Fumbo la Tatu
Mwana Aliyepotea
Mtu alikuwa na wana wawili. Mtu yule aliahidi kuwapa pesa zake pale atakapokufa. Mwana mdogo hakutaka kungojea. Alimsihi baba yake ampe sehemu yake ya pesa. Baba yake alimpa.
Mwana huyu alichukua pesa na kuondoka nyumbani. Alienda kwenye nchi nyingine. Mwana huyu alitenda dhambi tena na tena. Alitumia pesa zote.
Mwishowe mwana huyo hakuwa na pesa za kununua chakula. Alikuwa na njaa sana. Alimwomba mtu msaada. Mtu huyo alimwajiri kuwalisha nguruwe wake.
Mwana yule alikuwa na njaa sana kiasi kwamba alitaka kula chakula cha nguruwe. Alijua kwamba watumishi katika nyumba ya baba yake walikuwa na chakula kizuri sana cha kula kuliko alichokuwa nacho.
Aliamua kutubu na kusihi awe mtumishi katika nyumba ya baba yake. Mwana yule alipoenda nyumbani, baba yake alimuona akija.
Baba alikimbia kukutana na mwanaye. Alimkumbatia na kumbusu.
Mwana yule alimwambia baba yake kwamba alikuwa ametenda dhambi. Alihisi hakustahili kuitwa mwanaye.
Baba alimwambia mtumishi alete nguo nzuri zaidi na kumvisha mwanaye. Mtumishi alimvisha viatu miguuni na pete kwenye kidole chake.
Baba alimwambia mtumishi aandae karamu. Alitaka kila mtu asherehekee. Mwana aliyekuwa ametenda dhambi alikuwa ametubu na kurudi nyumbani.
Mwana mkubwa alikuwa akifanya kazi shambani. Aliporudi nyumbani, alisikia muziki na dansi. Mtumishi alimwambia kwamba nduguye mdogo alikuwa amerudi nyumbani. Baba yake alitaka kila mtu asherehekee.
Mwana mkubwa alikasirika na hakwenda ndani ya nyumba. Baba yake alitoka nje kuzungumza naye.
Baba alikuwa na shukrani kwamba mwana mkubwa daima alibaki naye. Kila kitu ambacho baba alikuwa nacho kingekuwa chake. Baba pia alisema kwamba ilikuwa sawa kusherehekea. Alikuwa na furaha mwanaye mdogo alikuwa ametubu na kurudi nyumbani.
Yesu aliwaambia Mafarisayo mafumbo hayo matatu kwa sababu aliwataka wajue ni kiasi gani Baba wa Mbinguni anavyompenda kila mtu. Anawapenda watu wanaomtii. Anawapenda wenye dhambi pia, lakini Baba wa Mbinguni hawezi kuwabariki hadi watubu. Anawataka wenye dhambi watubu na wamrudie Yeye. Na anatutaka sisi tuwasaidie kufanya hivyo na kuwa na furaha pale wanaporudi.