbuka Yeye. Pia tunaahidi kutii amri Zake. Kama tunayashika maagano yetu, tumeahidiwa kwamba Roho Wake atakuwa pamoja nasi.