Sura ya 49
Sakramenti ya Kwanza
Kila mwaka Wayahudi walikuwa na karamu iliyoitwa Pasaka. Iliwasaidia Wayahudi kukumbuka kwamba Mungu alikuwa amewaokoa mababu zao katika siku za Musa.
Yesu na Mitume Kumi na Wawili walihitaji mahali pa kula karamu ya Pasaka. Mwokozi aliwatuma Petro na Yohana kutafuta chumba na kuhakikisha kwamba kila kitu kilikuwa tayari kwa ajili ya karamu.
Walipata chumba na kuandaa karamu.
Yesu na Mitume wote walienda pale. Walikula karamu ya Pasaka pamoja.
Yesu aliwapa Mitume Wake sakramenti kwa mara ya kwanza. Alichukua mkate mikononi Mwake, akaubariki, na kisha akaumega vipande vipande. Aliwaambia Mitume wale mkate.
Yesu aliwaambia wafikirie juu ya mwili Wake wakati wakila mkate. Aliwasihi wakumbuke kwamba angekufa kwa ajili yao.
Yesu alimimina divai katika kikombe. Alibariki divai na kuwaambia Mitume wainywe.
Yesu aliwaambia wafikirie juu ya damu Yake wakati walipokunywa divai. Aliwasihi wakumbuke kwamba angemwaga damu na kuteseka kwa ajili ya dhambi za watu wote.
Yesu pia aliwaambia Mitume kwamba watu waovu punde wangemwua. Mitume Kumi na Mmoja walikuwa na huzuni sana. Walimpenda Mwokozi na hawakutaka afe. Yesu alijua kwamba mmoja wa Mitume angewasaidia wale watu waovu. Jina lake lilikuwa Yuda Iskariote.